Upload
cathbert-angelo
View
1.706
Download
14
Embed Size (px)
DESCRIPTION
SERIKALI MALIZA TATIZO LA UKOSEFU WA DAMU SALAMA NCHINI
Citation preview
Taarifa kwa Vyombo vya Habari, 22 Machi 2015
SERIKALI INAPASWA KUMALIZA TATIZO SUGU LA
UKOSEFU WA DAMU SALAMA NCHINI
Sikika inasikitishwa na taarifa za kukosekana kwa damu salama katika vituo
vya kutolea huduma za afya nchini. Damu salama ni moja kati ya dawa
muhimu kwa kuwa inakidhi vipaumbele vya afya katika jamii kama
ilivyobainishwa na Shirika la Afya Duniani (WHO). Ni dawa muhimu na ya
kipekee kwa kuwa pindi inapohitajika kutumika hakuna mbadala wala haiwezi
kutengenezwa kiwandani. Hivyo, uwepo wa damu salama katika hospitali zetu
ni jambo la lazima.
Nchini Tanzania, Mpango wa Taifa wa Damu Salama (NBTS) uliopo chini ya
Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, una wajibu wa kuhamasisha watu ili
kujitolea damu. Vile vile, mpango huu una wajibu wa kuhakikisha kuwa damu
salama pamoja na bidhaa zitokanazo na damu zinapatikana katika vituo
vyenye dhamana ya kutoa huduma za damu.
Ijapokuwa NBTS imeweza kuongeza upatikanaji wa damu salama kutoka
chupa 12,500 (2005) hadi chupa 160,000 (2013) kwa mwaka, hata hivyo,
ukusanyaji wa damu bado upo chini ya mahitaji halisi ya nchi ambayo ni kati
ya chupa 400,000 hadi 450,000 kwa mwaka kwa mujibu wa Shirika la Afya
duniani. NBTS imekuwa ikikusanya takribani asilimia 38 tu ya mahitaji ya
damu salama nchini kwa mwaka, hivyo kusababisha upungufu wa kudumu wa
damu salama katika vituo vyenye dhamana ya kutoa huduma za damu nchini.
1
Kumekuwepo na taarifa katika vyombo mbalimbali vya habari kwa majuma
kadhaa sasa, kuhusu upungufu mkubwa wa damu katika vituo vyenye
dhamana ya kutoa huduma za damu nchini. Uhitaji wa damu salama nchini ni
mkubwa kutokana na kuongezeka kwa tatizo la upungufu wa damu mwilini
unaosababishwa na malaria na matatizo ya uzazi hasa wakati wa ujauzito na
kujifungua. Tanzania ni moja kati ya nchi zilizo kusini mwa jangwa la Sahara
zenye idadi kubwa ya vifo vya watoto na wanawake. Inakadiriwa kuwa karibu
asilimia 28-30 ya vifo vya kina mama vinatokana na upungufu wa damu
mwilini. Hii inaweza kuonekana katika matumizi ya damu salama nchini
ambayo karibu asilimia 80 ya damu inayokusanywa inatumika kwa wanawake
na watoto, wakati asilimia 20 inatumika kwa matumizi mengine kama
upasuaji, ugonjwa wa selimundu (sickle cell anaemia) na tiba ya saratani. Kwa
hiyo upatikanaji wa damu salama kwa wakati unazuia kuongezeka kwa
ugonjwa na hata vifo na hivyo kuboresha afya za wananchi.
Ni kutokana na umuhimu huu wa damu salama, Sikika iliamua kuangalia kwa
undani ukubwa wa tatizo hili, sababu na namna linavyoweza kutatuliwa ili
kuboresha upatikanaji wa damu salama nchini.
Katika utafiti wetu tulibaini kuwa, kuna upungufu mkubwa wa damu salama
katika vituo vingi vya kutolea huduma hiyo. Kwa mfano katika wilaya ya
Simanjiro, mahitaji ya damu salama kwa mwaka ni chupa 145 hata hivyo
wamekuwa wakipokea chini ya nusu ya mahitaji yao. Mwaka 2013 walipokea
chupa 74 tu, na kati ya mwezi Februari na Machi mwaka huu hawakuwa na
akiba kabisa kwani mara ya mwisho kupokea damu ilikuwa mwezi Septemba
mwaka 2014.
2
Hali hiyo pia ilionekana katika wilaya ya Mpwapwa, ambapo kati ya mwezi
Februari na Machi 2015 hawakuwa na akiba ya damu salama. Mahitaji yao
kwa mwaka ni chupa 1,400, hata hivyo wamekuwa wakipokea wastani wa
chupa 20 kwa mwezi ambazo ni sawa na chupa 240 tu kwa mwaka ikiwa ni
mara 6 pungufu ya mahitaji yao.
Kwa mkoa wa Dar es salaam, hali ni kama ilivyo katika mikoa mingine
ambapo, vituo vyote vilivyotembelewa vilikutwa na upungufu mkubwa wa
damu salama kutokana na kupatiwa damu pungufu na NBTS. Kwa mfano,
hospitali ya Wilaya ya Temeke imekuwa ikipokea damu salama inayokidhi
mahitaji ya hospitali kwa asilimia 20% tu kwa mwaka, huku hospitali ya
Amana ikiwa inapatiwa asilimia 40% tu ya mahitaji yake. Hospitali ya Taifa
Muhimbili, ambayo imekuwa ikishugulikia mgonjwa makubwa na sugu, nayo
imekuwa ikipatiwa damu salama kwa takribani asilimia 50 - 60 ya mahitaji
yake. Uhaba wa damu salama umekuwa sugu nchini kote kutokana na kuwa
vituo vyote vinategemea NBTS katika kupatiwa bidhaa hiyo.
Sikika inatambua na inaamini Serikali inatambua kuwa, chanzo kikubwa cha
uhaba sugu wa damu salama nchini ni upungufu wa fedha unaoikabili NBTS.
Hii inasababisha NBTS kushindwa kutekeleza majukumu yake muhimu kama
vile kufanya kampeni za kuhamasisha wananchi kuchangia damu kwa hiari
pamoja na kununua vitendanishi vya kutosha kwa ajili ya kupima, kuhifadhi
na kutengeneza bidhaa zingine zitokanazo na damu salama. Kwa takribani
miaka 10, bajeti ya NBTS kwa zaidi ya asilimia 80% imekuwa ikitoka kwa
wafadhili, hususani Serikali ya Marekani, kupitia Mpango wa dharura wa
UKIMWI (PEPFAR) ambao wamekuwa wakipunguza ufadhili wao unaofikia
kikomo mwaka huu 2015. Serikali imekuwa ikichangia asilimia 20 tu ya bajeti
3
ya NBTS huku ikishindwa kuziba pengo lililokuwa linaachwa na wafadhili,
jambo ambalo ndio chanzo kikubwa cha NBTS kushindwa kukusanya damu
salama ya kutosha nchini. Kwa mfano, Mahitaji ya damu salama nchini ni
chupa 100,000 hadi 112,000 kwa muhula kiasi ambacho NBTS imeshindwa
kukusanya hata nusu ya kiasi hicho. Mathalani, katika kipindi cha mihula
miwili iliyopita (Oktoba – Disemba 2014 na Januari – Machi 2015), NBTS
imeweza kukusanya kiasi cha chupa 34,000 tu ambacho ni sawa na asilimia 17
ya mahitaji ya damu salama kwa kipindi hicho.
Kushindwa kwa NBTS kukusanya damu salama ya kutosha, kumepelekea
baadhi ya vituo vya huduma kutumia damu wanayoikusanya kutoka kwa
familia, ndugu na jamaa za wagonjwa badala ya kuipeleka katika vituo vya
kanda au taifa kwa ajili ya kupima, kuhifadhi na kutengeneza bidhaa zingine
zitokanazo na damu salama. Hii ni hatari kiafya, kwani huweza kusababisha
maambukizi ya magonjwa na pia kuchangia matumizi mabaya ya damu kwa
kuwa vituo vya huduma havina mashine na utaalamu wa kutosha hususani
katika kutengeneza bidhaa zingine zitokanazo na damu.
Kama ilivyo kwa bidhaa zingine, uhaba wa damu salama kwa kiasi kikubwa
umekuwa ukisababisha baadhi ya watoa huduma za afya kujihusisha na
vitendo vya rushwa - ‘’kuuza damu kwa wagonjwa’’ kutokana na ongezeko la
mahitaji ya damu huku upatikanaji wake ukiwa ni mdogo.
Sikika, tumefurahishwa na tunapongeza jitihada za wadau mbalimbali kama
taasisi za kidini na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya kwa kuandaa kampeni
za kukusanya damu. Jitihada hizi ni nzuri katika kutatua tatizo kwa muda
4
mfupi lakini kunahitajika mpango endelevu ambao utaiwezesha NBTS
kutimiza wajibu wake ipasavyo.
Tunaitaka Serikali kuwajibika katika kutatua tatizo la damu salama nchini. Ni
jukumu la Serikali kuiwezesha NBTS kifedha badala ya kutegemea wafadhili
na watu binafsi. Serikali ipange bajeti inayotosha pamoja na kutoa fedha kwa
wakati kwa Mpango huu ili kuuwezesha kukusanya na kusambaza damu
salama inayokidhi mahitaji ya nchi. Tunaamini kuwa, iwapo Mpango wa
Taifa wa Damu Salama utakuwa na fedha za kutosha na zinazotolewa kwa
wakati hakutakuwa na Upungufu wa damu salama nchini.
Mr. Irenei Kiria, Mkurugenzi wa Sikika, S.L.P 12183 Dar es Salaam,Simu: +255 222 666355/57, Nukushi: 2668015, Barua pepe: [email protected],
Twitter: @sikika1, Facebook: Sikika Tanzania, Tovuti: www.sikika.or.tz
5