30
TAASISI YA ELIMU YA WATU WAZIMA DAR-ES- SALAAM KOZI: SHAHADA YA ELIMU YA WATU WAZIMA NA MAFUNZO ENDELEVU. MSIMBO: KUCHAMBUA NADHARIA ZA UHAKIKI MSIMBO KODI: KIU 07431 MWAKA WA MAFUNZO: 2013/2014. MUHULA : II MKUFUNZI : MADAM KILEO AINA YA KAZI: KAZI YA KIKUNDI MAJINA YA WASHIRIKI 1. ISSA TWAHA 336/BACE/2012 2. KIWANGO IRENE 360/BACE/2012 3. TUZIHIRWE NIKUNDIWE 471/BACE/2012 4. MAEMBE PATRICIA 373/BACE/2012

MAUDHUI ALMASI ZA BANDIA2

Embed Size (px)

Citation preview

TAASISI YA ELIMU YA WATU WAZIMADAR-ES- SALAAM

KOZI: SHAHADA YA ELIMU YA WATUWAZIMA NA

MAFUNZO ENDELEVU.

MSIMBO: KUCHAMBUA NADHARIA ZA UHAKIKI

MSIMBO KODI: KIU 07431

MWAKA WA MAFUNZO: 2013/2014.

MUHULA : II

MKUFUNZI : MADAM KILEO

AINA YA KAZI: KAZI YA KIKUNDIMAJINA YA WASHIRIKI

1. ISSA TWAHA 336/BACE/2012

2. KIWANGO IRENE 360/BACE/2012

3. TUZIHIRWE NIKUNDIWE 471/BACE/2012

4. MAEMBE PATRICIA 373/BACE/2012

5. NGUNGULU NEEMA 434/BACE/2012

6. PALANGYO DEBORA 445/BACE/2012

7. HAMISI RABIA 334/BACE/2012

8. LWEYEMAMU ALFRED 368/BACE/2012

9. SOWOKI DEOGRATIAS.J 462/BACE/2012

10. BARTHOLOMEW MARY 310/BACE/2012

SWALI:

Uhakiki wa maudhui katika Riwaya ya Almasi za Bandia.

MPANGO WA KAZI

A: UTANGULIZI

(i) Historia Ya Mwandishi

(ii) Muhtasari Wa Kitabu

B: KIINI CHA SWALI

(i) Nadharia Iliyotumika Katika Uchambuzi

(ii) Uchambuzi wa Maudhui na vipengele vyake mbalimbali

vikiwemo:

Dhamira

Migogoro

Msimamo wa Mwandishi

Falsafa

Ujumbe

C: HITIMISHO

(Maoni ya jumla kuhusu mchango wa kitabu mchango)

Kufanikiwa kwa mwandishi

Mapungufu ya Mwandishi

UTANGULIZI

Historia ya Mwandishi

Mwandishi wa Riwaya ya Almasi za Bandia, Marehemu Chachage C.S.L

alikuwa Mhadhiri katika idara ya Elimu ya Chuo Kikuu cha Dar-es-

salaam baada ya kutunukiwa shahada ya P.H.D ya chuo kikuu cha

Glasgrow, Uingereza. Katika uhai wake amaeweza kuandika riwaya

nne zikiwemo Almasi za Bandia, Sudi ya Yohana , Kivuli na Makuadi wa Soko

Huria. Kwa ujumla riwaya zake hizi zimejikita katika masuala ya

historia ya nchi katika vipindi mbalimbali ikiwemo historia mara

tu baada ya Uhuru na wakati wa utandawazi na tahri zake katika

nchi ya Tanzania.

Muhtasari wa Riwaya

Riwaya ya Almasi za Bandia inazungumzia matatizo mbalimbali

yanayoikumba jamii yetu ya Afrika kwa sasa katika Nyanja za

uongozi, kisiasa, kiuchumi na katika nchi za Ulaya jinsi watu

weusi wanavyobaguliwa kutokana na rangi zao.

Mwandishi Chachage amesawiri mawazo ya kimapinduzi kwa kuichambua

jamii ya Tanzania na hali nzima ya mfumo wa uongozi katika nyanja

za serikali, uchumi na kuonyesha uozo uliomo katika jamii ambayo

viongozi kwa kutumia madaraka yao hufanya biashara za magendo

kama vile; Gordoni ambaye ni Inspekta wa polisi alivyomtumia

ndugu yake Mertoni Mpwito kumuuzia mzungu ambaye anaitwa John

Gregory na mhindi Kanjir Almasi za Bandia uk 112.

Vilevile bado ubaguzi wa rangi upo katika bara la Ulaya

umeoneshwa kwa kuonyesha jinsi Waafrika wanavyobaguliwa na

kunyanyaswa, mfano huko Ulaya waafrika walikuwa hawaruhusiwi

kuchanganyika na wazungu katika makazi na hoteli.

Katika riwaya ya Almasi za Bandia iliyoandikwa na C.S.L Chachage,

mwandishi amesawiri matukio mbalimbali ambayo yapo na yanaendelea

kujitokeza katika jamii mbalimbali hapa nchini na hata nje ya

nchi. Katika riwaya hii msanii ameonyesha/amechora mambo

mbalimbali yanayojitokeza katika jamii mfano, matumizi mabaya ya

madaraka, ubaguzi wa rangi, umaskini, rushwa, matabaka ya

walionacho na wasiokuwanacho, biashara haramu, mapenzi na ndoa,

ubakaji, migomo, ulevi, matumizi ya madawa ya kulevya, elimu,

ujasiri pamoja na nafasi ya mwanamke katika jamii. Dhamira hizi

zimechorwa na msanii kupitia wahusika mbalimbali kama Merton

Mpwito kada wa chama na kiongozi serikalini, Yakini ambaye

alikuwa ni mfanyakazi wa shirika la Umma, Faraji ambaye alikuwa

ni Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Kilimo na Gordon ambaye ni

askari mpelelezi.

Nadharia Zilizotumiwa katika Uchambuzi

Katika uchambuzi wa riwaya ya Almasi za Bandia nadharia tatu

zimetumika zikiwemo nadharia ya U-Marx, Ufeministi na Semiotiki.

Nadharia ya U-marx ambayo misingi yake inaonyesha uyakinifu wa

hali ya juu katika kutumia wahusika kama vipaza sauti. Tumeona

alivyowatumia akina Yakini, Zambe, Tereza na Mzee Majikondo ambao

walikuwa wanakataa mfumo kandamizi katika jamii hususani katika

nyanja za uongozi. Mwandishi amemchora Merton Mpwito na mwenzake

Gordon ambao ni viongozi katika chama na serikali na ambao

hutumia nyadhifa zao kwa kukandamiza tabaka la chini ndani ya

serikali.Wahusika wamechorwa kusawiri mabadiliko ya kimapinduzi

ya kimaendeleo. Tereza anaonekana akihamasisha wenzake katika

kufanya maandamano ya kupinga vikali suala la viongozi

kujiongezea marupurupu wakati hali ya jamii ilikuwa ni mbaya.

Nadharia ya Ufeministi, vilevile imetumika katika kusawiri yale

yanayotokea katika jamii hususani mfumo wa ugandamizaji wa

wanawake katika ya ndoa na mila, na jinsi wanawake wanavyojaribu

kujikomboa ili kuleta haki na nafasi sawa kati ya mwanamke na

mwanaume.

Nadharia ya Kisemiotiki, pia imetumika ambayo inahusu msimbo wa

kiishara na jinsi watazamaji au wasomaji wa kazi ya fasihi

wanavyogundua maana ya ishara katika kazi hiyo. Mfano, Yakini

alimgeukia Tereza na kusema huku akimbonyezea jicho kwa utani wa

mazoea (uk 62).

Vilevile Merton Mpwito alivyotumbua macho yaliyoashiria mshangao

mkuu akiwa ametabasamu kwa dharau ya wazi kabisa (uk 77). Pia

tunamwona Yakini akichorwa na mwandishi katika (uk 75) kuwa

“Yakini aliduwaa. Hakuamini kabisa kile kilichotaka kutokea

dakika moja iliyopita”.

Dhamira Kuu

Dhamira kuu katika riwaya hii ni unafiki wa viongozi wa Kiafrika

na taswira hasi aliyovishwa Mwafrika kutokana na mtazamo wa

Wazungu huko Ulaya. Katika riwaya hii ya Almasi za Bandia, Mwafrika

anavishwa taswira hasi kama kujihusisha na uuzaji wa madawa ya

kulevya, wanawake weusi kujihusisha na ukahaba, Waafrika kupenda

starehe na mapenzi kuliko kufanaya kazi, Waafrika kuwa tabia za

ubakaji Hii inaonesha unafiki ambao unawagusa Wazungu kuhusu

mtazamo wao juu ya Waafrika waishio huko Ulaya pamoja na viongozi

wa Kiafrika wanaofuata nyayo za Wazungu badala ya kusaidia

Waafrika wenzao. Kwa ufupi mtazamo wa Wazungu kuhusu Waafrika ni

mtazamo hasi kwani Waafrika waliojaliwa kufika Ulaya wamekuwa

wakidharauliwa na kuvishwa sifa mbaya kama watu wanaojali sana

mapenzi kuliko kazi na watu wasiokuwa na maendeleo. Pia Mwafrika

mwenyewe amejivika sura ya bandia (Almasi za Bandia) kwa kufanya

mambo ambayo yanamwaibisha Mwafirika na kuwafanya Wazungu kuwa na

mtazamo hasi kuhusu Mwafrika. Kwa mfano ubakaji na uuzaji wa

madawa ya kulevya, ukahaba na kupenda starehe ni sifa walizovikwa

Waafrika kuwa ndiyo wanaofanya mambo hayo na siyo Wazungu. Kwa

mfano, tunaona Wazungu wakiamini kwamba Waafrika ndio wanaofanya

biashara ya madawa ya kulevya na ndio sababu iliyopelekea Yakini

na Chaupele wakamatwe na askari polisi pale uwanja wa ndege wa

Amsterdam. “Basi wote waliochukuliwa hapa ni Waafrika watupu. Kisa? Kwa kawaida

wanawashuku watu weusi kuwa ndio wauza bangi na madawa ya kulevya. Hakuna

hata mzungu mmoja aliyechukuliwa…” (uk.48).

Waafrika pia wanachukuliwa kuwa ni watu ambao hawajasoma, kwa

mfano pale Muhindi anaposema Fanya kaji mingi African hapana soma na iko

vivu. Hapana kuwa kama European.” (uk 19). Hapa alikuwa akiongea kwa

lafudhi ya Kihindi akimaanisha kuwa Waafrika wanastahili kulipwa

ujira mdogo na sio sawa na Wazungu kwa sababu hawajasoma. Bara la

Afrika pia linachukuliwa kuwa ni sehemu yenye shida nyingi,

umasikini, magonjwa njaa kwa mf…………………. .

Suala la Uongozi Mbaya

Kwa upande wa viongozi wa Kiafrika ni kuwa, Almasi za Bandia

zinawakilisha viongozi ambao si wakweli yaani walaghai na

matapeli ambao huyatafuta madaraka kwa udi na uvumba kwa

kuwaahidi wananchi mambo ya uongo ambayo hawayatekelezi. Hali

hii huonesha uongozi mbaya na matumizi mabaya ya madaraka kwani

viongozi hawa hutumia madaraka waliyopewa kinyume cha sheria kwa

kukandamiza, kunyonya, kuonea na hata kudharau walioko chini

yako. Msanii amewachora viongozi wa chama na serikali wakitumia

ovyo madaraka yao kwa kufanya mambo ambayo ni kinyume cha miiko

ya kazi zao. Viongozi hawa wa Kiafrika wanaonekana hata

wakiwatishia Waafrika wenzao kama inavyojidhihirisha katika nukuu

ifuatayo. Merton Mpwito, msanii amesawiriwa akitumia wadhifa wake

na kuwatishia wenzake kwa kujivunia madaraka yake.

Tunathibitishiwa na mwandishi anaposema “…………Mwache atakuja

tambua madaraka yangu siku moja” (uk 58), “……………… basi

tutakaporudi nyumbani ninyi wote hapa mtanikoma! Nimemaliza! Na

sina mchezo!”................ (uk 76)

Msanii amemchora Merton Mpwito ambaye alikuwa ni kiongozi katika

chama na serikali akiwatishia wenzake Yakini na Zambe ili tu

wasiseme ukweli juu ya tabia na mienendo mibaya ya kiongozi huyo.

Msanii amemchora Faraji Changamoto ambaye ni Afisa Utawala wa

Shirika la Uhuduniaji wa miradi ya kilimo akitumia madaraka yake

vibaya, pale alipomlinda mfanyakazi mwenzake Yakini kwa kutomkata

mshahara baada ya kubainika kwamba ana kesi mahakamani kama

sheria zinavyoagiza. Yakini alikuwa ni rafiki yake na Faraji

Changamoto. Alitumia urafiki wao kuvunja sheria, rejea uk 26,

mwandishi anasema, “………kwa kawaida kama ninavyotegemea kwamba

unaelewa, mfanyakazi akiwa katika hali kama hiyo, hubidi

asimaishwe kazi na kukatwa nusu mshahara hadi idhihirike kwamba

hana hatia. Naona ugumu sana kukutendea jambo hili. Wengi wetu

tunatambua na kuithamini kazi yako na msaada uwapao wafanyakazi

wenzako kikazi. Sitafanya hivyo, japo natambua kwamba navunja

sheria. “Sitafanya hivyo kwako” (uk.26)”.

Pia tunamwona Gordon askari mpelelezi ambaye amechorwa na

mwandishi akitumia vibaya nafasi yake ya uaskari. Gordon anafanya

biashara haramu ya kuuza Almasi za Bandia. Pia anamlazimisha

Yakini kusaini hati ya maelezo bandia ili atiwe hatiani kwa

makosa ambayo hakuyafanya (uk .86).

Kwa ujumla katika ujenzi wa jamii mpya tabia hizi za utumiaji

mbaya wa madaraka hazipaswi kuvumiliwa. Jamii inabidi iamue na

kujitoa mhanga kupambana na hali hii. Rejea (uk 106-107). Msanii

amechora jamii inapambana na viongozi wanaohujumu rasilimali za

nchi. Msanii anasema “…………….. hapa kulikuwa na mamia ya watu

waliokasirika, kulikuwa na wengine zaidi waliokuwa wanakuja pale

kwa nguvu na hasira za kifaru………..” (uk 107). Hii dalili ya watu

kukataa tabia mbaya za viongozi wetu na kuamua kufanya mapinduzi

katika harakati za ujenzi wa jamii mpya.

Saula la Uonevu na Ukiukwaji wa haki za binadamu (Injustice)

Dhamira hii imejidhihirisha kwa kuangalia jinsi vyombo vya dola

vianvyokiuka haki za binadamu kwa kuwaonea wananchi ambao

wanapigania haki zao. Kwa mujibu wa (Wamitia K.W, 2003: 347),

vyombo kandamizi vya dola vinahusishwa na mtaalam Lous Althusser

kueleze vyombo vinavyotumiwa na tabaka linalotawala kudhulumu na

kukandamiza tabaka tawaliwa. Vyombo kndamizi vya dola ni asasi

ambazo hutumia njia za kukandamiza ili kuwafanya watu na hasa

wafanyakazi kulitii tabaka tawala. Vyombo hivi ni kama polisi,

magereza na majeshi.

Katika riwaya ya Almasi za Bandia Mwandishi ameonesha jinsi vyombo

vya dola vilivyokuwa vinawakandamiza watu wa tabaka la chini,

akina Yakini ambao walikuwa wanapigania haki za wafanyakazi.

Wafanyakazi hao walikuwa wakifanya migomo kwa kutetea maslahi ya

wakulima pamoja na wafanyakazi wadogo lakini tunaona kuwa nguvu

za dola zinatumika ili kuwagandamiza badala ya kuwasaidia.

“…. Polisi Polisi! Watoto wa wakulima wanawapiga virungu.

Watoto wa wenzao wa wakulima wanaotetea maslahi ya wakulima! Polisi! FFU! FFU!....

Suala la Matatizo ya Kiuchumi

Hali mbaya ya uchumi ni hali ambayo jamii inashindwa kupata

mahitaji muhimu kutokana na kipato chao kuwa kidogo. Hali hii

imejitokeza pale wanafunzi walipokuwa wanakula chakula chenye

wadudu na huku wengine wakikosa kabisa hata hicho chenye wadudu.

“………. Siku zilivyozidi kwenda ndivyo maisha yalivyozidi kuwa

mabaya. Watoto walikosa matunzo kutokana na wafanyakazi kupata

kipato kidogo watoto walizagaa wakiwa matumbo wazi” (uk .20).

“Baadhi walidai kuwa wanafunzi ndio wanaoonewa kwa kupewa chakula

chenye wadudu na wengine wakadai ilibidi wavumilie chakula hicho”

(uk.12).

Wahusika mbalimbali walichorwa katika riwaya hii wanaonekana

kutegemewa mfano Zambe alitegemewa na mama Sadiki pia mwanae

Sadiki. Pia Yakini alitegemewa na watoto wake na Tereza alipokuwa

chuoni. Pia Tereza alikuwa anampelekea mama yake pesa kidogo ya

kujikimu kimaisha inadhihirishwa na mwandishi anaposema,

“… Tereza Mtweza mtoto pekee kwa wazazi wake naye alikuwa ni

tegemeo kubwa kwa mama yake” (uk. 63).

Pia tunaona wanafunzi wakipanga kuandamana hadi ofisi ya magazeti

ya serikali kupinga kitendo cha viongozi kujipa marupurupu wakati

hali ya uchumi ilikuwa ni mbaya (uk.13). Vilevile njaa ilitawala

kila mahali nchini inadhihirishwa na mwandishi.

“…..Hali ya maisha ilikuwa mbaya sana nchini gharama ya maisha

ilikuwa imepanda maradufu na sehemu nyingine za nchi zilikuwa na

njaa si Dodoma, si Moshi” (uk.18).

Tukiangalia maisha ya sasa ya Tanzania elimu inayotolewa

haimwezeshi mwanafunzi kujitegemea hivyo jamii kuendelea kuwa na

hali mbaya kiuchumi hata wale waliopata elimu.

Suala la Rushwa na Ulaghai

Rushwa ni hali ya kutoa/kupokea fedha au kitu cha thamani ili

kutoa huduma Fulani. Rushwa inaweza ikawa kati ya mtu aliye

kwenye nafasi fulani au mtu aliye kwenye madaraka ya jambo fulani

ili mtoaji apewe upendeleo. Pia tunaona jinsi rushwa ilivyotawala

katika sehemu za kazi tunamwona Yakini akiwa Uwanja wa ndege

akielekea Londoni lakini walinzi wanamtaka alipe fedha za kigeni

kama ushuru wa uwanja kinyume na maelekezo ambayo yalikuwepo.

Baada ya kutokuwa na fedha za kigeni analazimika kulipa sh 500/=

badala ya 200/= ambazo alitakiwa alipe.

“… Kwa hiyo unatakiwa kulipa ushuru wako wa fedha za kigeni na si

za Tanzania. Wewe si rushwa bado ni tatizo katika maeneo mengi

nchini Tanzania mfano Jeshi la polisi, askari wa barabarani

wanaomba rushwa na kuwaachia dereva wazembe, mahakamani na

hospitalini pia.

Suala na Migomo

Migomo ni hali ya kukataa kufanya jambo fulani kutokana na

kutoridhishwa na mwenendo mzima wa utendaji wa jambo hilo na

kipatikanacho kutokana na jambo hilo. Katika riwaya ya Almasi za

Bandia.Vilevile tumeona migomo mbalimbali ikifanywa na wanafunzi

pamoja na wafanyakazi walikuwa wakifanya migomo kwa kutetea

maslahi ya wakulima pamoja na wafanyakazi wadogo.

“…. Polisi Polisi! Watoto wa wakulima wanawapiga virungu.

Watoto wa wenzao wa wakulima wanaotetea maslahi ya wakulima!

Polisi! FFU! FFU!....

“Japokuwa waajiri walitukubalia, lakini walikuwa

wamechelewa.Tayari tulikuwa tumeshaanza mgomo. Hatukwenda kazini

uk 2”. Pia katika uk 13, mwandishi ananukuu kwa kusema kuwa:

“Na wengine wakaona kwamba migomo ndiyo njia mojawapo ya

kurekebisha hitilafu katika jamii uk 13”. Hata katika jamii yetu

ya sasa, tumeona migomo mbalimbali ya walimu, madaktari na hata

wabunge wa upinzani katika bunge la Tanzania ambayo inatokana na

kunyimwa haki za msingi za makundi mbalimbali katika jamii.

Suala la Mapenzi na Ndoa

Mapenzi ni hali ya kuingiwa moyoni na kuthamini mtu au kitu zaidi

ya mwingine au kingine. Ni hisia zinazohusiana na mahaba au hisia

za ndani kati ya mume na mke au kwenye familia.

Ndoa ni muunganiko wa mume na mke kutengeneza familia.

Mwandishi anamwonyesha Yakini pamoja na Tereza jinsi walivyokuwa

na mapenzi ya kweli toka wakiwa chuoni hadi pale walipooana.

Tereza alikuwa na mapenzi ya dhati kwa mumewe na Yakini alimpenda

Tereza pia. Tunaona pale jinsi Tereza alivyokuwa akifuatilia

jinsi mume wake alivyopelekwa pale uwanja wa ndege na akaenda

kulipa ushuru aliotakiwa kulipa. Tunadhihirishiwa na mwandishi

anaposema

“…. Tereza mkewe Yakini alizitoa hizo shilingi mia tano.Yakini

aliondoka pale hima huku mzee masharubu akimtakia safari njema”.

(uk 6)

Vilevile tunamwona Tereza alivyomtafuta mtu wa kumwekea dhamana

mumewe Yakini pale alipokuwa amekamatwa na polisi. Mwandishi

anatudhihirishia kwa kusema,

“…. Ilikuwa awekwe chini ya ulinzi, lakini kwa bahati njema,

Tereza alikuja hima na mtu wa kumwekea dhamana…” (uk 11)

Suala la Ngono Zembe na Ukahaba

Ngono zembe ni hali/ kitendo cha kufanya mapenzi yasiyo salama na

kiholelaholela bila kutumia zana za msingi, yaani kufanya mapenzi

na mtu asiye mumeo au mkeo wakati. Ukahaba ni hali ya mwanamke

kufanya biashara ya ngono au kuuza mwili wake kwa ajili ya

kujipatia pesa/fedha au kipato. Mwandishi anaonyesha suala la

ngono zembe pale tunapomuona Merton akishiriki ngono na Jane

ambaye si mkewe na mkewe Gloria anafumania. “……naye Gloria

alimtazama kisha akatazama kitandani Merton alikuwa amemlalia

Jane akimbusu kwa mapenzi motomoto..” (uk 97). Pia wanawake

wakubwa weusi walivyokuwa wakijihusisha na ngono zembe na vijana

wadogo. ukahaba ulivyokuwa ukifanyika ambapo wanaume wazee

walikuwa wakitembea na watoto wadogo kama binti zao wa kuwazaa

lakini ni katika hali ya kutaka kupata raha ya kijinsia. Vilevile

wanawake wakubwa nao pia kuchukua wavulana wadogo kwa lengo la

kutimiza raha zao kijinsia. Inadhihirishwa na mwandishi pale

anaposema;

“…. Unakaona kale kajamaa kafupi kale? Basi kanatoka Malawi. Sasa lile limama lizee,

nene na refu vile sijui katalipeleka wapi? Katamezwa na hilo jike” (uk 36)

Tunaona jinsi wanawake walivyofanya ukahaba kama ni biashara. Mwandishi

anasema;

“…. Waliwapa bei za huduma mbalimbali, kama ni kwenye maficho ya mlemle mitaani

bei ilikuwa nafuu, na kama ilibidi waende wote nyumbani basi bei iliongezeka zaidi” (uk

40).

Starehe

Hii inajidhihirisha pale ambapo akina Yakini wanaonekana

wakipenda mambo ya starehe kama kunywa pombe na kwenda kucheza

dance katika baa ya Western ambapo kuna mijimama ya Kiafrika

inayofanya mapenzi na vijana wadogo. Hii inajidhihirisha pale

wanapoonekana katika sehemu za starehe, Yakini na wenzake wakiwa

masomoni Uingereza ambapo kulikuwa na sehemu za starehe za

wazungu peke yao na Waafrika peke yao, kama vile mabaa. Hii pia

ianonesha jinsi Wazungu walivyokuwa na mtazamo hasi kuhusu

Waafrika. Kwa mfano pale wanapoambiwa na mtu mmoja, “Kwanini

hamkwenda kwenye baa ambazo zinatembelewa na watu weusi, badala yake mkaja

hapa?” (uk.41).Mbali na starehe ya kucheza dansi na kunywa, Yakini

na rafiki zake walioneakana kujihusisha na masuala ya kimapenzi

na wanawake waliikuwa wakijiuza baa. Kwa mfano pale

Suala la Ubakaji

Ubakaji ni kitendo cha kulazimisha kufanya mapenzi au ngono kwa

nguvu bila ridhaa ya mhusika. Katika riwaya hii tunaona jinsi

Vilevile mhusika mwingine Merton Mpwito anaonekana akimbaka binti wa Kihindi

aitwaye Patricia Tereza, ambapo alimfanyia tendo hilo bila ridhaa yake. Mwandishi

anadhihirisha hayo pale anaposema;

“….. Usinisogelee! Ukinisogelea nitapiga kelele! Merton alicheka kwa ufedhuli na

kumjibu, unapoteza wakati wako bure. Hakuna atakaye kuamini. Hukuja hapa kwa

kulazimishwa, wewe mwenyewe umejileta!!”….aliivuta chupi yake yule msichana na

kuichanilia mbali bila ya huruma wala kujali. Alikuwa anahema kama faru na kutoka

udenda wa uchu” (uk 70-71)

Nafasi ya Mwanamke Katika Jamii

Kwa kuangalia nafasi ya mwanamke katika jamii, msanii amemchora

mwanamke katika nafasi mbalimbali ndani ya riwaya hii ya Almasi za

Bandia chanya na hasi. Kwa kiasi kikubwa katika riwaya ya Almasi

za Bandia, mwanamke amechorwa katika nafasi hasi.

Kwa upande wa nafasi hasi, mwanamke amesawiriwa kama kiumbe

kinachonyanayaswa ambapo hali hii huletelezea ukatili na

unyanaysaji wa kijinsia kama inavyojidhihirisha katika maelezo

yafuatayo:

Kwanza mwanamke amechorwa kama kiumbe duni kinachokandamizwa

katika jamii katika kipengele cha mapenzi. Hii inaonyesha kwamba

mwanamke amechorwa katika nafasi hasi. Tunaona jinsi Patricia

alivyokamatwa kwa nguvu na kunajisiwa na Merton Mpwito (uk 3)

Pia tunaona kitendo alichofanyiwa Patrisia kwa kubakwa na Merton

Mpwito (uk 62).

“…. Umesema Merton Mpwito alikukamata kwa nguvu na kukunajisi?”

Pia jamii ilimnyanyapaa Tereza baada ya kufukuzwa chuo kikuu

aliposhiriki kwenye maandamano, kwahiyo jamii ilimwona kuwa ni

dhalimu maradufu katika jamii kule kijijini kwao (uk 63).

Pili msanii anaendelea kuonyesha jinsi wanawake wanavyokandamizwa

na kunyanyaswa katika jamii, katika asasi ya kiutamaduni wa

kiafrika. “…. Lo! Wanawake duniani ni kundi moja kubwa la watu

wanaoonewa! Yaelekea jamii zote zimejaa ngono za kuhalalisha

uonevu….” (uk 62)

Tatu, msanii amemchora mwanamke kama chombo cha starehe (uk 40)

tunaona wanawake wakiuza miili yao mitaani. Msanii anasema “…..

wanawake waliuliza kama wanataka biashara? Pia katika (uk 28)

tunamuona mwanamke akigombaniwa na wanaume ili aende

kuwastarehesha kimapenzi (uk 36-37) Msanii anasema “….. kijana

alipigwa hadi kung’olewa meno kwa sababu ya kugombea hawa

wanawake.

Kwa upande chanya mwanamke amechorwa kama mtu anayeweza kuleta

maendeleo. Kwa mfano, mwanamke amechorwa kama kiongozi na

mwanamapinduzi na mtu shujaa anayeweza kuongoza jamii yake katika

kupambana na maovu. Pale tunapomuona Tereza akiongoza na

kuhamasiha maandamano ya wanafunzi wenzake pale chuo kikuu cha

Dar-es-salaam, wakitetea haki za wakulima na wafanyakazi.

Wakipinga kitendo cha viongozi kijipa marupurupu wakati ilikuwa

wazi kwamba hali ya nchi kiuchumi ilikuwa mbaya…” (uk 16) …..

huyu msichana aliitwa Tereza. Alikuwa amemuona usiku wa jana yake

wakati alipokuwa amejitokeza jukwaani kutoa maoni yake na

mawaidha kuhusu mbinu za kutumia katika maandamano….. (uk 16).

Pia mwanamke amechorwa kama mshauri mzuri wa wanaume na mwenye

upendo. Msanii amemuonyesha Tereza kama mwanamke jasiri

mfuatiliaji wa haki na mwenye upendo kwa Yakini amabaye ni mume

wake, pale alipotafuta mtu wa kumwekea mumewe dhamana (uk 116)..“

tereza alikuja hima na mtu wa kumwekea dhamana”.

Sita, msanii amemuonyesha mwanamke kuwa ni mtu mwenye msimamo,

pale Patricia alipokataa kwenda ugenini, “….. Patricia alisema

sikujua kama ninyi mna mawazo ya ubabe wa kiume, kwamba kuna kazi

fulani za wanawake tu. Karne ya ishirini hii! (uk 68)

Hata leo katika jamii zetu mwanamke anachukuliwa kwa namna chanya

na hasi mfano mwanamke ana chukuliwa kama mlezi, mchapakazi,

jasiri na mshauri katika jamii. Pia amechukuliwa kwa namna hasi

kwani anatumiwa kama chombo cha starehe, kufanya kazi ndogondogo

kama vile kupika, kufua na kuangalia watoto.

Suala la Ukatili na Unyanyasajiwa Kijinsia

Ukatili na unyanayasaji wa kijinsia ni masuala ambayo yana uhusiano

wa karibu. Suala la unyanyasaji wa kijinsia ni suala ambalo linatokea

sana katika jamii zetu za sasa na limekuwa ni chanzo na tatizo la

kuleta mifarakano katika jamii. Katika jarida la FEMA (2010, Des),

linaeleza kuwa unyanayasaji wa kijinsia ni tendo lolote lenye mtazamo

wa jinsia linaloweza kumsababishia mtu adha au kero, madhara na mateso

ya kimwili, kisaikolojia na kingono. Unyanayasaji wa kijinsia unatokea

kwa watu wengi hasa wasichana na wanawake kupewa mimba na kutelekezwa,

kupigwa, kudhulumiwa haki zao za msingi. Mifano ya unyanayasaji wa

kijinsia ni kama ifuatavyo: Kwanza, unyanaysaji wa kimwili kwa kumpiga

mtu au kumtishia mtu wa jinsia tofauti kwa silaha. Pili, unyanyasaji

wa kisaikolojia kwa kumdhalilisha mtu, kumtishia kumwacha na kumnyima

mahitaji mtu anayekutegemea. Tatu, unyanayasaji wa kingono kwa kumbaka

mtu, kufanya ngono na watoto wadogo na kumshikashika mtu bila ridhaa

yake. Hii yote ni sehemu ya ukatili na unyanyasaji wa kijinsia.

Suala la Ubaguzi wa Rangi

Ni kitendo cha kutowathamini au kuwatenga binadamu kwa misingi ya

rangi za ngozi zao.

Katika dhamira hii ndogo pia msanii Chachage ameonyesha jinisi

wazungu walivyokuwa wakiwabagua watu wengine wakiwaita weusi,

mfano waafrika na wahindi. Waliwadharau na kuwanyanyasa kwa

kuwalipa ujira mdogo.

“ bwana mkubwa, kwanini mnaendelea kuwalipa Waafrika ujira mdogo na wazungu

ujira mkubwa pamoja na marupurupu mengi!” (uk 18-19)

“ ndio kijana, iko tambua ninyi ishi hali ngumu. Lakini kila mutu nalipwa kwa jinsi yake.

Fanya kaji mingi African hapana soma na iko vivu. Hapana kuwa kama European.” (uk

19)

“ hapana kataa iko jusi African kuwa tofauti na European’’ (uk 19)

Ubaguzi wa aina hii makazini/maofisini bado upo katika jamii zetu

za sasa, kwa mfano katika mabenki hapa nchini yanayomilikiwa na

wazungu au wahindi nafasi zote za juu zinashikiliwa na wao na

waafrika wanaishia kuwa makeshia, wafagizi na walinzi. Hii pia

tunaiona katika makampuni ya uwekezaji kama Tigo, Airtel, Vodacom

na migodini nafasi zote za juu ni za wazungu na wahindi wakati

waafrika wanafanya kazi ngumu kwa ujira mdogo.

“Penye kituo cha magari moshi yapitayo chini ya ardhi alikutana

na mashabiki wa mpira wa timu ya Rangers, wacha wamzomee,

wakimwita mtu wa Katanga, Nignog ambalo ni tusi maarufu la

wazungu kwa waafrika linalomaanisha mwanaharamu mweusi!Rudi kwenu

we mwanaharamu mweusi. Yakini alikasirika sana” (uk 32)

Hata sasa bado ubaguzi huo upo katika nchi za Ulaya katika

viwanja vya michezo, mashabiki wa kizungu na wachezaji wa kizungu

wanapowazomea na kuwatukana wachezaji wa kiafrika. Mfano,

Balotelli mchezaji wa taifa la Italia alipotupiwa ndizi kiwanjani

kwa kuashiria yeye ni nyani mweusi na John Terry alivyotoa lugha

chafu kwa Fednand wa uingereza na Suarez alivyomkashifu Patrick

Evra wa Ufaransa kwa kuwa wanarangi/ ngozi nyeusi, hayo yote

yanaonyesha jinsi ubaguzi wa rangi ambavyo bado upo katika baadhi

ya watu huko Ulaya.

Pia ubaguzi wa rangi unaonekana katika sehemu za starehe pale

kina Yakini na wenzake wakiwa masomoni Uingereza ambapo kulikuwa

na sehemu za starehe za wazungu peke yao na waafrika peke yao,

kama vile mabaa. Hii pia ianonesha jinsi Wazungu walivyokuwa na

mtazamo hasi kuhusu Waafrika.

“Kwanini hamkwenda kwenye baa ambazo zinatembelewa na watu weusi, badala yake

mkaja hapa?” (uk. 41).

“Baada ya muda mfupi Yule kijana aliwaasa tena kwamba ile baa haikuwafaa, ilifaa

waende kwenye baa ya watu wa aina yao” (uk. 42).

Ubaguzi wa aina hii pia bado upo katika baadhi ya nchi hapa

Afrika na hata Ulaya. Kwa mfano Afrika ya Kusini.

Katika kipengele kingine cha ubaguzi wa rangi tunaona wazungu

wakiamini kwamba waafrika ndio wanaofanya biashara ya madawa ya kulevya na ndio

sababu iliyopelekea Yakini na Chaupele wakamatwe na askari polisi pale uwanja wa

ndege wa Amsterdam.

“Basi wote waliochukuliwa hapa ni waafrika watupu.Kisa? Kwa kawaida wanawashuku

watu weusi kuwa ndio wauza bangi na madawa ya kulevya. Hakuna hata mzungu

mmoja aliyechukuliwa…” (uk 48)

Hali hii ipo hata sasa kutokana na matukio mengi ya hivi karibuni

ya baadhi ya waafrika wengi kukamatwa katika nchi za ughaibuni

wakiwa na madawa ya kulevya. Chanzo ni umaskini unaosababisha

watu kutamani/kutaka utajiri wa haraka kwa uvivu wa kufanya kazi

halali na kutumiwa katika usafirishaji wa madawa hayo kwa maslahi

ya wafanyabiashara wakubwa wa mataifa makubwa.

Suala la Elimu

Ni tendo au uzoefu wenye athari ya kujenga akili, tabia ama uwezo

wa kimaumbile wa mtu binafsi. Katika dhana ya kiufundi, elimu ni

njia ambayo hutumiwa kimakusudi na jamii kupitisha maarifa, ujuzi

na maadili kutoka kizazi kimoja kwenda kizazi kingine.

Msanii anawachora wahusika kama Yakini, Tereza, Zambe na wengineo

ambao walikuwa masomoni Chuo Kikuu ambapo waliweza kuandaa migomo

ya kupigania haki za watu wa kipato cha chini. Elimu yao

iliwawezesha kujiamini na kuandaa mipango hiyo kwani kile

walichokuwa wanakipigania kilikuwa na faida kwa jamii nzima.

Tunathibitishiwa na mwandishi anaposema;

“ Jumapili ya tarehe tano mwezi wa tatu, wanafunzi walionekana

wakiteremka mjini, wakiwa wamebeba mabango na nyoyo zao zikiwa

zimejaa hamasa za kimapinduzi” (uk 14)

Hali hii bado inaendelea kujitokeaza katika jamii yetu ya sasa,

wasomi wa vyuo vikuu hugoma kutokana na hali ya kutotimiziwa haki

zao za msingi, kama vile Bodi ya mikopo ya Elimu ya juu

kuwacheleweshea mikopo yao yaani kutowapa kwa wakati. Mfano mwaka

jana tuliona Chuo Kikuu cha Dodoma. Pia walimu na madaktari

waligoma kwa kutotimiziwa maslahi yao na vitendea kazi.

Msanii anaelezea kuhusu elimu kwamba, kiwango kikubwa cha elimu

kinaweza kusababisha mtu apate kipato kikubwa ili hali elimu

ndogo inafanya mtu apate kipato kidogo.

“Aliajiriwa katika bandari ya Dar-es-salaam kama mnyampara.

Alikuwa na kipato kikubwa kuliko mamia ya vibarua walioajiriwa

pale, lakini kwa madarasa yake mawili aliyosoma hakufua dafu kwa

makarani waliosoma kuliko yeye’’ (uk 18)

Hali hii inasawiri hali halisi ya muktadha wa waajiriwa katika

sekta mbalimbali serikalini na hata katika mashirika, taasisi na

makampuni mbalimbali nchini.

Imani na Itikadi za Kichawi na kishirikina

Msanii ameelezea suala la imani katika pande mbili, imani ya dini

na imani za kishirikina. Anaelezea imani ya dini kwamba ni

kumtegemea Mungu pale anaposema,

“Hawa wakristo walipinga kabisa imani ya kwamba iliwezekana watu kujilinda kama

jumuiya, kwani walidai kwamba ulinzi ilikuwa ni kazi ya Mungu na si ya binadamu.

Kwa hiyo wakakataa kushiriki katika migowe, shughuli za jumuiya na matambiko

yaliyowahusisha wahenga”. (uk 64). Pia mwandishi kwa upande mwingine

anaongelea imani za kishirikina jinsi zilivyopigwa vita pale

anaposema,“Baba yake Tereza hakuepukana na matatizo hayo, kwani

wakati wa uhuru na baada ya hapo kulikuwa na vita vikali dhidi ya

ushirikina na matibabu ya mitishamba…” (uk 65),“mara kukatokea

wimbi la imani kwamba kuna mtu aitwaye Chikanga huko Nyasaland

aliyeweza kuwatoa watu tunguri zao”.

Hii pia inadhihirisha hali halisi ya muktadha wa maisha ya sasa,

wasomi wengi hawaamini na wanapinga ushirikina, wao wanaamini na

kumtegemea Mungu peke yake ambapo jamii ya watu wasiosoma wengi

wanaamini sana ushirikina.

Suala la Kuiga Utamaduni na Mambo ya Kigeni

Utamaduni ni uzoefu wa kimaisha wa kundi la watu au jamii fulani

Utamaduni hujumuisha michakato ya kijamii ambayo huiwezesha jamii hiyo

kujielezea, kujitambulisha na pamoja na kufanya shughuli zakila siku,

(Wamitila, 2003:330). Mara nyingi vijana huwa wa kwanza kufuata

mienendo na matendo mipya ya maisha kwa kuwa huwa hawajazama katika

mfumo maalum wa maisha na wana matamanio makubwa ya kujaribu mienendo

mipya. Kwa hiyo ni rahisi kwa vijana kubadilika kwa vile imani zao za

kimsingi huwa zinaendelea kujengeka, (Wafula,1999: 18). Utamaduni ni

uzoefu wa kimaisha wa kundi la watu au jamii fulani Utamaduni

Katika riwaya ya Almasi za Bandia, mwandishi ameonyesha jinsi ambavyo

wanajamii imevamiwa na kuiga mambo ya Kizungu ikiwemo utamaduni wa

kigeni na masuala mengine hasa mambo ya usasa. Katika kuchambua

dhamira hii utamaduni wa kigeni na wa vipengele kama lugha, shughuli

za kiuchumi, matendo ya wahusika, uongozi, siasa na mtindo wa maisha

kwa ujumla kama vile mavazi, vyakula, mila na desturi vitaangaliwa.

Kwa mfano, Yakini na wenzake walivyokuwa Ulaya walikuwa wakienda

kucheza madansi ya Kizungu kwenye hoteli za kizungu. Almasi za Bandia

inaashiria/inawakilisha Waafrika Weusi wanaoiga tamaduni na mambo ya

Ulaya hususani pale wanapopata nafasi za kwenda Ulaya. Waafrika hawa

wameacha utamaduni wao na kuiga utamaduni wa Kizungu ambao

umefananishwa na Almasi za Bandia. Mfano, mhusika Merton na Wazungu.

Almasi za Bandia pia inawakilisha Wazungu wanaojifanya kuonea huruma

Bara la Afrika na kutoa misaada kumbe mioyoni mwao na katika hali ya

ukweli wanataka kuendelea kuwanyonya Waafika.

Motifu

Katika riwaya ya Almasi za Bandia, motifu zinazojitokeza ni motifu ya

safari na motifu ya msako. Hii inajidhihirisha kwa kumwangalia mhusika

Yakini anavyofunga safari toka Tanzania kwenda kusaka elimu nchini

Glasgow, Uingereza ambapo alifanikiwa kumaliza elimu yake ya Chuo

kikuu lakini alipata changamoto nyingi sana kuanzia alipoanza safari

yake pale Airport ya Dar es Salaam kwenda Ulaya. Yakini kule Ulaya

anakutana na kundi la vijana wa Kiafrika ambao wamejiingiza katika

matendo mbalimbali kama starehe na mengineyo, ambao kwa matendo yao na

vitu wanavyovifanya wanaibua dhamira mbalimbali kama elimu, starehe,

uuzaji wa madawa ya kulevya n.k Motifu hizi za safari na msako wa

elimu zinaibua dhamira na migogoro mbalimbali kama vile unyanyasaji wa

kijinsia, ubakaji Merton kumbaka Patricia ambayo hivi vinaibuliwa na

Yakini ambaye anaamuuliza Partricia mweneyewe.

Suala la Migogoro

Migogoro ni kipengele kimojawapo kinachotumika kuelezea maudhui.

Kutokana na mivutano inayotokea katika kazi ya fasihi, yanazuka

matukio ambayo yanasaidia katika kupata maudhui. Wamitila (2003)

anaeleza kuwa mgogoro hutumiwa kurejelea mvutano unaokuwako kati ya

mhusika mmoja na mwingine katika kazi ya fasihi au katika akili ya

mhusika mmoja. Migogoro ni sehemu muhimu katika msuko wa kazi ya

fasihi na huchukua sehemu kubwa ya kazi hiyo. Mgogoro hujitokeza kwa

njia mbalimbali. Senkoro ( 1982:4 ) anaeleza kuwa katika kazi ya

fasihi kuna migogoro kati ya wahusika, ama vikundi vya wahusika,

familia zao, matabaka yao na kadhalika. Migogoro yaweza kuwa ya

kiuchumi, kiutamaduni au kisiasa. Halikadhalika kuna migogoro ya

kinafsia ambayo inatokea katika nafsi ya mhusika.

Katika riwaya ya Almasi za Bandia ipo migogoro mingi ambayo imejitokeza.

Migogoro hiyo yaweza kuwa kati ya makundi ya watu na migogoro ndani

ya mhusika mwenyewe yaani migoggoro nafsia. Ifauatayo ni aina ya

migogoro iliyojitokeza kwenye riwaya ya Almasi za Bandia:

Migogoro ya watu wawili

Mgogoro kati ya Patricia na Merton

Chanzo cha mgogoro wao ni Merton kutaka mapenzi kwa Patricia.

Suluhisho ni Merton kumbaka Patricia. Je kulikuwa na suluhisho la

mgogoro?

Mgogoro kati ya Yakini na Merton

Chanzo chake ni kusingiziwa kwa Yakini kwamba, alimtumia

majambazi wakampiga. Suluhisho ni Merton kusema ukweli kwamba

alipigwa na wahindi kwa ajili ya kuwauzia almasi za bandia.

Mgogoro kati ya Gloria na Merton

Chanzo ni Gloria kumfumania Merton akiwa na Jeni. Suluhisho ni

Merton na Gloria kusuluihishwa na mjumbe wa nyumba kumikumi.

Mgogoro kati ya Zambe na Merton Mpwito

Chanzo chake ni Merton anadai Zambe anamchafulia jina lake.

Suluhisho ni barua ya wasafirishaji mizigo ambayo iliarifu kwamba

mizigo imefika salama.

Migogoro ya makundi

Mgogoro kati ya wanafunzi wa chuo kikuu na serikali

Chanzo ni wanafunzi kupinga kitendo cha viongozi kujipa

marupurupu wakati hali ya uchumi ilikuwa mbaya. Suluhisho ni

wanafunzi kuandamana kupinga kitendo hicho.

Mgogoro kati ya wananchi na viongozi kina inspekta Gordon.

Chanzo ni kumgonga mtu kwa gari la akina inspekta Gordon.

Suluhisho ni wananchi wenye hasira kali kuwapiga mawe na kuwauwa

kina Inspekta Gordon na Athuman.

Falsafa

Katika riwaya hii ya Almasi za Bandia, msanii anaamini kuwa kuna

unafiki/ ubandia katika nyanja au nafasi mbalimbali zinazoshikwa

na watu mbalimbali katika jamii ndani na nje ya Tanzania kwa

ujumla si kitu kizuri. Kwa mfano, ubandia wa viongozi ambao

wanaahidi kuwahudumiwa wananci lakini mwisho wa siku wanaenda

kinyume na maagano ambayo huletezea kuwa na uongozi mbaya.

Ubandia/ unafiki wa Wazungu kujifanya kuwa wanawapenda Wafrika

kwa kuwapa misaada na kufungua vitega uchumi mbalimbali kumbe nia

yao kubwa si kuwasaidia Waafrika bali kuwanyonya kiuchumi.

Pia msanii anaamini na kuonyesha kuwa ili kuweza kuondoa Almasi

hizi za Bandia, inabidi kuwe na ushirikiano mzuri katika jamii

ambao ni jambo muhimu kukuza jamii katika nyanja zote kisiasa,

kijamii, kiuchumi na kiutamaduni. Tena anaamini kuwa palipo

mvutano kati ya wema na ubaya lazima wema utashinda na kwamba

haki ya mtu haipotei hivihivi. Mwisho wa ubaya ni aibu.

( Ubaya alioufanya Merton kuuza madini bandia na baadae kupigwa.

Kisha akamsingizia Yakini kwamba ndiye aliyetafuta watu wampige

baadae tunamwona akiaibika baada ya kosa lake kugundulika).

Ujumbe katika Riwaya ya Almasi za Bandia

Umoja ni nguvu utengano ni udhaifu, wananchi walijiunga na

wanachuo kwenye maandamano wakiwa wamebeba mabango yaliyopinga

unyonyaji na kuunga mkono ujamaa huku yakilaani kitendo cha

viongozi kujiongezea maslahi (uk 14).

Mwanamke katika jamii ni lazima athaminiwe, aheshimiwe na

kushirikishwa katika maamuzi, Yakini alimshirikisha Tereza katika

mabo yote wakiwa bega kwa bega mfano ni pale wakati Yakini

alipoambiwa alipe shilingi mia tano mkewe Tereza alimlipia, pia

Tereza alionekana akimleta mtu wa kumwekea dhamana Yakini

(mumewe) (uk 5-6), (uk.11)

Uongozi mbaya ni adui wa maendeleo. Merton na Inspekta Gordoni

wanaonekana wakitumia vibaya dhamana zao za uongozi kwa kufanya

biashara haramu ikiwa ni pamoja na kutishiana kutokana na

madaraka waliyokuwa nayo (uk.110).

Kusingiziana si tabia nzuri kwa watu kwani inawezekana kutia watu

katika hasara, majonzi na sintofahamu, pia na kuleta utengano

mkubwa. Hali hii inaonekana pale Merton Mpwito akimsingizia

Yakini kuwa ndiye aliyemvamia na kumjeruhi. Usemi huu

unadhihirishwa na Merton Mpwito pale alipokiri mwenyewe alipokuwa

hospitali kuwa alipigwa na mzungu Gregory na Yule mhindi Kanjir,

aliendelea kueleza kuwa kaka yake Gordon na Athumani walikuwa

wamenipa Almasi za kumpelekea Gregory hotelini kwake. (uk 110-

111).

Hali ya kuwa na ubaguzi katika jamii sio kitendo kizuri kwani

huweza kukwamisha maendeleo na kuleta vita vikali. Hali hii

inaonekana pale ubaguzi wa rangi unapofanyika kati ya weupe dhidi

ya weusi na kuleta ugomvi wa mara kwa mara na vifo

visivyotarajiwa (uk.42).

Mbio za sakafuni huishia ukingoni, Merton na kaka yake Inspekta

Gordon walijitafutia utajiri wa haraka haraka kwa kuuza almasi za

bandia na wakaishia kufa.

Msimamo

Mwandishi ana msimamo wa kimapinduzi kwa kuyatolea macho matatizo

yanayoikabili jamii katika kujikomboa kutokana na ukandamizaji

unaofanywa na viongozi wa Kiafrika na unyonyaji na ukandamizwaji

toka kwa Wazungu. Kwa mfano, Yakini ametumiwa na mwandishi kama

kipaza sauti cha kuleta mapinduzi haya na hatimaye anakamatwa na

kutiwa mbaroni bila kosa lolote. Mfano, Yakini anatengenezewa

kesi, anakamatwa, anateswa bila kosa lolote, viongozi wanakaa

kikao Wete Pemba cha kujiongezea maslahi wakati jamii inateseka.

Mwisho kunatokea maandamano/migomo kwa wanafunzi, wakulima na

wafanyakazi ambayo inaashiria kupinga hali za kionevu ili kuleta

mapinduzi.

Hitimisho

Almasi za Bandia ni riwaya inayosadifu mifumo ya siasa, uongozi na

masuala mbalimbali ya kijamii kama uchumi siasa na utamaduni na

kuonyesha jinsi watu wanvyopambana ili kukabiliana na kubadilisha

mifumo hiyo kandamizi katika nchi ya Tanzania na Afrika kwa

ujumla. Hivyo mwandishi ameonesha mapambano kati ya makundi

mbalimbali ya kijamii ili kuleta mapinduzi hayo hususani uongozi

na tabaka la chini la makabwela.