76
1 http://www.fortunecity.com/victorian/abbey/313/ukweli.html UKWELI NI HUU (KUUSUTA UWONGO) Aman Thani Fairooz Dibaji Kitabu Hichi Ukweli Ni Huu (Kuusuta Uwongo) Utukufu Na Neema Ya Zanzibar Zanzibar Na Ubaguzi Kabla Ya Mavamizi Ubaguzi Umeanzishwa Zanzibar Wakati Wa Serikali Yenye Kujiita Ya "Mapinduzi" Elimu Na Matibabu Bure! Taalimu Matibabu Hali Za Maisha Neema Zilikuwepo Kuanza Harakati Za Siasa Sheikh Ali Muhsin Kwenda Nchi Za Ulaya Ikiwemo Na Uingereza Kupigania Uchaguzi Wa "Common Roll" (Mtu Mmoja Kura Moja). Kuasisiwa HizbulWattan (Zanzibar Nationalist Party) Wakoloni Dhidi Ya Hizbu, Uhuru Na Umoja Wa Zanzibar Makao Makuu Ya Hizbu Hizbu Kumleta Zanzibar Seyyid AbdulRahman (Babu) Natija Ya Safari Ya Sheikh Ali Muhsin Wakoloni Na Nyerere Ndio Waasisi Wa AfroShirazi Uchaguzi Wa Mwanzo Juni 1957 Kwanini Sheikh Ali Muhsin Aliamua Kusimama N'gambo Badala Ya Majumba Ya Mawe? Kwenye Shari Huzaliwa Kheri Kukuwa Kwa Harakati Za Siasa Ati Husemwa Kuwa Hizbu Imefeli! Kugawanyika Kwa AfroShirazi Kuasisiwa Kwa Zanzibar And Pemba Peoples' Party (ZPPP) Tume Ya Sir Hillary Blood Uchaguzi Wa Pili, Januari 1961 Uchaguzi Wa Tatu Juni 1961 Ushirikiano Wa ZNP/ZPPP Kutokufaulu Mazungumzo Ya Mwanzo Ya Katiba Ya Uhuru AfroShirazi Iliandaa Machafuko Siku Ya Uchaguzi Muungano Wa ZNP/ZPPP, Waunda Serikali Kutokufaulu Mazungumzo Ya Mwanzo Ya Katiba Ya Uhuru Babu Kutoka Katika Hizbu Dhamiri Za Babu Kufungwa Gerezani Kwa Seyyid AbdulRahman Babu Kutolewa Gerezani Babu Babu Na Fisadi Yake Ya Mwisho Kipi Kilicho Mpelekea Babu Kuchukua Khatua Kama Hizo Uchaguzi Wa Julai 1963 Nyerere Anasema Wakoloni Walipendelea Kuiacha Serikali Ya Zanzibar Mikononi Mwa Hizbu Mkutano Wa Katiba Ya Uhuru. Uhuru Wa Zanzibar Sherehe Za Uhuru Yaitwayo "Mapinduzi" Kuuliwa Kwa Muhsin, Suleiman Na Ahmed

Ukweli Ni Huu

Embed Size (px)

Citation preview

http://www.fortunecity.com/victorian/abbey/313/ukweli.html UKWELI NI HUU (KUUSUTA UWONGO) Aman Thani Fairooz Dibaji Kitabu Hichi Ukweli Ni Huu (Kuusuta Uwongo) Utukufu Na Neema Ya Zanzibar Zanzibar Na Ubaguzi Kabla Ya Mavamizi Ubaguzi Umeanzishwa Zanzibar Wakati Wa Serikali Yenye Kujiita Ya "Mapinduzi" Elimu Na Matibabu Bure! Taalimu Matibabu Hali Za Maisha Neema Zilikuwepo Kuanza Harakati Za Siasa Sheikh Ali Muhsin Kwenda Nchi Za Ulaya Ikiwemo Na Uingereza Kupigania Uchaguzi Wa "Common Roll" (Mtu Mmoja Kura Moja). Kuasisiwa HizbulWattan (Zanzibar Nationalist Party) Wakoloni Dhidi Ya Hizbu, Uhuru Na Umoja Wa Zanzibar Makao Makuu Ya Hizbu Hizbu Kumleta Zanzibar Seyyid AbdulRahman (Babu) Natija Ya Safari Ya Sheikh Ali Muhsin Wakoloni Na Nyerere Ndio Waasisi Wa AfroShirazi Uchaguzi Wa Mwanzo Juni 1957 Kwanini Sheikh Ali Muhsin Aliamua Kusimama N'gambo Badala Ya Majumba Ya Mawe? Kwenye Shari Huzaliwa Kheri Kukuwa Kwa Harakati Za Siasa Ati Husemwa Kuwa Hizbu Imefeli! Kugawanyika Kwa AfroShirazi Kuasisiwa Kwa Zanzibar And Pemba Peoples' Party (ZPPP) Tume Ya Sir Hillary Blood Uchaguzi Wa Pili, Januari 1961 Uchaguzi Wa Tatu Juni 1961 Ushirikiano Wa ZNP/ZPPP Kutokufaulu Mazungumzo Ya Mwanzo Ya Katiba Ya Uhuru AfroShirazi Iliandaa Machafuko Siku Ya Uchaguzi Muungano Wa ZNP/ZPPP, Waunda Serikali Kutokufaulu Mazungumzo Ya Mwanzo Ya Katiba Ya Uhuru Babu Kutoka Katika Hizbu Dhamiri Za Babu Kufungwa Gerezani Kwa Seyyid AbdulRahman Babu Kutolewa Gerezani Babu Babu Na Fisadi Yake Ya Mwisho Kipi Kilicho Mpelekea Babu Kuchukua Khatua Kama Hizo Uchaguzi Wa Julai 1963 Nyerere Anasema Wakoloni Walipendelea Kuiacha Serikali Ya Zanzibar Mikononi Mwa Hizbu Mkutano Wa Katiba Ya Uhuru. Uhuru Wa Zanzibar Sherehe Za Uhuru Yaitwayo "Mapinduzi" Kuuliwa Kwa Muhsin, Suleiman Na Ahmed 1

Kifo Cha Ali Mzee Mbalia "Skolashipu" Za Misri Yaliyo Nifika Nafsi Yangu Na Hayo Yenye Kuitwa "Mapinduzi" Maafa Ya Gerezani Kufungwa Kifungo Cha Miaka 10 Gerezani Kiasi Cha Kazi Alichokuwa Akifanyishwa Mfungwa Maovu Waliyotendewa "Wafungwa Wa Kisiasa" Kutolewa Gerezani Nakimbilia DarEsSalaam Mahabusi Wadhulumiwa Wa Mwalimu Nyerere Mateso Ya "Kwa Ba Mkwe" Maisha Ya Gereza Langoni Nyakati Za Kufanyishwa Kazi "Wafungwa Wa Sisasa" Ufungwa Wa Karume Ni Zaidi Ya Utumwa Kurejeshewa Uhuru Wetu Kuuliwa Wananchi Msikitini Kuuliwa Kwa Wananchi Wengine Namna Walivyo Uliwa Wafungwa Waliyokufa Gerezani (1) Mzee Mohammed Mbaba (2) Maalim Harun Ustadh (3) Idi Hassan (4) Ramadhan Ibrahim Saadalla Wameuliwa Vifungoni Wafungwa Wengine Wauliwa "Wafungwa Wa Siasa" Bado Waendelea Kuuliwa Aliyonizungumziya Twala Yalomfika Othman Shariff Kuteswa Na Kuuliwa Othman Shariff Kufungwa Na Kuuliwa Saleh Saadalla Karume Kuanza Kumbadilikia Twala Mwisho Wa Twala Makomred Wamechangia Maafa Yaliopo Nchini Kwanini Mwalimu Nyerere Alikataa Kuwapeleka Zanzibar Watuhumiwa Wa Kesi Ya Ukhaini? Siri Hii Ni Kubwa Sana!! Serikali Ya Mavamizi Ya Zanzibar Bado Imo Na Ubaguzi Wake Nilitakiwa Nitoke Nchini Namna Nilivyoondoka Kuukimbia Wattani Wangu Kuleta Ahli Zangu Dubai Mengineyo Kwa Ufupi Mwalimu Na Uislamu Mwalimu Na Utumwa Porojo La Mitaani Demokrasi Ya Vyama Vingi (MultiParty Democracy) Vipi Kuifikilia Demokrasi Shukrani DIBAJI Namshukuru Mwenye Enzi Mungu Mwenye Wingi wa Rehema Kubwa na Ndogo kuniwezesha kuandika kijitabu hiki ambacho nimejaribu kiasi nilichoweza kuyaeleza yale yaliyotokea katika Nchi yetu, Zanzibar. Na yaliyonitokelea mimi mwenyewe na yaliyowatokelea Wananchi wenzangu kutokana na hayo yenye kuitwa, "Mapinduzi" yaliyofanyika katika Visiwa vyetu mnamo taarikh 12 Januari, 1964. Haya ninayoyaandika ni kiasi ya hayo niyajuayo mimi tu; hapana shaka yapo mengi ambayo sikupata kuyajuwa. Bali nataraji watatokea wenzangu nao, wakayaeleza waliyotendewa au waliyoyaona yakitendwa. 2

Nafanya haya si kwa makusudio yoyote mengine zaidi ya kutaka kueleza ukweli wa yaliyotendeka katika Nchi yetu ili Wananchi wenzangu (na ndugu zetu wa Tanganyika, bali na ulimwengu, pia) na khasa wale waliokuwa wadogo, na wale ambao hawajaja duniani wakati huo waweze kuyafahamu japo kwa uchache yaliyotendeka katika Nchi yao kwa hayo yenyekuitwa "Mapinduzi". Ikiwa katika kuyaelezea haya, kutahitajia kumtaja mtu au watu kwa njia yoyote, itakuwa nafanya hivyo kwa kutokana na maudhui ninayo izungumza wala si kwa ajili ya kusengenya au kukejeli au kudharau au kwa kutia illa za namna fulani, hashaa! Bali kwa vile dhamiri ya kukiandika kijitabu hiki ni kuelezea ukweli wa mambo yalivyokuwa, basi sitochelea kulieleza lolote madhali kwa kufanya hivyo ndio itakuwa natimiliza lengo nililolikusudia, nalo ni kuueleza ukweli. Kutokana na hayo, nachukuwa nafsi yangu masuliya yote yatayotokea katika maandishi haya. Muhimu, nawaomba wasomaji wangu wajishughulishe zaidi na hayo niliyokusudia kuyaeleza, kwani hayo hayana shaka yoyote, ni kweli tupu. Na nawaomba wasijishughulishe na makosa madogo madogo, kama vile ya upigaji chapa, makosa ya lugha au juu ya utaratibu wa uwandishi. Ikiwa litatokea suala lolote, au ikiwa lolote halitafahamika, basi wakurejelewa ni mimi. Inshallah, nitajaribu kama nitavyoweza kutanzua kila lililotanzika na ikiwa nitashindwa, basi sitoona taabu kutaka msamaha. Mwenye kukamilika kwa yote ni Mwenye Enzi Mungu. Tunamuomba Mwenye Enzi Mungu ajaaliye haya tunayoyaeleza yapate kusomwa, kuzingatiwa na kufahamika na ipatikane faida ndani yake kwa kutumiwa kwa kheri. Kubwa ya kheri hizo ni kusahihisha palipo haribika, kuiondosha haramu, kuomba toba na kutenda mema, kwani mema huondowa mabaya. Mwenye Enzi Mungu atupe taufiq, Amin. Aman Thani Fairooz P.O. Box 10836 Telephone 04850802 Dubai United Arab Emirates Januari, 1995

3

KITABU HICHI Kidogobasi, Chungutamu. Kwa hakika Kitabu hichi ni kidogo basi. Lakini, kama alivyosema muandishi kuwa kaandika kwa ufupi, bali ufupi wa kutosheleza faida yake. Yoyote atakaye kisoma kitabu hichi kwa kutaka kufahamu na bila ya mawazo yake kudhibitiwa na kupenda au kuchukiya, basi hapana shaka atapata faida. Atafahamu jinsi wananchi wa Zanzibar walivyokuwa katika harakati zao za kuwania uhuru wa nchi yao kutokana na ukoloni wa Muingereza. Harakati ambazo zalianza kabla ya miaka ya 1940. Pia ataweza kufahamu ni nani walioanzisha harakati hizo, namna zilivyopata kuungwa mkono na wananchi na namna zilivyokuwa zikiendeleya. Pia atapata kufahamu jinsi ya pingamizi zilivyokuwa. Atafahamu pingamizi hizo zilivyoanzia, nani aliyezianzisha na kuzipalilia na kuzikuza. Atafahamu natija yake! Pia atafahamu vipi wananchi chini ya uwongozi wa vyama vyao ZNP/ZPPP walivyokuwa wakizikabili pingamizi hizo. Na zaidi atafahamu juhudi za waongozi wa ZNP/ZPPP katika kutaka mafahamiano na ushirikiano na wananchi wenziao ASP na nini ulikuwa muelekeo wa waongozi wa ASP, muelekeo ambao mara nyingi ulikuwa ukiathirika kwa uwongozi na fikra zilizokuwa zikipangwa na kuletwa kutoka nje ya nchi. Chungutamu. Kweli ni chungu! Lakini ni wajibu isemwe na kubainishwa. Uchungu uliyomo ndani ya kitabu hichi ni kuona jinsi wananchi walivyohangaika kwa jasho, mali na hata damu zao kwa kuwania uhuru wao kutokana na ukoloni wa Muingereza, lakini kwa sababu ya husda, chuki na ufisadi uhuru huo haukuachiwa kuishi zaidi ya siku thalathini! Isitoshe, sio kuwa uhuru huo ulipotezwa kwa kutumiliwa njiya za usalama, sivyo, bali kwa fujo! Fujo ambalo natija yake ni kupotezwa Dola ya Zanzibar, roho za wananchi, heshima ya binaadamu, mali za watu na mwisho kuwachwa wananchi kuishi ndani ya haramu. Utamu japo kwa hakika sio utamu ni kwa vile kuweza wananchi kupata kuufahamu UKWELI ambao kwa muda wa zaidi ya miaka thalathini umekuwa ukifunikwa kwa UWONGO. Lakini, kama yalivyo maumbile, kweli daima huibuka. Tunamshukuru Mwenye Enzi Mungu kwa kudhihiri kitabu hichi na kuweza kuufahamisha umma, bali na ulimwengu, maafa yaliofikishiwa Zanzibar, Nchi na Wananchi. Msomaji, na pengine hata asimuliwaye haya, huenda akasema, yaaleiti yalielezwa haya kiasi cha miaka ishirini liyopita, au kabla ya hapo. Hivyo ni kweli! Lakini kila kitu kwa majaaliwa, na kuchelewa kwengine kuna kheri zake kama kwengine kunavyo shari zake. Kheri katika kuchelewa kudhihiri kitabu hichi ni kuwa vijana waliokuwa wadogo wakati wa maafa ya Zanzibar leo ni watu wazima, wenye uwezo wa kufikiri, kuamua na kutenda. Kwa hivyo wanahitajia kuujuwa Ukweli. Wao si kwa ajili ya Kuusuta Uwongo, hashaa!! Bali ni kwa ajili ya kuujuwa ukweli, kisha iwe ni mafunzo kutokana na yaliotendeka. Watasoma, na Inshallah watayafahamu na kuyatumia. Na haya ndio khasa makusudio na faida ya kitabu hichi. Kutumia kwao huko kwanza iwe ni kwa kuepusha yasitendeke tena maafa yaliyotendwa, kufuatilia hilo au yote mawili sambamba ni kwa kufanyakazi katika kujenga palipo bomolewa. Kubomowa daima ni rahisi kuliko kujenga, kujenga kunataka umoja na ushirikano wa kila mmoja wetu. Kwa hivyo ni waajibu wa kila mmoja wetu kushirikiana, bega kwa bega, kwa nia na nguvu moja kufanyakazi kuirejesha Zanzibar. Kwanza, kuirejesha katika ramani ya ulimwengu ili iwe na jina na pahala pake kuwa ni Dola kaamili na iliyo huru. Kisha, bali ndio la muhimu, kuirejesha katika neema zake. Hichi ni kitabu cha kusomwa na kila Mzanzibari, bali na ndugu zetu wa Tanganyika, pia. Abdulla Ali (Baba)

4

UKWELI NI HUU (KUUSUTA UWONGO) Nimelichagua jina hili la UKWELI NI HUU KUUSUTA UWONGO, baada ya kuyasikia na kuyasoma me ngi ya uwongo na hata yakafika kusomeshwa watoto wetu katika maskuli ya Zanzibar kukhusu hayo yenye kuitwa "MAPINDUZI" yaliyofanyika katika visiwa vyetu vya Zanzibar mnamo taarikh 12 Januari 1964. Kabla ya kuingia katika hayo, ningependa ku waambia wasomaji wangu wote kuwa mimi si mjuzi hata kidogo wa fani hii ya uandishi; tena ni mbovu sana katika "spellings" na ka tika "nahau" za Kiswahili cha kisasa. Pia nawaomba radhi kwa Kiswahili changu cha kizamani. Bali, kutokana na huo uzushi na kupotezwa kwa makusudi ukweli wa hayo yaliofanyika kukhusu hayo yenye kuitwa "mapinduzi" nimeona sina budi illa ni kujitolea hivyo hivyo juu ya upungufu wangu katika fani hii ya uandishi. Lakini ukweli lazima niudhihirishe ili vichipukizi vyetu viweze kuyaelewa vilivyo yaliyotendeka katika nchi yao. Kwani wengi walikuwa wadogo na wengine walikuwa hata hawajazaliwa katika wakati huo. Ilivyokuwa Kiswahili ni lugha yangu ya kuzaliwa, basi ninaiandika kama ninavyoisema. Si shughuliki na "kua au kuwa, aliniambia au aliniambiya, ameuawa au ameuwawa kenda au kaenda, amekwenda au ameenda". Hayo kwa wataalamu wa lugha ni mambo muhimu lakini kwa mimi nakutakeni msamaha juu ya hayo. Muhimu ya kuyaangaliya na kuyazingatiya ni yale nikusudiayo kuyaeleza, kwani hayo ndio muhimu na ndio ya kweli tupu isiyokuwa na dosari hata chembe. La mwanzo nitakalo kuombeni mlifahamu uzuri ni ile hakika kuwa hayo yaliyofanyika katika visiwa vyetu taarikh 12 Januari 1964, hayakuwa "MAPINDUZI" wala hayafai hata kidogo kuitwa 'mapinduzi' kwa maana asili ya neno. Bali kwa maana zote yalikuwa khasa ni "MAVAMIZI", yaani kwa Kiingereza "INVASION". Mapinduzi lazima yapangwe, yaongozwe na yatekelezwe na wananchi wenyewe kwa maslaha ya nchi na wananchi wake. Sasa tukiangalia hayo yaliotendeka Zanzibar, yalipangwa, yaliongozwa na yalitekelezwa na WAGENI kutoka nchi za nje za jirani zetu. (Ni wao wala si wananchi ndio waliochukua ngawira kubwa kubwa). Haya yanathibitika zaidi kwa vile kuwa huyo jamadari aliyeyaongoza hayo 'mavamizi' ni John Okello na wa chini yake walikuwa Injini na Mfaranyaki. Nani kati ya hao aliyekuwa kitovu chake kimezikwa visiwani? Okello amezaliwa na amekulia kwao Uganda, Injini amezaliwa na amekuliya kwao Kenya na Mfaranyaki amezaliwa na amekuliya kwao Tanganyika. Wote hao walikuja Zanzibar wakiwa watu wazima na shughuli zao, wamekuja kutafuta kibarua na kukimbia kodi za kichwa katika nchi zao. Liangalie hilo waliloliita "Baraza la Mapinduzi". Utaona sehemu kubwa ya wanachama wa Baraza hilo walikuwa si Wazanzibari, laa kwa kuzaliwa wala kwa kuchukua Tajnisi (Kuandikisha Uraia). John Okello, Khamis Darweshi, Seif Bakari, Said Natepe, Said Washoto, Muhammed Mfaume, Edington Kisasi, Mohammed Abdalla Kaujore. Ukiwaacha wengineo ambao nao vile vile walikuwa si wananchi wa Zanzibar kwa kuzaliwa, bali wao walikuja Zanzibar wakiwa katika migongo ya wazee wao na waliendelea kuishi humo visiwani kwa maisha yao yote. Na wakachukuliwa kama ni Wazanzibari. UTUKUFU NA NEEMA YA ZANZIBAR Mwenyezi Mungu amevipa visiwa hivi viwili yaani Unguja na Pemba bahati ya utukufu kwa kila jambo lake. Hayo yaliendelea tokea karne na karne mpaka pale ulipotendwa ufisadi wa taarikh 12 Januari 1964, ndipo neema na utukufu wa Zanzibar ulipoanza kutoweka. Hapo tena, badala ya zumari kuwa likipulizwa Zanzibar, watu wa maziwani (Bara) walikuwa wakihemkwa, ikawa linapulizwa Bara, tuliopo visiwani tunahemkwa! ZANZIBAR NA UBAGUZI KABLA YA MAVAMIZI Nathubutu kusema bila ya wasiwasi wowote kuwa Zanzibar hakukuwepo ubaguzi wa namna yoyote kwa maana khasa na ya wazi ya neno UBAGUZI. Kwanza Wazanzibari ni watu waliochanganya sana damu hata sio rahisi kuweza kumtambua mtu kuwa ni mwenye kutokana na asili ya kabila fulani kwa kuangalia rangi yake au pua yake au masikio yake au kimo chake au kwa jina lake. Jee, watu hao watabaguana namna gani? Malipo ya wafanyakazi serikalini yalikuwa hayakupangwa kiukabila. Wala serikali haikuwa na sehemu maalumu katika maskuli wala katika mahospitali kuwa zimetengwa kwa ajili ya watu wa makabila fulani.

5

Katika nchi za jirani zetu, Tanganyika, Kenya na Uganda kote huko kulikuwepo na ubaguzi uliyokuwa ukiongozwa na serikali za nchi hizo. Malipo ya mishahara ya wafanyakazi yalikuwa yakilipwa kutokana na makabila yao wala si kutokana na ujuzi wao wa kazi. Kulikuwepo "African Scale, Asian Scale na European Scale". Madaktari, Mainjinia, Waalimu na wowote nawawe wana elimu na ujuzi na maarifa ya namna moja, yaani wote sawa sawa kwa elimu na ujuzi wa kazi zao, lakini mishahara yao ilikuwa tafauti kutokana na makabila yao. Waafrika ndio wenye kulipwa malipo ya chini kabisa kuliko wote. Wazungu walikuwa ndio wenye kulipwa mishahara minono (hata baadhi yao walikuwa hawana elimu yoyote isipokuwa huwo Uzungu wao), waliowafuatia ni Waasia. Vyoo vya njiani (Public Toilets) na sehemu za kungojelea usafiri wa reli navyo vile vile vilikuwa vikitumika kwa ubaguzi wa kikabila. Waafrika waliekewa vyoo vyao na sehemu zao za kungojelea usafiri. Wazungu walikuwa na sehemu zao na Waasia walikuwa na sehemu zao, wote mbali mbali. Lilikuwa ni kosa na kuvunja sheria ikiwa imetokea kwa yoyote kuingia katika sehemu isiyo kuwa amekhusika nayo. Khasa Muafrika awe ameingia au amekaa katika sehemu za Waasia au za Wazungu. Katika Tanganyika, Kenya na Uganda kote huko kulikuwa na Kodi ya Kichwa. Kodi hiyo ilikuwa ikilipwa na kila mtu aliyekwishafika balegh katika umri wake. Nayo pia ikitekelezwa kwa njia za ubaguzi wa kikabila. Waasia na Wazungu, wao hata ikiwa wamechelewa kulipa kodi zao, basi walikuwa hawakamatwi majiani wala hawaendewi majumbani mwao kukamatwa. Lakini, Waafrika walikuwa wakisakwa majiani na wakiendewa majumbani mwao mnamo pinga pinga za usiku. Na wakikamatwa, basi walikuwa wakifungwa kamba za viunoni au hufungwa ncha ya shati la huyu na la huyu kisha walikuwa wakiongozwa mmoja nyuma ya mmoja na huku wakipigwa mateke na kusukumwa mpaka wakifikishwa Bomani. Huko ikiwa hawatokuwa na cha kulipa basi walikuwa wakihukumiwa na kufungwa. Kutokana na hali kama hizo, ndipo wengi kati ya wananchi wa nchi hizo, khasa kutoka Tanganyika walikimbia kutoka makwao na kuhamia Zanzibar kwa sababu ya kufuata hali njema za kimaisha. Zanzibar hakukuwepo kodi za kichwa wala ubaguzi wa vyooni wala malipo ya mishahara wala wa namna yo yote. Ilikuwa njema atakae naaje. UBAGUZI UMEANZISHWA ZANZIBAR WAKATI WA SERIKALI YENYE KUJIITA YA "MAPINDUZI" Mara tu baada ya kufika hiyo serikali ya 'mavamizi' katika Zanzibar ubaguzi wa ukabila ulianzishwa. Kila "mrangi rangi" kama walivyokuwa wakiwaita wenyewe, yaani wenye asili za Kiarabu, za Kihindi na za Kingazija walianza kutolewa makazini bila ya kupewa hata haki zao za ufanyaji wa kazi. Mashamba, majumba na hata mabiashara yao yalichukuliwa kwa nguvu na kupewa wageni ikiwa ni tunzo la ukatili na maovu waliyowafanyia wananchi katika nchi yao. Serikali ya 'mavamizi' ya Zanzibar ilitangaza rasmi kupitia vyombo vya khabari vya serikali kukhusu ubaguzi katika Taalimu. Waafrika, wakipasi au wasipasi bali idadi yao ya kuingia katika "Form One" ya "secondary school" ilikuwa ni 77 katika mia (77%), Waarabu 16 katika asili mia (16%), Wahindi 6 katika mia (6%), na Wangazija MMOJA katika mia! (1%). Si hayo tu, bali serikali ya 'mavamizi' imetumia fedha za umma kwa ajili ya kujijengea hospitali yao wao tu Wanachama wa Baraza la Mapinduzi na familia zao na wameita, "Mapinduzi Wing". Vitanda, mabetishiti, foronya za mito, vyombo vya kulia kama sahani, vikombe, visu na nyuma (forks) vyote viliagiziwa kutoka Ulaya. Ilikuwa ikitokea Mheshimiwa kulazwa huko, basi na mkewe alikuwa akihamia huko huko na kulala kitanda kimoja kama kwamba wamo katika siku za fungati! Haya yakitendeka wakati wananchi wanyonge hawana hata dawa mahospitalini! Huo ulikuwa ndio usawa, sio ubaguzi! ELIMU NA MATIBABU BURE! Tunaambiwa na serikali yenye kujiita ya 'mapinduzi' kuwa elimu na matibabu yameanza kuwa bure kwa wananchi baada ya kupatikana kwa Serikali ya 'mapinduzi'! Huu ni uwongo uliokuwa hauna hata kifuniko. Toka lini elimu na matibabu yalikuwa kwa malipo katika Zanzibar? Tangu kuanzishwa kwa skuli ya serikali na Sayyid Ali bin Hamoud na toka kuanzishwa kwa matibabu katika mahospitali, kamwe hayajapata kuwa ya malipo. Toka kwa kuangaliwa na madaktari mpaka kwa madawa, chakula, na mpaka kulala kwa kutibiwa katika mahospitali kulikuwa bure. TAALIMU Wananchi na wageni, kuanzia chumba cha kwanza yaani (standard one) mpaka kufikia chumba cha nane (standard eight), masomo yalikuwa bure kwa wote. Sio hivyo tu, kila mwanafunzi alikuwa na deski lake peke yake la kukalia na kila mwanafunzi alikuwa akipewa madaftari ya kuandikia bure, vitabu vya 6

kusomea bure, kalamu za kuandikia bure, vidawa vya wino na wino wake bure hata blotting papers (la kukaushia wino) pia wakipewa bure. Na kila Ijumaa wanafunzi walikuwa wakipewa sabuni za kufulia bure. Skuli za mashamba, wanafunzi walikuwa wakipewa kifungua kinywa kunde na uji kabla ya kuingia katika vyumba vya masomo, bure. Kuanzia chumba cha tisa mpaka cha 12, na baada ya muda katika miaka ya 1950 kuanzia chumba cha saba mpaka cha 12, wazee walitakiwa wasaidie kitu kidogo katika masomo ya watoto wao. Malipo hayo yalikuwa ya kitu kidogo sana na si kila mzee alikuwa akilipa ada hizo. Wengi sana katika wazee walikuwa hawalipi hata senti moja. Na hao waliokuwa wakilipa, wengi wao walikuwa wakilipa kuanzia Shs. tano mpaka Shs. 20 kwa wingi kila baada ya miezi mitatu au mine. Kabla ya mzee kuwa alipe au asilipe, kulikuwepo taratibu maalumu zilizokuwa zikifanywa. Mzee wa mtoto alikuwa akipelekewa "questionnaire" (karatasi) yenye masuala yaliyokhusu mapato yake, kazi yake na idadi ya watu wake wa nyumbani. Kwa kutaka kuhakikisha uwezo wa mzee huyo, basi akipelekewa waraka huo kwanza Sheha wa mtaa kuhakikisha yale yalioandikwa na akisha Sheha humpelekea Mudiri wake na Mudiri humpelekea D.C. wake. Baada ya khatuwa hizi ndio tena hapo hutolewa uamuzi wa kulipa au wa kutokulipa, na kama kulipa alipe kiwango gani. Kutokana na mipango kama hiyo, zaidi ya 70 katika mia (70%) ya wazee watoto wao walikuwa wakisoma bila ya kulipiwa kitu chochote na kiasi cha 20 katika mia (20%) walikuwa wakilipiwa kitu kidogo na kiasi cha 10 katika mia (10%) ndio waliyokuwa wakilipiwa idadi kamili ambayo ilikuwa chini ya Shillingi 200, kwa mwaka mzima. Wengi waliokuwa wakilipa kima hicho, walikuwa ni wazee wenye asili za Kihindi. Wanaoitwa Waafrika na wanaoitwa Waarabu hayo yalikuwa si maji yao. Muhimu katika hayo si kulipa au kuto kulipa, muhimu ni thamani (quality) ya elimu iliyokuwa ikipatikana siku hizo, jee leo inapatikana? Hilo ndilo suala muhimu la kujiuliza na kulizingatia. Ikiwa hiyo isemwayo leo kuwa elimu bure, na imekuwa wanafunzi hawana madeski ya kukalia, hawana vitabu vya kusomea, wala chochote cha kusomea, bali zaidi hawana hata walimu wenye ujuzi wa kusomesha; basi bure kama hiyo ni "bure ghali". Kwa hiyo bure, basi watoto wetu leo wametokwa na vibyongo kwa kuinama wakati wa kuandika. Wakirejea kutoka maskuli utadhania wanatoka kuchimba makaburi kwa mavumbi yalivyo watapakaa kwa kusota chini. Elimu bure! Wanafunzi wakipotezewa wakati wao wa masomo kwa kuchezeshwa ngoma za sindimba na kuimbishwa majimbo ya kanisani ati huitwa, "Kwaya". Kuanzia Disemba wanafunzi walikuwa wakianzishwa mazowezi ya kucheza ngoma na kuimba hizo kwaya pamoja na magwaride kwa ajili ya kujiweka tayari kwa sherehe za hayo yenye kuitwa 'mapinduzi' katika mwezi wa Januari. Wakimaliza tu, hawawahi hata kushusha pumzi wanangojewa kwa sherehe za kuasisiwa kwa Chama cha AfroShirazi, 2 2 (February 2). Wakimaliza tu, hawawahi hata kunywa maji, wanazolewa tena kwa mazowezi ya sherehe za "Muungano" April 26. Hawawahi hata kukaa kitako, wanabebwa tena kwa mazowezi ya Sikukuu ya Wafanyakazi "May Day". Hapo hupumua kidogo kisha huzolewa tena kwa mazowezi ya kusherehekea, "Saba Saba", July 7. Hawawahi hata kwenda chafya, hunyakuliwa tena kwa mazowezi ya sherehe za "Elimu Bure"! Septemba. Wakimaliza hapo wanazolewa tena kwa mazowezi ya sherehe za "Uhuru wa Tanganyika" Desemba. Ukiangalia utaona kuwa mwaka mzima badala ya watoto wetu kusomeshwa, walikuwa wakichezeshwa ngoma, kuchezeshwa magwaride na kuimbishwa manyimbo ya kanisani. Bado ati husemwa ELIMU BURE, kweli bure, lakini BURE KWA MJINGA! Kwa kweli kiwango cha elimu Zanzibar kimeanguka kiasi kikubwa sana, kiasi cha kuitwa, "chini ya sufuri". Imefika hadi leo kuwa mwanafunzi aliyemaliza hicho wanachokiita, "kidato cha nne" (Form IV), ukimwambia aandike barua ya kuomba kazi kwa lugha ya Kiingereza, anashindwa hata kujaribu kuandika na ikiwa atajaribu, basi kichwa huwa miguu na miguu huwa kichwa. Hapo yalipokuwepo masomo ya kweli na walimu wa kweli wenye kufunzwa wakafunzika katika fani ya kusomesha, wanafunzi waliyomaliza chumba cha nane ilikuwa wakiandika Kiingereza, utawavulia kofia. MATIBABU Tukija katika matibabu, ndiko tutakako kukuta kumeporomoka vibaya kabisa. Hospitali hazina madawa, hazina vifaa vya matibabu, hakuna hata vitanda na mabetishiti ya kutosha. Wagonjwa wanatakiwa wakenda kutaka matibabu, wachukue zana zao wenyewe tokea pamba, gauze, vijembe vya kunyolea na 7

hata chupa za "Drips" pia wende nazo. Shuka za kutandika vitandani, mito na foronya zake na nguo za kujifunikia wakati wa kulala vyote hivyo lazima wendenavyo mwenyewe; kama si hivyo basi hatapata matibabu. Ubavuni mwao wakitazama wanaiyona "Mapinduzi Wing" bwana na bibi wanaingia na kutoka! Tokea miaka yalipoanzishwa mahospitali ya serikali Zanzibar, matibabu yalikuwa bure kwa wote. Kwa wananchi, kwa wageni na hata kwa wapita njia. Kuangaliwa na daktari kulikuwa bure, dawa bure, ukilazwa kwa ajili ya matibabu, bure. Na hospitali zilikuwa hospitali kweli kwa kila kitu. Madawa ya kila maradhi yalikuwepo. Madaktari wenye ujuzi wa kazi zao, waliosomeshwa wakakhitimu walikuwepo wa kutosha. Sivyo kama ilivyo hivi sasa, wauguzaji (Staff Nurses) ndio madaktari, tena wa kufika kuuchana na kuupasua mwili wa binadamu! Kwenye nchi yenye sheria, pindi likitokea lolote, basi ushahidi wa watu kama hao, hauwezi kukubalika katika mahakama za sheria, kuwa ni ushahidi wa kidaktari. Lakini ndio kama ule msemo wa Kiswahili, "likikosekana la mama, hata la punda hufaa". Ni kweli kulikuwepo katika hospitali kuu ya serikali sehemu maalumu za kulala wagonjwa wa kulipa. Lakini hayo yalikuwa kwa kupenda kwake mwenyewe huyo mgonjwa. Malipo yenyewe yalikuwa kwa watu wenye kufanyakazi za serikali, walikuwa wakilipa Shs. sita kwa siku, na waliyokuwa hawafanyi kazi za serikali, walikuwa wakilipa Shs.12 kwa siku. Kwa hakika hakukuepo tafauti kubwa baina ya huko kwa malipo na kwa bila ya malipo. Tafauti ziliyokuwepo baina ya sehemu za kulala wagonjwa kwa malipo na sehemu za bure ni za nyongeza tu, sio kwa ya lazima. Kwa mahitajio ya kimatibabu kulikuwa hakuna tafauti hata kidogo. Tafauti zenyewe zilikuwa kama hizi: Katika upande wa malipo, wagonjwa walikuwa wakipewa panjama za kulalia, vyakula vyao wakiletewa katika sinia na sahani zao zilikuwa za kaure na walikuwa wakipewa chai ya kitandani (bedtea) na pia walikuwa wakipewa chai ya alaasiri (afternoon tea). Pia walikuwa wakipewa taula ya kujifutia maji baada ya kukoga. Chakula kikubwa kilikuwa wali na mchuzi wa nyama na kibakuli cha puding. Upande wa wagonjwa wa bure, wao walikuwa wakiletewa vyakula vyao bila ya kutiliwa katika sinia na sahani zao zilikuwa za senti (aluminium), chai walikuwa wakitiliwa katika makopo ya senti. Hapakuwa na tafauti kubwa ya chakula isipokuwa wao badala ya kupewa chai ya kitandani, wakipewa uji. Wagonjwa wote wa kulipa na wa bure walikuwa wakipewa matunda na mboga. Na ikiwa mgonjwa ameandikiwa na daktari chakula maalumu kutokana na maradhi yake, basi alikuwa akipewa chakula hicho (bila ya malipo) sawa sawa na mgonjwa aliyekuwa katika sehemu za malipo ikiwa maradhi yao ni ya namna moja. Madaktari na wauguzaji walikuwa ndio hao hao na matibabu yalikuwa ndio hayo hayo kwa wote, wa kulipa na wa bure. Leo tuambiwayo kuwa matibabu bure, mgonjwa akenda hospitali baada ya kuangaliwa na daktari (pengine na muuguzaji "nurse" tu) na akaandikiwa dawa, akifika kwa watoa dawa jawabu analolipata ni kuwa, "dawa hizi hazipo. Kanunue nje"! Jawabu kama hizo ni za kila siku. Ukenda kuwaangalia wagonjwa waliolazwa, ukianza tu kupanda ngazi, unakaribishwa na harufu za mikojo na za mashonde kutoka vyooni. Hospitali haina maji ya kutosha. Ukiingia katika vyumba vya kulala wagonjwa, unawakuta mapaka wanacheza foliti kwa jinsi ya uchafu uliomo ndani. Makunguru wanaruka huku na huku humo vyumbani, wanapitia dirisha hili na kutokea jengine. Sakafu zinanata kwa uchafu. Sasa watizame hao wagonjwa namna walivyo lala humo vitandani. Vichekesho khasa. Wengine wamejifunika kanga za kisutu, wengine za mkeka, wengine za visima, na za namna mbali mbali. Utadhania watoto wa kizamani walipokuwa wakitiwa kumbini (kutahiriwa) Mabetishiti yaliyotandikwa vitandani kwa ilivyokuwa kila mmoja amekuja na lake, basi, huyu katandika jeupe la mfuto, huyu lililofumwa tausi na huku limeandikwa KARIBU MGENI, na kwa kipembeni ya chumba utaona mengine yameandikwa FURAHA YA BIHARUSI, na jengine limeandikwa kwa maandishi ya nakshi SINA MWENGINEWE, au MAPENZI YETU YA UTOTONI, au MIMI NA WEWE HATULISHANI YAMINI, mradi huwa rangi rangire. Hospital zimepoteza jina na thamani yake kwa kila upande, haziwezi hata kidogo kutowa huduma zitarajiwazo. Hiyo ndio hali ya hayo yanayoambiwa matibabu ya bure! Lakini haya yote yanaowapata ni wananchi wa kawaida tu. Ama wenyewe wakina fulani na fulani pamoja na watoto wao, wao bukheri wa sururu hata hawana khabari nayo wala hawayasikii licha kuyaona. Khalafu kwa kuudanganya umma ati husema, "Tumeondoa serikali ya kisultani na kibwanyenye!". Wakati wa huo Usultan, Mfalme wa nchi hajapata kuwa na hospitali yake peke yake. Yeye pamoja na ukoo wake wakenda katika hospitali hiyo hiyo wanayokwenda watu wa kawaida. Aliyekuwa Mfalme wa nchi, Seyyid Abdulla Bin Khalifa Bin Haroub, 8

alipopata maradhi, alilala katika hospitali hiyo hiyo na alifanyiwa operesheni katika hospitali hiyo hiyo wanayotibiwa watu wa kawaida. Wakoloni wa Kiingereza waliweka sehemu yao ya kutibiwa waliita "European Wing". Kutokana na makelele ya wananchi, khasa kutokana na makala yaliyokuwa yakiandikwa katika gazeti la wananchi la "Mwongozi", sehemu hiyo ilibadilishwa jina na badala ya kuitwa "European Wing", ikaitwa "West Wing". Kutokea wakati huo ilikuwa wazi kwa yoyote mwenye kupenda kwenda katika sehemu hiyo ikiwa yutayari kulipa ada zilizowekwa. Leo baada ya mapinduzi ya kuleta usawa na kuondoa usultani na ubwanyenye, mheshimiwa akiumwa na mdudu upande basi mbio anachukua ndege anakwenda zake Uingereza au Ujarumani kwa matibabu. Ikiwa matibabu yapo nchini bure, mbona wao wanayakimbia na kuyafuatia ya malipo, tena katika nchi za n'gambu na kwa kutumia pesa za wanyonge kwa matibabu yao? Sasa ipi inayostahiki kuitwa serikali ya kibwanyenye? Hii ya waheshimiwa waliyojitenga mbali na umma au ile ya waliyokuwa wakiishi pamoja na umma? Mwenye macho haambiwi tizama! Unaweza kuwadanganya baadhi ya watu baadhi ya siku, lakini huwezi kuwadanganya watu wote siku zote. HALI ZA MAISHA Matunda makubwa waliyopata wananchi wa visiwani wa Unguja na Pemba kutokana na hayo yenyekuitwa, 'mapinduzi', ni shida za kimaisha katika kila upande. Vyakula havinunuliki, nguo hazikamatiki. Mradi wananchi wamo katika kuhiliki kwa maisha yalivyo magumu. Vijana wamekuwa wazee kwa shida. Sokoni kunaitwa, "Uwanja wa Mapambano". Na kweli, ukenda sokoni basi upanie kweli kweli kwani fungu la mihogo sita ikiwa huna Shs.200, hulichukui. Mkungu wa ndizi ya mtwike, Shs.3000, nazi moja Shs.50, pilipili za mchuzi fungu Shs.30 mpaka 50, kicha cha mboga ya mchicha kuanzia Shs.70 mpaka kuteremka Shs.50. Fungu la machungwa sita yaliyotukuka kidogo, Shs.200 na yaliyokuwa madogo, Shs.100. Takriban watu wote wamekuwa Mabaniani, hawali nyama kwani kilo ya nyama ni Shs.1200! Mishahara ya wafanyakazi wa serikali ya kiwango cha chini ambao ndio wengi, ni Shs.7000! Mtu, yeye na mkewe na watoto wawili, inambidi, tena kwa kujibana, atumie Shs.1000 kwa siku kwa chakula cha asubuhi na cha mchana. Kwa hivyo inamlazimu apate Shs.30,000 kwa mwezi. Ikishakuwa mshahara wake ni Shs.7000 kwa mwezi, hizo 23,000, atazipata wapi? Kutokana na hali kama hizo za kimaisha, ndio utaona kuwa toka waongozi wa serikali mpaka wafanyajikazi wa chini wanaishi kwa magendo. "Corruption" (rushwa) katika nchi imefika katika kilele cha juu kabisa. Tunakubali kuwa ulimwengu wote umeingiwa na shida za kimaisha lakini huwepo sababu maalumu ambazo kwa Zanzibar Alhamdulillahi hazijatokea na Inshallah zisitokee. Mara nyingi watu hukutwa na shida za kimaisha katika nchi zao kwa kutokana na hali za mabadiliko kama kutokupata mvua, kutokea mifuriko ya maji, kutokea moto wa misituni, kutokea mitetemeko ya ardhi au vita vya wenyewe kwa wenyewe. Kama nilivyo tangulia kusema shida kama hizo, Alhamdulilah hazikufika katika nchi yetu. Sasa kipi kilicho sababisha taabu na dhiki zote hizi za kimaisha? Hili ni suala ambalo kila mwananchi lazima ajiulize, ikiwa tutajiuliza kwa insafu basi jawabu halitokuwa zito kulipata. Mpaka Januari 11, 1964, pishi moja ya mchele ilikuwa baina ya Shs. nne mpaka tano. (Pishi moja ni sawa na kilo tatu). Ina maana ya kuwa kilo tatu za mchele zilikuwa Shs. nne mpaka tano. Na zilikuwepo kabila mbali mbali za mchele yaani namna kwa namna. Neema zote zilizokuwepo Visiwani Zanzibar, Mwenyezi Mungu ameziondosha kwa kutokana na maovu yaliyoletwa na hayo yenye kuitwa "Mapinduzi". Ni kama wale watu waliyo mchinja bata aliyekuwa akitaga mayai ya dhahabu. Dhulma zilizofanywa za kupoteza roho za viumbe wa Mwenyezi Mungu, bila ya kuwa na kosa lolote la kisheria, mali za watu zimechukuliwa kwa nguvu kutokana na wenye haki nazo. Natija ya hayo imekuwa leo sehemu kubwa sana ya vyakula vinavyouzwa masokoni vinatokana na ardhi zilizoporwa. Kwa hivyo, wananchi wanalishwa vyakula vya haramu. Na wale waliokuwa wamenunua majumba ambayo wanajua ni yenye kutokana na kuibiwa kutoka kwa wenye haki nayo, basi wajue kuwa Sala zao wanazo zisali katika majumba hayo, Mwenyezi Mungu hazikubali. Na ni hivyo hivyo, kwa wale walionunua mashamba yaliyoporwa kutokana na wenye haki nayo, basi na wao wajue kuwa vyakula wanavyo vivuna katika mashamba hayo ni vyakula vya haramu. Kwa hivyo, wao wanakula haramu na wakiviuza, wao, ndio watao chukua dhima ya kuwalisha wenziwao vyakula vya haramu. Kutokana na 9

hali kama hizo zilizokuwa zimefanyika katika nchi, ndio ikawa kila lifanywalo haliwi. Na ikiwa hapatofanywa TOBA ya kweli, basi nawaje wowote wataokuja, ikiwa wataendelea na mwendo wa kurithi mwendo wa kidhalimu waliyoukuta, basi hapana litalo weza kutengenea ila itakuwa kuziba kiraka hapa na kupasuka pengine. Kauli ya Mwenyezi Mungu kattu haiwezi kwenda kombo. Mwenyezi Mungu Anasema kuwa: "Hazidi mwenye kudhulumu illa khasara". NEEMA ZILIKUWEPO Katika huo wakati unaoitwa wa kikoloni, Serikali ya Zanzibar ilikuwa ikiendesha mambo yake yote kama kujenga maskuli, mahospitali, mabarabara, kununua meli za usafiri, pamoja na kuyahudumia na kulipa mishahara ya wafanyakazi tokea wa kigeni mpaka wananchi. Na hao wafanyakazi wa kigeni ambao wengi wao walikuwa Wazungu, basi juu ya mishahara yao walikuwa wakipewa posho maalumu (Inducement Allowances), pia walikuwa wakilipiwa nauli za kuwaleta na kuwarejesha na za wakati wa likizo zao. Yote hayo na mengineyo yakifanywa kutokana na mapato ya ushuru tu wa forodha. Serikali hii yenye kujiita ya "Mapinduzi", ni wao peke yao ndio wenye kununua bidhaa muhimu zote za nchi kama vile, karafuu, mbata na pilipili hoho kutoka kwa wananchi kwa bei wazitakazo wao wenyewe na wakaziuza kwa bei ziliopo katika masoko ya ulimwengu. Isitoshe, serikali hii haina gharama za kuwalipa hao Wazungu kama ilivyokuwa hapo zamani, sasa ilikuwaje hata ifike serikali kuwa haina fedha hata za kuwalipa mishahara wafanyakazi wake wa kienyeji? Hapana shaka sababu kubwa ya hayo ni hii dhulma iendeleayo hadi hii leo, uwendeshaji mpotofu, ukiongozwa na siasa ya husda na uroho wa madaraka na kipato, siasa ya "Chukuwa Chako Mapema"! (CCM). Siasa ambayo immefanya mwananchi kuwa hana uwezo wala itibari yoyote katika nchi yake. Kwa hali za kimaisha nchini mwananchi hawezi kukaa akatua na kufikiri na kupanga juu ya maendeleo ya nchi yake, yeye anafikiri juu ya cha jiyo tu! Siasa mbovu hii iliopangwa makusudi imemzuiliya na kumnyima mwananchi uwezo na njia za kujiendeleza, laa si katika kimaisha, walaa si katika kiutamaduni au kielimu. Inatilia nguvu mizizi ya siasa yake ile ile ilioanziwa, nayo ni "Mwenye Elimu ni Aduwi" KUANZA HARAKATI ZA SIASA Kabla ya Serikali ya Kiingereza kuiingiza Zanzibar chini ya Himaya yake, Zanzibar ilikuwa ni Dola kamili iliyokuwa ina shughuli zake (ikiamiliana) na ulimwengu wote. Mara tu Muingereza alipoitia Zanzibar katika makucha yake mnano mwaka 1890, kila jambo kubwa na dogo lilikuwa lazima liamuliwe kutoka Uingereza. Mfalme wa nchi alifanywa kuwa ni alama tu ya Dola, hakuwa na uwezo katika kukata shauri juu ya uwendeshaji wa nchi. Kama ilivyo kawaida ya wakoloni popote ulimwenguni wanapotawala, lazima watumie mbinu za kuwagawa wananchi (ili waendeleze utawala wao) kutokana na hali za namna fulani ziliopo katika nchi. Ikiwa kwa njia za kidini, ukabila, urangi, utajiri, uwezo wa kimaisha na hata umadhehebu. Katika Zanzibar Muingereza alitumia njia za kuwagawa wananchi kwa kutumia asili za makabila yao. Aliwafanya wenye asili za Kiarabu wajione kuwa wao tu ndio wenye haki za utawala kwa vile ilivyokuwa Mfalme wa nchi anatokana na asili zao. Aliwafanya Washirazi yaani, Wahadimu, Watumbatu na Wapemba wajione kuwa wao tu ndio wenye kila haki za nchi kwa vile ilivyokuwa wao ndio waliyokwenda kuwaita Waarabu (kutoka kwao Oman) kuja kuwasaidia kumuondoa Mreno. Aliwafanya Waafrika (weusi) wajione kuwa wao tu ndio wenye kusitahiki utawala wa Zanzibar kwa vile Zanzibar imo katika Bara la Afrika. Na alichukua uchumi wote wa nchi na kuuweka katika mikono ya wenye asili za Kihindi kuwa wao ndio raia wa Kiingereza sahihi wa tangu asli, kwa uwezo wao wa kimaisha wakajiona kuwa wao ni wabora kuliko wengine katika nchi. Kutokana na hali kama hizo, wananchi walianza kujigawa mafungu kwa mafungu na walianza kufungua Jumuiya zao za Kikabila. Waarabu walifungua yao, Washirazi walifungua yao, Waafrika walifungua yao na Wahindi walifungua yao na Wangazija wakafungua yao. Na ndani ya hizo hizo, zilijitokeza zengine na kila moja ilikuwa ikijitapa kwa upande wake. Kwa muda mkubwa jumuiya hizo zilikuwepo katika nchi na hazikuweza kupata wala kufanya lolote kwa maslahi ya nchi. Kubwa walilokuwa wakilipata ni kualikwa chai ya alaasiri kwenye Bustani ya Jumba la Balozi wa Kiingereza, na kualikwa katika siku ya kuzaliwa Mfalme wa Kiingereza na Mfalme wa nchi na kualikwa kutembelea manuwari za Kiingereza zinapofanya ziara kuitembelea Zanzibar. Katika miaka ya 10

1920 Muingereza katika njama zake za kuzidi kuwafarikisha wananchi ili aendelee kuwatumia katika kuendeleza utawala wake, alianzisha kuwateuwa (appoint) wananchi kwa kuwatia katika Baraza la Kutunga Sheria (Legislative Council) kwa njia za kikabila. Aliwateua hatimaye Waarabu wane, Waafrika wane, Wahindi watatu na Mzungu mmoja. Na upande wa Serikali walikuwemo wakurugenzi wa idara wa Kiingereza kutoka idara mbali mbali za serikali walioteuliwa vile vile, hao walizidi kwa wingi katika baraza hilo kuliko raia. Mwendo huo uliendelezwa kwa muda wa miaka 28 na hapakuweza kupatikana lolote la maslaha ya nchi. Miaka nenda miaka rudi, nchi haikuwa na maendeleo yoyote kukhusu mabadiliko ya Katiba itayo wawezesha wananchi kuendesha wenyewe shughuli za nchi yao bila ya kuingiliwa na yoyote. Katika mwaka 1953 na 1954, Jumuiya ya Waarabu (Arab Association) iliamua kumpelekea Balozi wa Kiingereza madai ya kutaka yaletwe mabadiliko ya Katiba yatayo wawezesha wananchi wa Zanzibar kuchagua wajumbe wao wa kuwapeleka katika Baraza la Kutunga Sheria kwa njia ya uchaguzi wa Kura Moja Kwa Mtu Mmoja (One Man One Vote). Na miongoni mwa madai yao, walidai uondolewe mtindo wa kuwateua wananchi kwa njia za kikabila katika kila jambo la nchi. Pia walitaka baada ya kupatikana kwa matokeo ya uchaguzi huo, paanzishwe mazungumzo ya taratibu za kupatikana kwa Uhuru kamili wa Zanzibar. Balozi wa Serikali ya Kiingereza aliyekuwepo Zanzibar wakati huo akiitwa Mr. Renkin. Balozi huyo alikataa hata kuyatia maanani madai hayo. Jumuiya ya Waarabu walipoona hawakuweza kupata natija yoyote katika madai yao, bali hata hayakuzingatiwa, waliamua kuanzisha mgomo kwa kuwazuia wajumbe wao kushiriki katika vikao vya Baraza la Kutunga Sheria na katika vikao vya Kamati za Mabaraza yote waliyoteuliwa kushiriki. Mgomo huo ulichukua muda wa miezi 18 bara bara. Jambo la kulizingatia katika suala hili ni kuwa, madai hayo kutokana na Jumuiya ya Waarabu hawakuyafanya kwa maslahi yao binafsi zao, bali kwa maslahi ya Zanzibar na Wazanzibari wote bila ya kujali asili za makabila yao. Haya yanajithibisha zaidi kwa vile ukiangaliya idadi ya hao waliyokuwa wakiitwa (au wanaoitwa) Waarabu katika Zanzibar, walikuwa ni kiasi cha 16 katika 100 (16%). Juu ya hivyo waliamua kuziachilia mbali nyadhifa walizopewa, sio hivyo tu, bali kutoa muhanga nafsi zao wakiweka mbele maslahi ya nchi. Bahati mbaya hawakupata kuungwa mkono na wananchi wenziwao wenye asili za makabila mengine juu yakuwa walizungumza nao na waliwataka washirikiane katika madai hayo. Mmoja kati yao (alioteuliwa kushiriki katika Baraza la Kutunga Sheria akiwa ni mwenye asili ya Kiarabu), alipinga uamuzi wa Jumuiya yake na alihudhuria katika kikao cha Baraza la Kutunga Sheria wakati wenzake walipokuwa wamesha amua kugomea. Matokeo yake, alitokea mwananchi mwenye uchungu na nchi yake na kumpiga bwana huyu kwa visu. Kwa bahati mbaya alikufa kutokana na pigo hilo. SHEIKH ALI MUHSIN KWENDA NCHI ZA ULAYA IKIWEMO NA UINGEREZA KUPIGANIA UCHAGUZI WA "COMMON ROLL" (MTU MMOJA KURA MOJA). Wakati Jumuiya ya Waarabu ilipokuwa katika hekaheka za mgomo wao wa kuto kushiriki katika Mabaraza yote ya Serikali kwa madai ya kutaka papatikane mabadiliko ya Katiba yatayo wawezesha wananchi kuchagua wawakilishi wao wa Baraza la Kutunga Sheria kwa njia ya uchaguzi wa "One Man One Vote" na kusita kuteuliwa kutokana na asili ya makabila yao, mwananchi mwenzao mwenye uchungu wa nchi yake alifunga safari (kwa gharama zake mwenyewe) kwenda kupigania maslahi ya nchi yake, akiendeleza madai ya wananchi wenziwe huko nyumbani. Wakati Sheikh Ali Muhsin alipokuwa katika hekaheka hizo huko Uingereza, alikutana na Seyyid AbdulRahman Mohammed (Babu) na waliweza kushirikiana katika juhudi hizo. Katika harakati hizo Sheikh Ali alikutana na waongozi mbali mbali wa kisiasa na wengi wao walimshajiisha juu ya kuendelea na juhudi za ugombozi wa nchi yake na walimpa kila msaada (moral support). Huko Uingereza alipata kuzungumza na wakuu wa Serikali ya Kiingereza, wakuu wa upande wa Upinzani na wakuu wa Vyama vya Wafanyakazi. Pia alikutana na wakuu wa vyama na jumuiya mbali mbali zenye kupigania kuondoka kwa ukoloni katika Afrika na katika sehemu zengine za ulimwengu. KUASISIWA HIZBULWATTAN (ZANZIBAR NATIONALIST PARTY) Wakati Sheikh Ali Muhsin akiwemo katika safari zake huko nchi za Ulaya, huko nyumbani walichomoza wananchi wengine waliokuwa nao na ghera na mapenzi ya nchi yao. (wote, isipokuwa mmoja tu kati 11

yao Sheikh Abdalla Mahmoud walikuwa si Waarabu) Wananchi hao walikutana kuzingatia na kutafakari juu ya kupotea kwa nchi yao kutokana na mbinu za mkoloni za kuwagawa wananchi kwa kutumia asili za makabila yao. Wananchi hao waliibuka na amuo la kuanzisha Umoja wa Wananchi wa Unguja na Pemba. Umoja ambao kila raia wa Zanzibar atastahiki kuwemo bila ya kujali asili ya kabila yake wala Imani ya Dini yake, la umuhimu ni URAIA wake. Hichi kilikuwa ndio chama cha kwanza na pekee katika nchi kuasisiwa kwa kufuatia misingi ya Uwananchi. Wananchi waasisi hao walikuwa ni, Sheikh Vuai Kiteweo, Sheikh Miraj Shaalab, Maalim Zaid Mbarouk, Maalim Maksud Fikirini, Maalim Mwandoa Khamis, Maalim Wazir Ali bin Maalim, Sheikh Haji Hussain Ahmed, Sheikh Othman Soud, Sheikh Abdulla Mahmoud Kombo (wa Makunduchi), Sheikh Ramadhan Tosir (Ramadhan Madafu), Maalim Hija (wa Ndijani), Sheikh Ame, Sheikh Abdulla Mali, Sheikh Haji Kombo (wa Kiboje), Sheikh Abdalla Mahmoud na wenziwe wachache. Kwahivyo wale wenye kusema na kutangaza kuwa Hizbu (ZNP) iliasisiwa na Waarabu au kilikuwa chama cha Waarabu, hapana shaka wanakosea, amma kwa kutokujuwa ukweli ulivyo au wanasema hivyo kwa makusudio ya kutafuta maslaha yao. Ukweli na hakika ilivyo ni kuwa Hizbu haikuasisiwa na Waarabu wala hakijapata kuwa Chama cha Waarabu. Na kama Hizbu kingelikuwa ni Chama cha Waarabu, basi kisingeweza kupata ushindi katika chaguzi zilizofanyika za (One Man One Vote) kwani idadi ya hao wenyekuitwa Waarabu nchini ilikuwa ndogo; kwahivyo idadi yao hiyo haingaliwezesha kukipa (hicho kisemwacho ni chama chao) voti za ushindi. Madai hayo ni miongoni mwa maneno na mbinu za kufitinisha na kuwagawa wananchi kwa kuuwogopa umoja wao. Hapana shaka zimetungwa na wakoloni na kuimbwa na vibaraka vyao, kwa maslahi yao. Mabwana hao tuliowataja hapo juu wakiwa ndio waasisi wa Chama cha HizbulWattan, wao ndio waliyomuendea Sheikh Ali Muhsin nyumbani kwake baada ya kurejea kutoka safarini na kumueleza kukhusu kuasisi kwa chama chao na nini dhamiri zilizo wapelekea kuasisi chama hicho. Baada ya kumueleza, walimtaka na yeye awaunge mkono kwa kujiunga katika chama. Sheikh Ali Muhsin alipoona kuwa hayo wayatakayo wananchi wenzake ndio hayo hayo ayatakayo na kuyapigia mbio daima basi, hapo hapo aliamua kujiunga na kushirikiana nao. Baada yakujiunga, waasisi hao walimtaka Sheikh Ali Muhsin aanze kuzungumza na nduguze wenye asili za Kiarabu bali na kila anaefahamiana nae ili wajiunge na wananchi wenziwao. Sheikh Ali aliupokea na kuanza kuutekeleza ujumbe huo. Miongoni mwa wa mwanzo (kati ya hao wenye kuitwa Waarabu) kujiunga na Umoja huo ni, Sheikh Badr Muhammed Barwani, Sheikh Ahmed Seif Kharusi, Sheikh Amour Zahor Ismaily, Sheikh Ali Ahmed Riyamy Sheikh Nassor bin Isa Ismaily na Sheikh Ahmed Khalfan Naamani haikuchukuwa muda ila nao walijiunga. WAKOLONI DHIDI YA HIZBU, UHURU NA UMOJA WA ZANZIBAR Serikali ya kikoloni ilipoona Umoja wa Hizbu umesimama na kila siku unazidi kuungwa mkono na wananchi wa kila pembe na kila aina, walizidi kuogopea maslahi yao. Kwa kuhifadhi maslahi yao walianza kuuandama Umoja huo HizbulWattan nje ndani, usiku na mchana kwa kuwatumilia baadhi ya wananchi wafanyakazi wa Idara ya Utawala khasa Mamudiri na Masheha. Vitumishi hivyo vilifunga njuga na kuingia mitaani na viamboni katika juhudi za kuuvunja Umoja huo wa HizbulWattan. Kwa kiasi fulani hapo mwanzoni waliweza kufanikiwa, kwani walitumilia mbinu za kuwatisha wananchi; baadhi kwa kuwaambia kuwa, chama hiki azma zake ni kuleta michafuko katika nchi na kwa baadhi ya wananchi wakiwaambia kuwa chama hiki kinataka kumuondoa Mfalme. Kila mmoja wakimpigia mdundo waliofikiria kuwa utaweza kumshitusha na kukiepuka chama hiki. Bali wananchi hawakuchukuwa muda illa waliweza kuzielewa mbinu zao hizo na kuwaepuka na badala yake kuzidi kuungana na wananchi wenziwao. MAKAO MAKUU YA HIZBU Kabla ya uchaguzi wa mwanzo wa "Common Roll Election, yaani, "Mtu Mmoja Kura Moja", katika Zanzibar mnamo mwaka 1957, mwananchi, mzalendo Sheikh Mahmoud wa Mtendeni aliyekuwa mwishoni akijishughulisha na utengezaji wa saa, alijitolea kwa kukipa Chama jumba lake la ghorofa moja lililokuwepo mtaa wa Mwembetanga kuwa ni Makao Makuu ya Chama. Alilitoa jumba hilo bila ya kupokea kodi hata senti moja. Baada ya kumalizika kwa uchaguzi wa mwanzo wa 1957, Hizbu iliyaondoa Makao Makuu yake kutoka Mwembetanga na kuhamia Mkunazini karibu na Msikiti Gofu. Baada ya kuwepo hapo kwa muda, ndio iliweza kununua jumba lake wenyewe katika mtaa wa Darajani 12

na kulifanya ndio Makao Makuu ya Chama. Jumba hilo, baada ya 'Mavamizi' ya Januari 12, 1964, liliporwa na Serikali ya 'Mavamizi' na kufanywa Makao Makuu ya AfroShirazi Youth League. Kama ilivyo hali ya majengo mengi mengineo humo nchini, jumba hilo limetupwa bila ya matengenezo wala matumizi ya faida. Na linaachwa kubomka pole pole. Haya sio ajabu, bali haya yanazidi kuthibitisha jinsi hao viongozi wa Zanzibar walivyokuwa hawana uchungu na Nchi bali na chochote cha nchi. HIZBU KUMLETA ZANZIBAR SEYYID ABDULRAHMAN (BABU) Miezi michache kabla ya uchaguzi wa mwanzo wa 1957, Chama cha HizbulWattan kilimleta Babu Zanzibar ili ashirikiane na wananchi wenziwe katika harakati za kisiasa. Baada ya kufika Zanzibar, Hizbu ilimteuwa kuwa Katibu Mtendaji wa Chama (Excutive Secretary). Kutokana na maarifa aliyokuwa nayo katika mipango ya kuendesha chama cha kisiasa, Babu baada ya muda mdogo alianzisha Umoja wa Vijana (Youth Own Union) (YOU). Kwa msaada na ushirikiano wa waongozi wenziwe na wananchi Babu alifanya kazi kubwa katika kukijenga Chama cha Hizbu ndani na nje ya nchi. Lakini, kwa bahati mbaya, kama alivyokuwa hodari katika kukijenga, ndivyo alivyojaribu kwa uhodari au ilivyo khasa kwa kiujanja kutaka kukibomoa baada ya kushindwa kufikilia maslahi yake binafsi kwa kukitumilia chama. (Baadae tutaeleza aliyoyatenda katika kukibomoa chama na kuifisidi nchi). Alipojiunga Sheikh Ali Muhsin katika chama cha HizbulWattan Zanzibar Nationalist Party (ZNP) aliwapa shauri wakuu wa Chama kumtaka Babu achukue mafunzo katika kuendesha chama na baadae aje asaidie katika uendeshaji wa ZNP. Wakuu wakapendezewa na shauri hiyo, na Babu akawafik. Sheikh Ali hapo tena aliiomba Labour Party ya huko Uingereza kwa kupitia kwa (wasta wa) Mr. John Hatch na Mrs. Eirene White M.P. na Labour Party ikakubali kumpokea Babu kwa mafunzo. Mafunzo hayo yalikuwa ya muda wa miezi sita. ZNP (Hizbu) ililipia gharama zote za kimaisha kwa muda huo na za safari. Katika muda huo pia aliendelea kulipwa mshahara akiwa ni Executive Secretary wa Chama ZNP. Utaona dhahiri kuwa imani ya Hizbu juu ya elimu na maarifa haikufungika sehemu mmoja tu, bali ilikuwa ni kwa kila upande. Hizbu iliamini kuwa uwongozi mwema wa chama na nchi utapatikana kutokana na watu wenye ujuzi na maarifa, kwa hivyo iliona umuhimu wa kumpatia mafunzo na elimu ifaayo Katibu Mtendaji wake khasa, na wengine wafuatie. NATIJA YA SAFARI YA SHEIKH ALI MUHSIN Kama tulivyoeleza hapo mwanzoni kuwa Sheikh Ali Muhsin alizitembelea baadhi ya nchi za Ulaya pamoja na Uingereza kwa ajili ya kugombania kupatikana kwa mabadiliko ya Katiba ya Kuanzishwa kwa uchaguzi wa "Common Roll" yaani "One Man One Vote" katika Zanzibar. Natija ya safari hiyo, Serikali ya Kiingereza, ilimleta Zanzibar Mr. Coutts akiwa ni mchunguzi juu ya maendeleo ya Katiba. Mchunguzi huyo alifika Zanzibar kati ya mwaka wa 1956. Chama cha Hizbu kilifanya maandamano makubwa kwa kumpokea Mr. Coutts hapo kiwanja cha Ndege cha Kiembe Samaki siku aliyofika Zanzibar. Waandamanaji walichukuwa mabango yaliyokuwa yameandikwa: "TUNATAKA UCHAGUZI WA ONE MAN ONE VOTE" "TUNATAKA UHURU WA NCHI YETU" "TUMECHOKA KUTAWALIWA'' ''TUNAPINGA "UBAGUZI WA RANGI NA WA UKABILA" Mjumbe huyo alipokuwa nchini alikutana na wananchi pamoja na wakaazi mbali mbali wa nchini. Alionana hata na watu binafsi. Na alipokea risala (za maandishi na za mdomo) kutoka vyama mbali mbali vya kikabila na vya kidini. Chama cha Hizbu nao walionana na mjumbe huyo na walimkabidhi risala yao yenye kutilia nguvu matakwa yao, matakwa ambayo ndio msingi wa ujumbe wake wa kuja Zanzibar. Inafaa ifahamike kuwa tangu kufika kwa mchunguzi huyo na mpaka kuondoka hapakuwepo chama cha kisiasa nchini isipokuwa kimoja tu HizbulWattan. Vyama vyote vya kisiasa vyengine viliasisiwa baadae. Kwahivyo HizbulWattan ndicho chama cha mwanzo cha kisiasa kuasisiwa Zanzibar. Mr. Coutts alipomaliza shughuli zake alirejea kwao. Baada ya muda alileta mapendekezo ya uchunguzi wake kwa Balozi wa Serikali ya Kiingereza aliyekuwepo Zanzibar. Katika mapendekezo yake hayo, Mr. Coutts alikubali kuwa Zanzibar inafaa kuanzishwa uchaguzi wa "Common Roll" yaani uchaguzi wa kwa pamoja, bila ya kujali khitilafu za kabila. Lakini alipendekeza kuwa uchaguzi uanzie kwa viti sita na vilivyobakia viendelee katika mpango ule ule wa kuteuliwa na Balozi wa Serikali ya Kiingereza kwa kushauriana na Mfalme wa nchi. Pia katika mapendekezo yake, Bwana Coutts alitaka Balozi wa 13

Kiingereza aendelee kuwa Mwenye Kiti wa Baraza la Kutunga Sheria na watumishi wa Serikali ya Kiingereza waendelee kuwa waongozi wa upande wa Serikali. Hizbu haikuridhika hata kidogo na mapendekezo hayo, kwa vile asli ya madaai yao ni kuwa Wawakilishi wote wa Baraza la Kutunga Sheria wawe ni wananchi waliyo chaguliwa na wananchi kwa uchaguzi wa "One Man One Vote". Juu ya hivyo, Hizbu ilikubali kushiriki katika uchaguzi huo kwa kuona kuwa msingi wa matakwa yao ulipatikana; nao ni kuanzishwa kwa uchaguzi wa "Common Roll". Kwa kukubaliwa misingi hii Zanzibar ikawa ndiyo nchi ya mwanzo katika Afrika Mashariki, Afrika ya Kati na ya Kusini kuanzishwa uchguzi kama huo. Baada ya kupatikana haya HizbulWattan ilizidisha juhudi za kuwafahamisha wananchi misingi na faida ya kuchaguwa Wawakilishi wao kwa kupitia uchaguzi huo. WAKOLONI NA NYERERE NDIO WAASISI WA AFROSHIRAZI Wakuu wa Serikali wa Idara ya Utawala, Zanzibar baada ya kuona kuwa mpaka kuondoka kwa mchunguzi Coutts Zanzibar na mpaka kuleta mapendekezo ya uchunguzi wake, hapakuweza kuasisiwa chama chengine cha kisiasa nchni ili kipate kushindana na HizbulWattan (ZNP), waliamua kumtumilia Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Wakoloni walimtumilia Mwalimu kwa kuja Zanzibar kujaribu kuwashawishi waongozi wa vyama viwili vya kikabila waweze kuungana na kuasisi chama kimoja cha kisiasa ili kiweze kushiriki katika uchaguzi na kiweze kuwa pingamizi kwa Chama cha Hizbu. Katika ripoti ya Mr. Penny aliyekuwa Muangalizi wa Uchaguzi aliandika, "Ofisi yangu na Idara ya Utawala zilisaidia kuundwa kwa AfroShirazi na kwahivyo ikaokolewa Zanzibar na kuwa na utawala wa chama kimoja wa namna ya khatari." Mwalimu Nyerere alikuja Zanzibar pamoja na Sheikh Zubeir Mtemvu mnamo mwisho wa mwaka 1956. Mwalimu pamoja na ujumbe wake alikutana na waongozi wa African Association, Sheikh Abeid Amani Karume, Bwana Mtumwa Borafia na Bwana Boniface. Waongozi wa Shirazi Association aliokutana nao Nyerere katika ujumbe wake huo ni, Sheikh Ameir Tajo, Sheikh Thabit Kombo Jecha na Sheikh Othman Shariff Musa. Mkutano huo ulifanyika katika nyumba ya Sheikh Abeid Amani Karume iliyokuwepo mtaa wa Kachorora, Mwembe Kisonge. Nyumba hiyo kwa wakati huo, ilikuwa ikikaliwa na Maalim Haji Ali Mnoga na Bwana Hija Saleh Hija. Njama hizo za wakoloni pamoja na Mwalimu Nyerere zilifanikiwa. Taarikhi 2 Februari 1957, miezi michache tu kabla ya kufikia uchaguzi wa mwanzo wa Juni, 1957 Chama cha AfroShirazi kiliasisiwa rasmi (kikiwa ni muungano wa jumuiya mbili za kikabila yaani "African Association na Shirazi Association"). Karume akawa Rais wa chama, Sheikh Ameir Tajo Makamo wa Rais na Sheikh Thabit Kombo Katibu Mkuu. Uwongozi wa chama haukwenda kwa mzalendo, haukwenda laa kwa Sheikh Ameir Tajo walaa kwa Sheikh Thabit Kombo, walaa kwa Sheikh Othaman Shariff, bali kwa Mzee Karume. Mbinu na njama za kuuwangamiza Uzanzibari zilianzwa zamani. UCHAGUZI WA MWANZO JUNI 1957 Kutokana na mapendekezo ya uchunguzi wa Bwana Coutts kukhusu uchaguzi, uchaguzi wa mwanzo ulifanyika, June, 1957. Na kwa uchaguzi huo ndio wananchi wa Unguja na Pemba kwa mara ya kwanza waliweza kushiriki katika kuwachagua Wawakilishi wao wa Baraza la Kutunga Sheria la nchi yao. Uchaguzi huu ulikuwa wa viti sita. Majimbo mane yalikuwa kwa Unguja na mawili Pemba. Majimbo sita hayo yaligaiwa kama hivi: Unguja: Majumba ya Mawe Unguja: N'gambo Unguja: Kaskazini Unguja: Kusini Pemba: Kaskazini Pemba: Kusini Sheikh Ali Muhsin alisimama katika jimbo la N'gambo akiwa ni Mwakilishi wa HizbulWattan, akishindania na Sheikh Abeid Karume akiwa Mwakilishi wa AfroShirazi, na Sheikh Ibuni Saleh alisimama katika jimbo hilo hilo akiwa ni mgombea huru. (independent candidate). Bwana Rutti Bulsara alisimama katika jimbo la Majumba ya Mawe akiwa Mwakilishi wa Hizbu na washindani wake wakiwa, Bwana Choudhry, Mwakilishi wa Muslim Association, Bwana Anverali Hassan Virji, mgombea huru na Bwana AbdulQadir 14

Mukri, akiwa naye pia ni mgombea huru. Sheikh Amour Zahor alisimama jimbo la Kusini akiwa ni Mwakilishi wa Hizbu na Sheikh Ameir Tajo akiwa ni Mwakilishi wa AfroShirazi katika jimbo hilo. Sheikh Haji Muhammad alisimama katika jimbo la Kaskazini akiwa mgombea huru akiungwa mkono na Hizbu, Sheikh Daud Mahmoud yeye alikuwa Mwakilishi wa AfroShirazi katika jimbo hilo. Hizbu ilimuunga mkono Sheikh Haji Muhammad kwa kuamini kuwa ana fikra za kizalendo, na kutarajia kuwa hayuko mbali bali naye atajiunga na wananchi wenziwe ndani ya HizbulWattan; na hakika ikawa hivyo. Pemba Kusini alisimama Sheikh Rashid bin Ali Khaify akiwa Mwakilishi wa Hizbu na Sheikh Muhammed Shamte Hamad alisimama jimbo hilo akiwa mgombea huru. Pia alisimama katika jimbo hilo Sheikh Abdalla bin Suleiman Busaidy, akiwa naye ni mgombea huru. Pemba Kaskazini, alisimama Sheikh Rashid Hamad Othman akiwa Mwakilishi wa Hizbu, Sheikh Ali Shariff Musa akiwa mgombea huru na Sheikh Shaaban Soud Mponda akiwa Mwakilishi wa AfroShirazi. Matokeo ya uchaguzi huo, Chama cha AfroShirazi kilipata viti vitatu Unguja na hakikuweza kupata hata kiti kimoja Pemba. HizbulWattan ilishindwa kupata hata kiti kimoja laa Unguja wala Pemba. Viti viwili vya Pemba vilichukuliwa na wagombea huru wake, yaani Sheikh Muhammed Shamte na Sheikh Ali Shariff, baadae waliviunga viti vyao kwenye AfroShirazi na kuwa na viti vitano katika Baraza jipya la Kutunga Sheria. Kiti kimoja cha Nyumba za Mawe, kilichukuliwa na Bwana Chodhry Mwakilishi wa Muslim Association. Natija hii ya uchaguzi inathibitisha kuwa Hizbu ni chama kilicho asisiwa bila ya kutokana na asili ya chama au jumuiya ya kikabila iliyokuwepo nchini kwa muda, kama vile ilivyokuwa hali kwa AfroShirazi. Na kwa vile HizbulWattan ilikuwa ndio kwanza chama kichanga haikustaajbu kwa kutopata hata kiti kimoja katika uchaguzi huu, kwani kilikuwa bado hakijawafikilia wananchi kwa wingi. Amma AfroShirazi ambayo ni muungano wa jumuiya mbili za kikabila, jumuiya ambazo kwa muda zilikuwa zishakuwepo nchini hakikupata taabu kupata ushindi wa uchaguzi huu, kwani wanachama wake ndio walewale. Tafauti na HizbulWattan ambayo ilibidi ikuwe kwa kupitia kwa wananchi pole pole. KWANINI SHEIKH ALI MUHSIN ALIAMUA KUSIMAMA N'GAMBO BADALA YA MAJUMBA YA MAWE? Sheikh Ali alikuwa na hakika mia juu ya mia kuwa hatoweza kumshinda mpinzani wake katika sehemu hiyo kama alivyokuwa na hakika kuwa angeweza kupata ushinde ingekuwa amesimama katika Jimbo la Majumba ya Mawe. Lakini alitaka kuthibitisha kuwa kura chache za wananchi wenye asili mbali mbali zilikuwa pia nazo zina umuhimu katika kuendeleza siasa ya chama, si kasoro kuliko kura nyingi ambazo angeweza kuzipata katika Majumba ya Mawe. Lengo lilikuwa ni kuondoa ukabila na urangi. Kura 918 ndizo alizozipata, lakini zilikuwa na umuhimu mkubwa kwa chama na ziliongezea kumpa moyo zaidi katika kuendelea na juhudi za ugombozi wa nchi. Uchaguzi ulifanyika kwa salama na ulimalizika kwa salama ingawa wakoloni walijaribu kutaka zitokee fujo wakati wa uandikishaji wa uchaguzi. Kwani badala ya wao (wakiwa ndio serikali) kuchukua dhamana ya kuchunguwa na kuhakikisha ni nani mwenye kustahiki kuchagua na kuchaguliwa, kazi hiyo waliitupia vyama vya siasa. Kweli sheria waliziweka za kuwa ni raia wa Zanzibar tu ndiye mwenye haki ya uandikishaji na upigaji wa kura, lakini sharia hizo hawakuzilinda na kuhakikisha kuwa zinatekelezwa. Matokeo yake kulitokea kupingana na kuzozana baina ya watu wenyewe kwa wenyewe na hayo ndiyo yaliyozidi kupalilia chuki na ukhasama. Katika uchaguzi huu, wageni wengi khasa kutoka Tanganyika ambao walikuwa wakiishi Zanzibar walipenya katika kujiandikisha na walipiga kura. Hata hivyo, si haba uchaguzi uliweza kufanyika kwa salama bila ya kutokea fujo la namna yoyote. KWENYE SHARI HUZALIWA KHERI Kushindwa HizbulWattan katika uchaguzi wa mwanzo, ndiko kuliko zidi kuwazinduwa wananchi na kujitokeza paruwanja katika kusimama bega kwa bega na wananchi, wazalendo wenziwao katika juhudi za kuigomboa nchi yao kutokana na ukoloni wa Kiingereza. Baada ya kumalizika kwa machofu ya pirika pirika za uchaguzi, Chama cha Hizbu kilitayarisha mkutano maalumu wa hadhara katika Jumba la Seyyid Khalifa Hall (sasa ati linaitwa "Karume House"). Umma wa kike na wa kiume uliomiminika siku hiyo ulikuwa wa aina ya peke yake. Haukupata kutokea tangu kuanza kwa harakati za kisiasa katika Zanzibar. Kwa jinsi mabibi walivyokuja kwa wingi kwenye mkutana huo, ililazimu wanaume wote waliyokuwemo katika ukumbi wa jumba hilo watoke nje kwa kuwapisha mabibi. Wanaume, wao walikaa katika uwanja wa Bustani ya jumba hilo. Siku hiyo ndipo wanawake walipodai wawe na Sehemu yao katika Chama, na wapate kura sawa na wanaume. Waliopiga kifua mbele kati yao ni BiZuhura bt Saleh, 15

BiSharifa Ahmed na BiZamzam Sultan. Kuanzia siku hiyo, kila usiku uchao, wananchi wake kwa waume walikuwa wakijitokeza kwa wingi katika kujiunga na Chama cha Wazalendo wenziwao. Waongozi wa chama kwa kulingana na umma unavyozidi kujiunga na chama kila siku ilibidi watengeneze mipango kukhusu kueneza mafunzo na siasa ya chama kila upande. KUKUWA KWA HARAKATI ZA SIASA Baada ya kumalizika kwa uchaguzi wa Juni 1957, Hizbu ilianza kutayarisha mipango ya kueneza fikra na siasa ya chama kwa Unguja na Pemba kwa mjini na mashamba. Natija ya juhudi hizo haikuchukuwa muda illa zilidhihiri. Matawi ya Hizbu yalikuwa yakifunguliwa kila siku Unguja na Pemba, mjini na mashamba. Kila Tawi lilikuwa na skuli ya kusomeshea vijana na watu wazima (wa kike na wa kiume) waliokuwa hawakuwahi kuingia skuli wakati wa udogo wao. Vilevile kila Tawi lilikuwa ni kituo cha kutoa "Huduma ya Kwanza" (First Aid) kwa wenye kufikwa na maradhi madogo madogo. Vijana wa Youth Own Union ndio waliyokuwa walimu wa kusomesha na ndio waliyokuwa waganga wa kutibu maradhi madogo madogo. Sheikh Juma Aley, aliyekuwa Waziri wa Fedha katika Serikali ya ZNP/ZPPP, yeye ndiye aliyekuwa akiwapa vijana hao mafunzo ya haraka juu ya namna ya kusomesha. Dr. Said Aboud Bin Tahir, yeye alikuwa akiwapa mafunzo juu ya matibabu madogo madogo. Sheikh Ali Makka na Sheikh Juma Ali (dogo dogo), wao wakijitolea kwa kuwapa wogonjwa matibabu katika kituo cha matibabu cha Hizbu kilichokuwepo katika jumba la Makao Makuu ya Chama, hapo Darajani. Katika kituo hicho vilikuwepo kila vifao vyenye kuhitajika kwa matibabu. Wagonjwa walikuwa wakiangaliwa na wakitibiwa bila ya malipo yoyote na bila ya kutizamwa msimamo wao wa kisiasa. MuHizbu na MuAfro wote walikuwa wakipata matibabu sawa sawa. Pia katika Makao Makuu hayo ya chama kulikuwepo na sehemu ya "Welfare" ambayo ilikuwa ikijishughulisha na mambo ya kutoa misaada ya dharura kwa mwananchi yoyote (si kwa wananchama wa Hizbu tu). Sehemu hiyo ya "Welfare" ilikuwa na gari mbili za kuchukulia wagonjwa (ambulance) kutoka majumbani mwao kwa wale waliokuwa hawawezi kwenda kwa miguu yao au wanaishi katika sehemu zilizo mbali na hospitali, kama mashamba na sehemu zengine. Pia sehemu hiyo ya "Welfare" ilikuwa ikishughulikia kuweka majina ya wananchi wanaojitolea kutoa damu kwa kuwasaidia wagonjwa. Ilifika hadi hospitali kuu ya serikali wakihitajia damu kwa sababu ya wagonjwa, wakenda katika sehemu hiyo ya "Welfare" ya Hizbu kuomba watu wa kutoa damu. Vilevile ilifika wakati mmoja hospitali ya serikali kuazima dawa fulani kutoka katika kituo cha Hizbu cha matibabu. Sehemu hiyo ya "Welfare" ilikuwa chini ya uangalizi wa Seyyid Hashim Bin Abubakar Bin Salim, Bibi Aisha Salim (maarufu Bibi Aisha wa YOU au Aisha Mtumbatu) na Bibi Azza Mohammed Seif (mamewatoto wa Sheikh Ali Muhsin). Miongoni mwa harakati za Hizbu katika kuwahudumia wananchi, wazee na vijana wa kiume na wa kike walijitolea bila ya malipo kwa ujenzi wa njia ya Nungwi. Mwishowe Serikali ikaingia kusaidia katika ujenzi huo kwa kuleta mipango ya siku moja kuwalipa na siku moja ya kujitolea. Yaani katika siku 30, wakilipwa siku 15. Mpango huo ukiitwa "Jisaidie Nikusaidie". Vilevile Mahizbu kwa kuendeleza huduma kwa wananchi wenziwao walijitolea kuijenga njia ya Uzi toka mwanzo mpaka mwisho, kwa kuunganisha kisiwa cha Uzi na kisiwa kikubwa cha Unguja hapo Unguja Ukuu. Pia walijitolea kuwapelekea maji ndugu zao wa Tumbatu. Wakati wananchi wa Tumbatu walipokuwa na shida kubwa ya maji Chama kilikodi matishali na kupakia mapipa ya maji kutoka mjini mpaka Tumbatu. Ikiwa nitaendelea kutaja ya kheri yaliokuwa yakifanywa na Chama cha Hizbu katika kuwahudumia wananchi, basi itanifanya nisiendelee na hayo niliyo yakusudia khasa kuzungumza na wananchi wenzangu. Kwahivyo, haya machache yanatosha kukupeni sura na fikra namna gani Chama cha Hizbu kilivyokuwa kikiendeshwa. Na kutokana na maendesho kama hayo, ndipo kila uchao wananchi walikuwa wakijiunga na Wazalendo wenziwao. ATI HUSEMWA KUWA HIZBU IMEFELI! Ikiwa Hizbu imefeli, iliyofuzu ni ipi!? Yaliyofanywa na Hizbu kikiwa ni chama tu cha siasa, basi serikali ya Zanzibar hii iliyokuwepo ya "Mavamizi" kwa muda wa miaka 30 (1964 - 1994) haijaweza kuyafanya. Hospitali za serikali kuwa hazina hata vidonge vya Panadol licha ya Penicillin, ndio kufuzu huko? Skuli za serikali kuwa hazina hata madeski ya kukalia, licha walimu wajuzi wa kusomesha, ndio kufuzu huko? 16

Wanafunzi wa Chuo cha Kujifunza Uwalimu hawana hata matandiko wala mashuka katika vitanda vyao. Chakula ni cha mipango mipango na wakati mwingi wanafunzi wanalala na njaa kwa ukosefu wa chakula cha kutosha. Huko, ndiko kuffuzu! Barabara hazipitiki kwa uchafu wa maji ya makaro. Katika kila taa 10 za njiani, taa mbili tu ndizo zinazowaka na muwako wenyewe utadhani globu ya kurunzi (tochi) uchwara. Huko ndio kufuzu? Baada ya miaka 30 ya utawala wa Serikali yenye kujiita ya 'mapinduzi', kiwanja cha ndege cha Zanzibar hakina hata kiti kimoja cha kukalia wajao kuwashindikiza wasafiri wao. Ikiwa huko ndio kufuzu, basi hatujui kufeli kutakuwa na sura gani! Inaweza kuwa huko ndio kufuzu, yategemea nia na azma za waongozi wa hizo serikali. Bali kwa nchi na wananchi huko hata kwa lugha gani hakuitwi kufuzu, bali ni kudamirika. Kudamirika ambako ni sawa na kuteremkiwa na balaa, kwani iteremkapo balaa ya Mwenye Enzi Mungu (kwa maasi ya binaadamu) humfika mwema na mbaya. Maafa ya Zanzibar yamemteremkia kila mwananchi, mwema na mbaya, (Inshallah wako hao wema). Sababu kubwa ya hivyo ni kuwa juu ya maovu yaliofanywa na yaendeleayo kufanywa hakuna tena kukatazana maovu na kufahamishana kutenda mema, na hapo ndipo Mwenye Enzi Mungu azidishapo nakama Zake. Mwenye Enzi Mungu tunakuomba utunusuru. KUGAWANYIKA KWA AFROSHIRAZI Mwanzoni mwa 1959 kulitokea mgawanyiko wa waongozi wa Chama cha AfroShirazi. Sheikh Mohammed Shamte na Sheikh Ali Shariff waliamua kujitoa katika chama na kwa kutoka kwao, kulifuatiwa na wanachama wengi nyuma yao khasa Pemba. Katika wakati huo huo, Chama cha AfroShirazi kilimfukuza katika chama Sheikh Ameir Tajo kwa singizio la kuwa alikwenda kuwaombea msaada wa fedha vijana wa YASU (Young African Social Union) kwa Sir Tayabali Karemjee kwa ajili ya ujenzi wa klabu (club) yao iliyokuwepo Miembeni, bila ya kuiarifu kamati kuu ya AfroShirazi. Sababu kubwa zilizompelekea Sheikh Mohammed Shamte na wenziwe kujitoa katika Chama cha AfroShirazi ni zenye kutokana na hisia za uwananchi khalisi kwa nchi yake. Hisia zake za kisiasa na nyendo zake pamoja na matarajio yake juu ya nchi yake yalikuwa ya kutaka kutumikia upatikane uhuru wa Zanzibar. Uhuru utaongozwa na Wazanzibari wenyewe bila ya kuchukua amri au shauri kutoka pahala pengine popote. Sheikh Karume yeye alikuwa hawezi kufanya lolote bila ya kuzungumza na Mwalimu Nyerere na kama itavyoamuliwa na Mwalimu, ndivyo hivyo hivyo atavyofuata hata ikiwa si maslahi kwa Zanzibar (na mara nyingi hivyo ndivyo ilivyokuwa). Sheikh Mohammed Shamte, hayo yeye alikuwa hayakubali; kwahivyo daima walikuwa wakibuburushana mpaka mambo yalipofika hadi ya kufanywa mikutano ya Kamati Kuu ya Chama bila ya kuarifiwa Sheikh Mohammed kwa kukhofiwa kuwa akiwepo ataleta upingaji juu ya baadhi ya mambo. Ilipofika kiwango hichi, maji kuzidi unga, Sheikh Mohammed na Sheikh Ali Shariff walijitoa katika AfroShirazi. KUASISIWA KWA ZANZIBAR AND PEMBA PEOPLES' PARTY (ZPPP) Chama cha Z.P.P.P. kiliasisiwa Novemba, 1959. Raisi wa Chama alikuwa Sheikh Mohammed Shamte Hamad na Naibu Raisi alikuwa Sheikh Ameir Tajo. Makao Makuu ya Chama yalikuwa Malindi Zanzibar. Z.P.P.P. kilikuwa Chama cha wananchi wa Unguja na Pemba. Kwa Unguja hakikuweza kupata wanachama wengi kwa wakati huo lakini kwa Pemba kiliweza kupata wananchi wengi kujiunga katika chama. Misingi na dhamiri ya Z.P.P.P. ikilingana na ya HizbulWattan. Nayo ni kufanyakazi kwa pamoja Wazanzibari wote, bila ya kubali rangi, kabila au imani zao za kidini katika kugombania kupatikana Uhuru wa Zanzibar kwa ajili ya mslahi ya wananchi wote. Waongozi wa HizbulWattan hawakuwa na shaka yoyote juu ya uzalendo wa Sheikh Muhammed Shamte na wenziwe, kwahivyo walikuwa wakiamini kuwa iko siku wataweza kufanyakazi pamoja. TUME YA SIR HILLARY BLOOD Katika Mei, 1960 Serikali ya Kiingereza baada ya juhudi kubwa zilizokuwa zikifanywa na Chama cha Hizbu juu ya kutaka yapatikane maendeleo zaidi juu ya mabadiliko ya Katiba katika nchi, walimleta Sir Hillary Blood kutoka Uingereza akiwa ni mchunguzi wa mabadiliko ya Katiba. (Huyu ni wa pili, wa kwanza alikuwa Mr. Coutts). Hizbu kama kawaida yao waliandaa maandamano makubwa kutoka kiwanja cha ndege cha Kiembe Samaki mpaka mbele ya nyumba ya Balozi wa Kiingereza. Waandamanaji wote wa kike na wa kiume, walichukuwa mabango yaliyoandikwa neno moja tu, "UHURU 1960".

17

Sir Hillary Blood alipofika Zanzibar alivikuta vyama vitatu vya siasa, Zanzibar Nationalist Party (ZNP) yaani HizbulWattan, AfroShirazi Party yaani A.S.P. na Zanzibar and Pemba Peoples' Party yaani Z.P.P.P. Vyama vyote vitatu vilimpelekea Sir Hillary Blood risala za matakwa yao na vilevile Sir Hillary alipokea risala kutoka katika vyama vya wafanyakazi na kutoka kwa watu binafsi. Pia alizungumza na kuchukua fikra na nasaha kutoka kwa watu mbali mbali. Risala ya Hizbu na risala ya Z.P.P.P. zililingana sana katika matakwa yao. Zote mbili zilitaka Wawakilishi wote wa Baraza la Kutunga Sheria wawe wananchi waliyochaguliwa katika uchaguzi wa "One Man One Vote". Na baada ya matokeo ya uchaguzi huo yafuatiye mazungumzo ya Uhuru kamili wa Zanzibar. Ama risala ya AfroShirazi Party, ilitaka Wawakilishi wote wa Baraza la Kutunga Sheria wawe 25 na katika hao 22 wawe ndio wa kuchaguliwa kwa njia ya uchaguzi na watatu waliyobakia wawe miongoni mwa wafanyakazi wa Serikali ya Kiingereza waliopo nchini, hawa wateuliwe na Balozi wa Kiingereza. Kwa faida ya wasomaji, nitazinukulu sehemu muhimu za risala zote tatu, yaani ya Hizbu, ya AfroShirazi na ya ZPPP. Kwa kufanya hivyo hapana shaka itakuwa faida zaidi kwa wananchi na khasa kwa vichipukizi vyetu, na wao wapate kujionea kwa macho yao, chama gani kilichokuwa kikiwakumbatia na kuwataka wakoloni waendelee katika uwongozi wa Serikali ya Zanzibar. Pia wapate vilevile kujionea wenyewe vyama gani vilivyokuwa vikitaka upatikane Uhuru kamili wa nchi. Risala ya Hizbu ilikuwa kama hivi: "......It is unnecessary now to argue whether or not it is our right to rule ourselves compeletely and whether or not we have the capacity to do so. Those days are over. There are now no two sides to the question. ".......In framing the recomendations regard should be paid to Her Majesty's Government's view that the legislature should become predominantly elective in character and that the executive should be reorganized to permit the establishment of a ministerial system. "......Under any circumstances you will be failing in your duty and mocking the people of Zanzibar if you recommand anything less than full independence for the country". Risala ya Z.P.P.P. ilikuwa kama hivi: ".....That the Zanzibar and Pemba Peoples' Party feels that this Sultanate should be given full independence within the British Commonwealth soon after the next election. "....That the Legislative Council should be of 30 members and that all 30 seats should be contested on Common Roll Election as stipulated in your terms of reference". Risala ya AfroShirazi Party ilikuwa kama hivi: ".......the AfroShirazi Party believes and recommends that the Legislative Assembly should consist of no more than 25 seats of which three seats should be reserved for exofficio members. The rest should all be open seats to be fought in Common Roll Election. "......The exOfficio members should be the Minister for Justice, Minister of Finance and Minister of Defence and External Affairs. "......It will indeed be fitting, and we entreat Her Majesty's Government, that 30th October, 1960, should mark the granting of selfgovernment to the people of these islands". Mimi sitoongeza langu ila ninawaachia wasomaji baada ya kuzisoma risala zote tatu waamuwe wenyewe, ni wepi hao waliyokuwa bado wakitaka kurambatia urojo wa wakoloni. Ikiwa Wizara ya Uadilifu, Wizara ya Fedha na Wizara ya Ulinzi na Mambo ya Nje, ziwe katika mikono ya wakoloni, sasa wananchi watakuwa wamejitawala kitu gani? Ndio wenye kuitambua siasa ya AfroShirazi, na kwa kujidhihirisha zaidi kwa kimaandishi kama hivi, hawakustaajabu walipomuona Karume ameyatia mambo yote muhimu kwa nchi, chini ya amri ya Serikali ya Muungano ambayo kwa ukweli ni Serikali ya Tanganyika, chini ya amri ya kidikteta ya Bwana Nyerere. Umoja wa Vijana wa Youth Own Union walikasirishwa sana na mapendekezo ya Sir Hillary Blood. Kwa kuthibitisha uchukivu wao, waliandaa mkutano maalumu wa hadhara katika mtaa wa Mwembe Sanda, Miembeni, mkutano huo ulihudhuriwa na mamia ya wananchi. Baada ya kusomwa mapendekezo ya 18

Mchunguzi huyo mbele ya wananchi, ilikubaliwa kuilani na kuichoma moto ripoti hiyo, kwa vile ilivyo kwenda sana katika kudharau matakwa ya wananchi. Pia ilikubaliwa katika mkutano huo kumpelekea Sir Hillary risala maalumu kutoka kwa Umoja wa Vijana wa Youth Own Union ya kupinga mapendekezo yake aliyoyatoa kukhusu maendeleo ya Katiba katika Zanzibar. Mapendekezo aliyoyatoa Sir Hillary Blood katika uchunguzi wake ni kuwa viti 22 tu viwe vya kuchaguliwa katika uchaguzi wa "Common Roll Election" na viti vinane viendelee kuwa vya kuteuliwa na Balozi wa Kiingereza kwa kushauriana na Mfalme wa nchi, yaani vyote viwe 30. Mapendekezo yake haya hayakuwa mbali na yale ya Chama cha AfroShirazi. Kama tulivyoona hapo juu katika risala yao, AfroShirazi wao walipendekeza kuwa viti vyote visizidi 25, kati ya hivyo vitatu viwe vya wajumbe wa kuteuliwa na kuchukuwa nafasi muhimu katika serikali. UCHAGUZI WA PILI, JANUARI 1961 Baada ya miaka mitatu unusu tokea kufanyika kwa uchaguzi wa mara ya mwanzo, Juni 1957, ulifanywa uchaguzi mwengine, katika Januari, 1961. Safari hii, mabibi nao walipata fursa ya kushiriki katika uchaguzi. Uchaguzi huu ulikuwa wa viti 22. Vyama vyote vitatu vilishiriki kwa ukamilifu. Matokeo ya uchaguzi huo yalikuwa, AfroShirazi walipata viti 10, Hizbu viti tisa na ZPPP viti vitatu. Kwa natija hii, hapakuwa na chama kilichoweza kuunda Serikali ila kwa kushirikiana na chama chengine. Balozi wa Kiingereza Sir George Mooring aliwaalika waongozi wa vyama viwili vikubwa, yaani Hizbu na AfroShirazi kwa kuzungumzia tatizo liliokuwepo juu ya utaratibu wa kuweza kuunda serikali. Baada ya mazungumzo marefu ya hivi na hivi mwongozi wa Chama cha Hizbu, Sheikh Ali Muhsin alitoa shauri la kutaka ifanywe serikali ya pamoja ya vyama vyote vitatu. Mwongozi wa Chama cha AfroShirazi, Sheikh Abeid Amani Karume, yeye aliipinga shauri hiyo na badala yake alitaka matokeo ya uchaguzi huo yafutwe na pafanywe uchaguzi mwengine. Baada ya kuzozana zozana na pasipatikane natija yoyote ya kurahisisha tatizo hilo, Balozi wa Kiingereza, Sir George Mooring alimpa kila kiongozi katika hao wawili muda wa wiki moja ajaribu kupata waakilishi waliyochaguliwa kuchanganya viti vyao pamoja naye ili aweze kupata wingi wa viti vya kumuwezesha kuunda serikali. Fursa hiyo kwanza alipewa Sheikh Abeid Amani Karume kwa kuwa Chama chake kilipata kiti kimoja zaidi kuliko Chama cha Hizbu. Wakati Karume alipokuwa katika juhudi za kuzungumza na Chama cha ZPPP, kwa kuwataka waviunge viti vyao vitatu upande wa Chama cha AfroShirazi, baadhi ya watumishi wa Serikali wa kikoloni na khasa wa Idara ya Utawala, nao waliingia kazini kwa kufunga njuga kwa njia za siri siri. Miongoni mwa utumishi wao ilikuwa ni kukisaidia Chama cha Afro waweze kupata viti vya kutosha waunde serikali. Kwa kutaka kutekeleza utumishi wao huo walizungumza na Sheikh Othman Shariff na walimtaka afanye kila njia na kila jitihada mpaka ampate Sheikh Mohammed Shamte akubali kuvipeleka viti vyao (vya ZPPP) vitatu upande wa AfroShirazi. Kwa ilivyokuwa Sheikh Othman aliahidiwa malipo fulani fulani kama vile kulipiwa deni la nyumba yake ya "Kijipu House" iliyokuwepo Gongoni, Zanzibar, na mengineyo yaliyokhusika na mambo ya kisiasa, aliukubali utumwa huo. Na kwa kuwepo makhusiano ya kuowana baina yake na Sheikh Mohammed Shamte, yaani Sheikh Mohammed Shamte alimuowa binti wa Sheikh Issa Shariff (mtoto wa kaka yake Sheikh Othman Shariff), na vilevile mmoja katika hao washindi watatu wa ZPPP, alikuwa ni kaka yake yeye Othman, yaani, Sheikh Ali Shariff, basi Sheikh Othaman aliona itamuwiya rakhisi kufuzu utumwa huo. Othman aliingia mbioni kwa "Full speed". Baada ya kuona jitihada zake zote alizozifanya za kumtaka Sheikh Mohammed Shamte ayakubali matakwa yake zimefeli, alianza kumtishia kaka yake Sheikh Ali Shariff kwa kumwambia kuwa, "Ikiwa na wewe hukubali kufuata shauri yangu, basi hutoniona tena baada ya leo. Afadhali nijiuwe kuliko kuona umeungana na Hizbu". Kwa kutaka kutimiza tishio lake hilo kwa kaka yake, Sheikh Othman alitoka kwake na asijulikane aliko kwenda, kwa muda mkubwa sana. Alijificha! Zogo la kutafutwa Sheikh Othman lilianza mjini, vijana wa YASU upande wao na Polisi upande wake. Kaka yake, Sheikh Ali Shariff aliingiwa na khofu na kihoro kwa mapenzi ya ndugu yake. Aliwambia vijana wa YASU wamtafute Sheikh Othman na watapomwona wamwambie kuwa yeye (Ali Shariff) ameikubali shauri yake ya kukiunga kiti chake katika upande wa 19

AfroShirazi. Haukupita muda mkubwa baada ya hapo, ila Sheikh Othman alirejea kwake kutoka huko alikojificha, kwani baadhi ya hao vijana wa YASU walikuwa wakijuwa mpango huo alioufanya Sheikh Othman na wakijua wapi alipojificha. Kwa hivyo, walipopata uhakika kwa Sheikh Ali Shariff wa kukubali kujiunga na AfroShirazi, mara tu walizifikisha salamu hizo kwa Sheikh Othman. Muda wa wiki aliopewa Karume ulimalizika kwa kupata kiti kimoja tu zaidi, yaani kiti cha Sheikh Ali Shariff. Kwa kutowezakana kuunda Serikali kwa viti walivyokuwa navyo AfroShirazi hadi wakati huo, basi Balozi wa Kiingereza alimpa Sheikh Ali Muhsin naye muda wa wiki ajaribu kupata waakilishi wa kujiunga naye ili aweze kupata wingi wa kutosha wa kuwezesha kuunda serikali. Sheikh Ali pamoja na wenziwe hawakuchukua muda mrefu ila waliweza kukubaliana na Sheikh Mohammed Shamte na Sheikh Bakari Mohammed wote wawili hao wakiwa ni washindi wa ZPPP kuviunga viti vyao upande wa Hizbu. Muda wa wiki mbili ulimalizika na ikawa kila upande wanavyo viti kumi na moja. Ilivyokuwa hali ndio hivyo, Balozi wa Kiingereza alitoa uamuzi wake kuwa pafanywe Serikali ya Mshikizo ya muda wa miezi sita na baada ya hapo pafanywe uchaguzi mwengine. Mwongozi wa Hizbu, Sheikh Ali Muhsin, ilipokuwa hali imefika hadi hii alizidi kumnasihi mwongozi mwenziwe Sheikh Karume kwa kumtaka atizame na kuyapa umuhimu maslahi ya nchi kuliko ya vyama. Alimnasihi waondoe mzozo na wakubaliane kuunda Serikali ya pamoja. Alizidi kwa kumfahamisha Sheikh Karume kuwa kufanya hivyo kutainusuru nchi na kuingia katika uchaguzi mwengine, ambao ni gharama na pia kukhatarisha usalama. Pia alimueleza kuwa kuunda Serikali ya pamoja itawezesha nchi bila ya kuchelewa zaidi kufikilia Uhuru. Sheikh Karume akiwa keshakuwa na mipango na matakwa yake, mbali na maslahi ya nchi, yote haya aliyakataa katakata na alishikilia fikra iliyotolewa na Balozi wa Kiingereza ya kufanywa Serikali ya Mshikizo na kufanywa uchaguzi baada ya miezi sita. Baada ya kuwa hakuna jengine isipokuwa kutekelezeka shauri hiyo iliyotolewa na Balozi, lilizuka tatizo jengine nalo ni, nani ataye kuwa Waziri Kiongozi wa Serikali hiyo ya Mshikizo? Sheikh Ali Muhsin alipendelea nafasi hiyo apewe raia aliyekuwa na uzowevu juu ya mambo au uwendeshaji wa serikali. Kwahivyo, alipendelea nafasi hiyo ya Waziri Kiongozi wa Serikali ya Mshikizo apewe Sheikh Ahmed Lakha, ambaye ni Mzanzibari, mwenye ujuzi, maarifa, itibari na hakuwa mwenye kujiambatisha na chama chochote. Mwongozi wa AfroShirazi Sheikh Abeid Amani Karume alikataa katakata kukhusu nafasi hiyo kupewa Sheikh Ahmed Lakha. Yeye alitaka nafasi hiyo apewe Bwana Roberts, mfanyakazi wa Serikali ya Kiingereza ambaye wakati huo alikuwa ni "Chief Secretary" wa Serikali ya Zanzibar na pia ndiye aliyekuwa akikamata nafasi ya Ubalozi wa Kiingereza wakati Balozi akiwa katika likizo. Shauri ya mzee Karume ndiyo iliyokubaliwa na Balozi, Sir George Mooring na Bwana Roberts akawa Waziri Kiongozi wa mwanzo wa Serikali ya Mshikizo ya Zanzibar. Ukifuatia na kuzingatia utatambua kuwa katika harakati za kisiasa hizi zilizopita muda wote huu, fikra za ASP daima zilikuwa zikilingana na kukubaliana na fikra na matakwa ya kikoloni. UCHAGUZI WA TATU JUNI 1961 Kwa kuchelea natija ya uchaguzi huu kutokea kama ile ya uchaguzi uliopita (wa Januari, 1961) hata kutokumkinika chama kimoja pekee kuunda Serikali kwa idadi ya viti walivyokuwa navyo, katika uchaguzi huu liliongezwa jimbo moja na kufanya idadi ya viti vyote 23 badala ya 22. Ushirikiano Wa ZNP/ZPPP Katika uchaguzi huu, Hizbu na ZPPP walikubaliana na walitangaza rasmi kuwa watashirikiana katika kusimamisha wagombea wao kwa pamoja. Yaani, jimbo litalo simamiwa na mgombea wa Hizbu, ZPPP haitoweka mgombea wake bali wanachama wote wa Hizbu na wa ZPPP watampigia kura mjumbe huyo na hivyo hivyo kwa mgombea wa ZPPP. Fikra hii ilifanyika kwa kuzidi kutilia nguvu umoja na vile kila siku idhihirivyo kuwa misingi na matakwa ya ZNP/ZPPP juu ya maslahi ya nchi yakilingana. Ndugu zetu ASP wao daima muelekeo wao (kama tulivyoona na tutavyozidi kuoona) ulikuwa kinyume na hivyo, maslahi yao binafsi ndio yaliokuwa mbele.

20

AfroShirazi Iliandaa Machafuko Siku ya Uchaguzi Waongozi wa Chama cha AfroShirazi walipoona ushirikiano wa Hizbu na ZPPP katika uchaguzi, walijua kuwa hawatoweza kushinda, kwa hivyo waliandaa kufanya machafuko katika vituo vya uchaguzi. Walianza kwa kuwasukuma sukuma wanachama wa Hizbu na wa ZPPP khasa mabibi na vizee. Waliendelea katika mipango yao hiyo ya fujo kwa kuwatowa wanachama wa ZPPP/ZNP katika mistari waliyokuwa wamejipanga kwendea kwenye masanduku ya kutilia kura. Ilipokuwa wanachama wa Hizbu na ZPPP hawakukubali kutolewa katika mistari, hapo tena wanachama wa AfroShirazi walianza kuwapiga wanachama wa ZNP/ZPPP kwa magumi, mateke na mwisho walianza kutumia silaha kama visu, mapanga na mawe. Michafuko hiyo ilianza katika vituo vya uchaguzi na baadae iliendelea majumbani, mitaani na viamboni. Waongozi wa Hizbu na ZPPP, walipoona wenziwao wao wanauliwa na kujeruhiwa, waliwatangazia wao wote waondoke katika vituo vya upigaji kura na waliwazuia waliyokuwa bado hawajafika katika vituo vya upigaji kura, wasende mpaka watapoambiwa na chama chao ZNP/ZPPP kuwa wende ndio wende. Michafuko hiyo ilimalizikia kwa kuuawa MaHizbu na MaZPPP 68 na mamia kujeruhiwa vibaya vibaya. Wengi wao walibakia na vilema vya muda na wengine vya milele. Michafuko hiyo ilianza tokea saa 12 za asubuhi kabla hata kufunguliwa hivyo vituo. Na tokea wakati huo, askari wa polisi walikuwa wamesha kuwepo katika vituo vyote vya mjini na mashamba lakini walijifanya kama hawayaoni yenye kutokea. Serikali ya kikoloni walipoona mambo yamezidi watu wanauliwa na kujeruhiwa kwa wingi, ndipo walipoagizia kikosi cha askari wa kuzuwia fujo (GSU) kutoka Kenya. Askari hao walifika Zanzibar kiasi cha saa saba za mchana. Baada ya kuingia mitaani waliweza kutuliza michafuko na kurejesha hali ya kawaida. Lakini wakati huo waliyokuwa wameuliwa, wamesha uliwa na waliyokuwa wamejeruhiwa, wameshajeruhiwa. Juu ya fujo hilo lililoandaliwa na AfroShirazi katika uchaguzi huo kwa kufikiria kuwa kwa kufanya hivyo watapata ushindi, wanachama wa ZPPP na Hizbu walisema, Mungu Mmoja kheri tufe lakini hatutowacha kwenda kuzitia kura zetu. Baada ya kuhisabiwa kura, AfroShirazi walijikuta na viti vyao vilevile 10 walivyovipata katika uchaguzi wa Januari 1961. ZNP/ZPPP walijipatia viti 13. Katika sehemu ya Zanzibar kulikofanywa ukatili mkubwa sana siku hiyo ya uchaguzi wa taarikh moja Juni 1961, hapakutokea kuliko Bambi. Huko Mwalimu mmoja wa skuli, anayeitwa Bwana Ali Muhsin Mshirazi (bwana huyu pia alishiriki katika mauwaji ya Januari 12, 1964) alishirikiana na makatili wenzake kwa kuwachukua vijana wadogo, ambao wengi wao walikuwa ni miongoni mwa wanafuzi wake na kuwatia ndani ya tanuri la kuchomea mbata kwa kuwadanganya ati kuwa "anawahifadhi na ghasia ziliopo katika mji". Baada ya kuwatia humo, waliiondoa ngazi waliyo wateremshia kisha waliwamiminia geloni kwa mageloni ya petroli kisha wakawawasha moto. Vijana hao waliachwa wakiteketea mpaka kuwa majivu. Tanuri hilo ndilo lililokuwa kaburi lao. Jee nini kosa la vijana hao? Na wawe wana makosa ya aina yoyote, jee ulimwenguni huu tuishio iko kanuni ya adhabu ya aina hiyo? Kwa Kiislamu haifai kuadhibu kwa moto hata kwa mnyama mwenye kudhuru. Seuze binaadamu, tena watoto wadogo! Malipo ya Mwenyezi yanaanza tangu hapa duniani, natunayaona, kesho ndio hesabu na malipo ya milele. Kwa bahati, mmoja kati ya vijana hao ambaye siku yake ilikuwa bado Mwenye Enzi Mungu hajamuandikia, aliweza kupenya wakati walipokuwa wenzake wana teremshwa ndani ya tanuri mmoja mmoja. Kijana huyo, ndiye baadae aliyeweza kuzifikisha khabari hizo katika mikono ya polisi na kuweza kukamatwa mikatili hiyo. Jambo la kustaajabisha na kusikitisha ni kuwa mahakama iliyokuwa ikiendeshwa na Naibu Jaji Mkuu mkoloni, Muingereza haikuweza kupata hata mshitakiwa mmoja kati ya wote waliyopelekwa mbele yake kwa mashitaka ya kuuwa, kuwa ni mukhalifu. Hakutokea hata muuwaji mmoja aliyepewa adabu ya kuuliwa au hata ya kufungwa gerezani kifungo kikubwa. Wote waliachiliwa huru. Katika kesi ya mwalimu (Ali Muhsin Mshirazi) na mikatili wenzake, ushahidi aliyoutoa kijana yule mdogo mbele ya mahakama, kila aliyekuwepo na kumsikia kijana huyo jinsi alivyotoa ushahidi wake dhidi ya mikatili hiyo, aliona mikatili hiyo itapewa adabu inayo wasitahikia. Hakimu wa kesi hiyo alipokuwa anatoa hukumu yake alisema kuwa, "Ushahidi nilioupata kutokana na kijana huyu ni ushahidi mzuri, na 21

nampa sifa kwa kutokana na umri wake na alivyoweza kutoa ushahidi wake na alivyoweza kuikabili mahakama kwa ushujaa. Lakini, nasikitika ushahidi wake haukuweza kupata kusaidiwa na mtu mwengine ambaye mwenye umri mkubwa. Kwa kuwa huyu ni kijana mdogo, nashindwa kuamini ushahidi wake peke yake. Kwa hivyo basi, sina budi na kuwaachilia huru washitakiwa hawa"!! Yote haya tuliokuwa tukitendewa na wakoloni, bado utamsikia Mwalimu Nyerere akidanganya na akikejeli kwa kusema kuwa Chama cha HizbulWattan kikipendelewa na wakoloni! Nyimbo hii ya kijanja na ya kejeli pia ikiimbwa na waongozi wa hii serikali inayojiita ya 'mapinduzi'. Haikuimbwa na hao tu, bali hata wale ndugu zetu tuliyokuwa pamoja kwa muda hapo mwanzoni walikuwa shangweni kwa kujitafutia maslahi ya nafsi zao. Maneno haya ni istihzai ya dhahiri, kwani ingelikuwa wakoloni wameipendelea Hizbu bali sio kuipendelea, lakini lau wangelifanya insafu na uaminifu tu basi hata hayo yenye kuitwa 'mapinduzi' yasingeweza kutokea. MUUNGANO WA ZNP/ZPPP, WAUNDA SERIKALI Waswahili wanasema, "Wanja wa Manga, si Dawa ya Chongo". Fujo lote walilolifanya AfroShirazi kwa kutarajia kupata ushindi, hawakupata ushindi. ZNP/ZPPP, waliunda Serikali kwa kupata viti 13 kwa viti 10 vya AfroShirazi. Serikali hii ikiitwa, "Responsible Government" yaani "Serikali ya Madaraka" kufikilia Uhuru. Sheikh Mohammed Shamte Hamad ndiye aliyekuwa Waziri Kiongozi (Chief Minister) wa Serikali hiyo. KUTOKUFAULU MAZUNGUMZO YA MWANZO YA KATIBA YA UHURU Baada ya miezi 10 mpaka 11 tokea Serikali ya Muungano wa ZPPP/ZNP "Serikali Ya Madaraka" kuwa katika madaraka, Serikali ya Kiingereza ilikubali baada ya kushikiliwa na serikali hiyo ya madaraka kufanya mkutano wa mazungumzo ya uhuru. Mkutano huo wa Katiba ya Uhuru ulifanywa katika miezi ya Machi na April 1962 huko Lancaster House, London. Pande zote mbili yaani upande wa Serikali na upande wa Upinzani walihudhuria kwenye mkutano huo. Kwa bakhti mbaya mkutano huo haukuendelea kwa siku nyingi illa ulivunjika bila ya kukubaliana kwa kuwekwa kwa taarikh ya Uhuru. Waongozi wa AfroShirazi walikataa kuzungumzwa chochote kilicho khusika na kutolewa taarikh ya Uhuru mpaka kwanza pafanywe uchaguzi mwengine. Baada ya matokeo ya uchaguzi huo, ndio yafuatie mazungumzo ya kutolewa kwa taarikh ya Uhuru. Waongozi wa upande wa Serikali waliwanasihi mwisho wa uwezo wao waongozi wa upande wa Upinzani yaani AfroShirazi waache kuleta vizingiti vitavyo sababisha kuchelewa kwa Uhuru wa Zanzibar. Bali waongozi wa AfroShirazi walin'gan'gania uzi wao huo huo wa kupinga kuzungumzwa chochote kitachofikilia kutolewa kwa taarikh ya Serikali ya Ndani kabla ya kufanywa uchaguzi mwengine. Waongozi wa upande wa Serikali, walipoona waongozi wa upande wa Upinzani hawataki kubadili msimamo wao, walijaribu kuzungumza nao nje ya mkutano. Katika mazungumzo hayo, upande wa Serikali waliutaka upande wa Upinzani wakubali kufanyika serikali ya pamoja, yaani "Government of National Unity" (hii ni mara ya pili ASP kupewa shauri na wenzao ZNP/ZPPP kufanya serikali ya pamoja.) Katika serikali hiyo ya pamoja, upande wa Serikali watawapa ASP wizara tatu kati ya wizara nane na pia watawapa uwezo wa kutumia "veto" kwa jambo lolote litalotokea nao wakaliona si maslahi kwa upande wao. Yaani ASP watakuwa na madaraka sawa sawa na ZNP/ZPPP katika uendeshaji wa hiyo serikali ya pamoja. Waongozi wa AfroShirazi baada ya kuyasikia hayo, walitaka muda wa kuyazungumza na kuyazingatiya wakiwa peke yao, na waliahidi kutoa uamuzi wao siku ya pili kabla ya kuhudhuria kwenye kikao cha mkutano wa Katiba. Kwa dalili zote, walionesha kuwa wamevutika na mashauri hayo, na ilikuwa kuna tamaa kuwa watawafik. Upande wa Serikali walingojea kwa hamu na matumainio (pia na wasi wasi) kuwa shauri waliyoitoa itakubaliwa au sana watataka wazidishiwe wizara moja badala ya tatu ziwe nne, yaani wawe wao ASP na wizara nne na ZNP/ZPPP wizara nne. Wakati ulipofika siku ya pili, waongozi wa ASP wakiongozwa na Sheikh Karume walifika kwa Mawaziri. Walikataa hata kukaa kitako, Karume alisema, "Tumeyazingatia mashauri yenu. Mazuri! Lakini sisi hatutaki kushirikiana na nyinyi!" Wakazunguka wakatoka. Kutokana na msimamo huo wa ukorofi uliopangwa, waliyokuwa wakiutumia AfroShirazi, Mwenyekiti wa mkutano huo, Waziri wa Makoloni, aliufunga mkutano bila ya kuzungumzwa lolote kukhusu maendeleo ya Katiba. Aliwashukuru wajumbe wote kwa kuhudhuria na aliwataka warejee nyumbani mpaka 22

watapoweza kuwafikiana baina yao, wakati huo Serikali ya Kiingereza itakuwa tayari kufungua tena mazungumzo ya maendeleo ya Katiba. Wajumbe wote wa upande wa Serikali (isipokuwa Sheikh Ali Muhsin) na wa upande wa Upizani, walirejea Zanzibar bila ya kuwaletea wananchi Uhuru wa nchi yao waliwokuwa wakiungojea kwa hamu kubwa. Wananchi wa Zanzibar kwa jumla walivunjika moyo na matokeo haya. Baada ya kufuzu hayo yenye kuitwa 'mapinduzi' ya Januari 12, 1964, Katibu Mkuu wa AfroShirazi, Sheikh Thabit Kombo alisema wakati akikhutubia mkutano wa hadhara mbele ya Makao Makuu ya AfroShirazi, hapo Mapipa ya Ngozi, Kisiwandui: "Tunamshukuru Mwalimu Nyerere kwa kutuvua mtego waliyotaka kutunasa Mahizbu wakati wa mkutano wa mwanzo wa Katiba, huko Uingereza. Mahizbu walitaka kutufanyia ujanja wa kutaka tuungane pamoja katika kuendesha serikali na kwa kutaka kutimiza ujanja wao, walikiri kutupa wizara tatu katika serikali yao. Lakini mzee Karume kabla ya kusema lolote, alizungumza na Mwalimu kwa simu kumtaka shauri yake juu ya jambo hilo. Mwalimu alimwambia mzee Karume asikubali kufuata shauri hiyo ya Hizbu kwani huo ni ujanja tu wakutaka kusiwepo na upinzani. Mkitaka shauri yangu kataeni. Ndipo mzee alipokataa", alisema Thabit Kombo. Mara nyingi utamsikia Mwalimu akisema kuwa yeye hakukhusika na lolote katika mizozo ya kisiasa ya Zanzibar. Hatujui Mwalimu anataka akhusike namna gani zaidi ya hivyo alivyokhusika (alivyo jikhusisha). Yeye Mwalimu ndiye aliyekiasisi Chama cha AfroShirazi na ni yeye aliyekuwa, "master mind" katika kuyaandaa hayo yenye kuitwa 'mapinduzi'. Wavamizi wal