Upload
others
View
10
Download
0
Embed Size (px)
Citation preview
TAASISI YA UTAFITI NA UTETEZI WA HAKI ZA ARDHI
(HAKIARDHI)
MADA:- UCHAMBUZI WA MAENEO MUHIMU YANAYOWAGUSA WAZALISHAJI
WADOGOWADOGO KATIKA BAJETI YA WIZARA YA ARDHI, NYUMBA NA
MAENDELEO YA MAKAZI
MADA HII IMEWASILISHWA KATIKA SEMINA YA MWEZI JULAI, 2010 KATIKA
UKUMBI WA TAASISI YA HAKIARDHI.
MTOA MADA:- CATHBERT TOMITHO
JULAI 23, 2010
[Mada hii imejikita zaidi katika kuchambua masuala muhimu katika bajeti ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa kuangalia maeneo muhimu yanayowagusa wazalishaji wadogowadogo kwa yale
yaliyotekelezwa kwa mwaka 2009/10 na uhalisia wake pamoja na yale yaliyopangwa kwa mwaka 2010/11. Hii
ikiwa ni pamoja na kuangalia vipaumbele vilivyowekwa na Wizara katika kupambana na matatizo na changamoto
katika sekta ya ardhi ili kulinda haki za wazalishaji wadogowadogo katika kupata, kutumia na kumiliki ardhi.]
2
UCHAMBUZI WA MAENEO MUHIMU YANAYOWAGUSA WAZALISHAJI
WADOGOWADOGO KATIKA BAJETI YA WIZARA YA ARDHI, NYUMBA NA
MAENDELEO YA MAKAZI.
Utangulizi
Bajeti hii ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya
Makazi iliwasilishwa Bungeni mapema mwezi Julai 2010 na Waziri mwenye dhamana ya
Wizara husika Mhe. John Zefania Chiligati.
Lengo hasa la uchambuzi huu ni kuonyesha na kujadili kwa pamoja kama wadau wa Ardhi
masuala ambayo Wizara imetekeleza kwa kipindi cha mwaka 2009/10 pamoja na kuchambua
yale yote yaliyopangwa kufanyika katika mwaka 2010/11. Mjadala huu utatupa nafasi ya kupata
picha ya jumla ya nini serikali imepanga kufanya na sisi kama wadau mahsusi tuna nini cha
kusema ambacho hata kama hakitakuwa na athari kwenye bajeti ya mwaka huu lakini italeta
mabadiliko katika mwaka unaokuja; muhimu zaidi ikiwa ni kupata hoja za msingi kabisa za
kuwahoji wabunge wetu na watendaji wa serikali kuhusu sekta nzima ya Ardhi.
Katika uwasilishi wa uchambuzi huu mada itajikita kwa kifupi zaidi katika kuangalia baadhi ya
vipengele muhimu katika bajeti hasa vile vinavyogusa moja kwa moja maeneo ya wazalishaji
wadogo wadogo kwa maana ya wakulima, wafugaji, na watumiaji wengine wote wa ardhi.
Katika mtiririko wake uchambuzi huu umegawanyika katika sehemu kuu mbili; kwanza
uchambuzi wa maeneo ambayo Wizara imetekeleza kazi kwa mwaka 2009/10 kwa kuangalia
umuhimu na uhalisia wa kile kilichofanyika pamoja na tarakimu za asilimia zilizotolewa na
Wizara kama zinaendana na ukweli wa kile kilicho katika maeneo husika ya utekelezaji na ikiwa
ni kweli au la kuwa kuna mabadiliko chanya kutokana na kile kilichotekelezwa kwa mwaka
uliopita na kwa miaka mitano inayohitimika mwaka huu. Sehemu ya pili ya mada itachambua
vipaumbele kama vipo vilivyowekwa na Wizara kwenye bajeti ya mwaka 2010/11 katika
kuhakikisha kuwa rasilimali ya ardhi inakuwa yenye tija kwa wananchi na taifa zima.
SEHEMU YA KWANZA
UCHAMBUZI WA BAADHI YA MAENEO MUHIMU KWENYE BAJETI
1. Kuanza kwa utekelezaji wa Mkakati wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara Tanzania
(MKURABITA) kwa lengo la kuwezesha Watanzania kurasimisha ardhi na nyumba zao
ili waweze kuzitumia kupata mikopo ya benki na mifuko mingine ya fedha inayokopesha.
Lengo la kuanzisha Mkakati wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara Tanzania ni kurasimisha
rasilimali vijijini ili wananchi wapate vyeti ambavyo watavitumia kwa manufaa katika kuongeza
uzalishaji na kutumia rasilimali zao kujipatia mitaji. Pamoja na wadau wa Mkurabita wenyewe
kukubaliana na changamoto za Mkakati huu hasa kwenye kile kinachoitwa wananchi kutumia
rasilimali zao katika kupata mitaji kupitia vyombo na taasisi za kifedha. Na katika kupambana na
uwezo huu mbovu wa Mkurabita katika kuwasaidia wananchi kupata, kutumia na kumiliki ardhi
yao uku wakitajirika kwa kupata mitaji kupitia mikopo ndio maana watekelezaji wa Mkakati huu
wamekuja na hoja ya kufutilia mbali sheria ya ardhi ya vijiji Na. 5, 1999. Jambo ambalo
kimsingi likitekelezwa na serikali ndio utakuwa mwisho wa uhakika wa wazalishaji wadogo
3
wadogo kwa maana ya wakulima, wafugaji, waokota matunda na wachimbaji wadogo wadogo
wa madini kupata, kutumia na kumiliki ardhi.
Utekelezaji wa MKURABITA unatambulika kwa athari mbali mbali ulizozileta katika kuweka
hai uhakika wa wazalishaji wadogo wadogo hasa wale wanaotumia umiliki wa kimila; mifano
mizuri ni kule Handeni, ambapo baadhi ya wafugaji walikosa umiliki wa maeneo yao kwa kile
cha kutotambulika na kukubalika kama wazawa wa vijiji husika. “Lakini suala la nani aliyesema
kuwa hawa sio wakaazi halisia wa maeneo yale ni suala la kujiuliza na kujadili”. Kwanza
itambulike mapema kuwa Mkakati huu toka kwenye vifundo vya kibepari ni katika harakati za
kuua na kuuzika umilki wa kutumia mila. Kwa maana nyingine Mkakati huu ni kifo cha sheria
ya Ardhi ya Vijiji ambayo ipo katika kusimamia maslahi na mahitaji ya wazalishaji wadogo
wadogo.
Swali la msingi la kujiuliza kuhusu Mkakati huu ni yako wapi yale mafanikio au zile ndoto
ambazo waasisi wake walikuwa wanaziota? Je hati hizo kwenye wilaya na vijiji hivyo ambavyo
vimefanikiwa kupata zimeleta mafanikio gani ambayo yanaweza kuwa au kuleta morali kwenye
kuuendeleza Mkakati huu kwa moyo wa unyenyekevu na wa dhati. Kimsingi bado hakujawa na
mafanikio kutokana na kukosekana taasisi za kifedha ambazo zimelenga katika kuinua maisha ya
watumiaji/wamiliki wadogo wadogo. Vikundi kama SACCOS na VICOBA haviwezi kuingia
katika eneo hili kutokana na kujiendesha katika mifumo mingine mingine kabisa ya kibiashara
Suala jingine ni uhakika wa kukamilika kwa Mkakati huu kwa wakati, kutokana na serikali
kuendelea kushinikiza utekelezaji wa Mkakati basi kungewekwa kwa mikakati mingine ambayo
ingeharakisha na kuusukuma utekelezaji wa Mkurabita ili kuachana na dhana ya kuutumia
Mkakati huu kama chapuo la kila baada ya miaka mitano. Pamoja na kupata fedha kutoka katika
bajeti ya serikali na wafadhili bado utekelezaji wake umekuwa wa kusuasua zaidi jambo ambalo
halionyeshi nia dhabiti katika kuukamilisha Mkakati huu.
Jambo ambalo Wizara na wadau wengine wa ardhi wanatakiwa kulitambua ni kuwa urasimishaji
sio suala la kuundiwa Mkakati ila ni suala hatua linalokuwa na kuota mizizi lenyewe kwa kuwa
sehemu ya utamaduni wa jamii husika kutokana na changamoto za kimaendeleo na mabadiliko
ya ukuaji wa kiuchumi ya muda kwa muda yanayotokea katika jamii husika. Kwa kupitia mfumo
huu Urasimishaji unaweza kuleta maana kwakuwa utakuwa umekubalika na kusimikwa ndani ya
misingi na mihimo ya jamii husika na wala sio Mkakati unaozaliwa kutoka nje ya mipaka ya
jamii husika.
Ndio maana hata utekelezaji wa Mkakati huu wenyewe unakuwa wa kusuasua kutokana na
kutokukubalika na zaidi kutokueleweka miongoni mwa wananchi. Kwa mfano toka mwaka 2005
hadi Juni 2010 ni hatimiliki laki moja na kumi na moja elfu na mia tisa na tano (111,905) pekee
zilitayarishwa, kusajiliwa na kutolewa kwa wananchi katika wilaya mbalimbali nchini.
4
2. Upimaji wa mipaka ya vijiji
Kwa mujibu wa Wizara kwa miaka mitano iliyopita vijiji 5,890 vimepimwa hali inayopelekea
jumla ya vijiji vipatavyo 11,000 kukamilisha upimaji wa mipaka yake.
Katika mojawapo ya malalamiko kwenye vijiji vingi ambavyo Asasi za Kiraia zimefanikiwa
kufanya kazi ni vijiji kutokuwa na vyeti vinavyoainisha na kuonyesha ukubwa wa vijiji vyao.
Vijiji vingi ni kweli inawezekana vimepimwa lakini vyeti vinavyothibitisha upimwaji wake
havijawafikia wananchi wenyewe na kuna usumbufu wa kuvipata kutokana na kupigwa
danadana na Maafisa Ardhi wa Halmashauri za Wilaya. Lakini suala jingine linaloibuka hapa ni
ushirikishwaji wakati wa upimwaji wa vijiji hivi; wananchi wengi wamekuwa wanalalamika
kuwa kumekuwa na ushirikishwaji wa watu wasiokuwa na uelewa na mipaka ya vijiji husika
jambo ambalo limekuwa linapelekea kuibuka kwa migogoro mingi ya ardhi baina ya vijiji
kwenye mipaka; mifano hai ni mingi katika Wilaya za Kilindi, Rufiji, Mkinga na hata
Kilombero. Chanzo cha haya yote ni katika mchakato wa watekelezaji wa kazi hizi kupambana
na asilimia za kiasi gani kazi imetekelezwa pasipo kuwepo na utathimini wa kazi yenyewe kama
kweli ina tija au ni ya kuridhisha viongozi wa ngazi za juu wakati matatizo ya wananchi bado
yakiwa yapo palepale.
3. Kusimamia uanzishwaji wa taasisi za kutoa mikopo kwaajili ya ujenzi na ununuzi wa
nyumba nchini.
Kwa mujibu wa Wizara kumetungwa sheria muhimu sana katika Nyanja hii ambazo ni sheria ya
umiliki wa sehemu ya jengo (Unit Titles Act) 2008 na Sheria ya mikopo ya nyumba ya 2008.
Suala la muhimu hapa ni serikali kuongeza rasilimali kwenye mfuko wa kutoa mikopo kwaajili
ya ujenzi na ununuzi wa nyumba kwa watumishi wa serikali ili uweze kuwanufaisha watumishi
wengi zaidi.
Hoja kubwa miongoni mwa wananchi ni kwanini serikali imeamua kuweka mgawanyo huu baina
ya watumishi wa sekta za umma na wananchi ambao wanategemea sekta zisizo rasmi, waajiriwa
kwenye sekta binafsi pamoja na wananchi wa kawaida kabisa katika suala zima la kuwa na
makazi bora. Ni jambo la kushangaza sana kuona Wizara inaitwa “Wizara ya Ardhi, Nyumba na
Maendeleo ya Makazi” halafu ukiingia ndani yake unakuta uboreshaji wa makazi ya watumishi
kwenye sekta za serikali pekee wakati idadi ya watumishi wa serikali haifikii hata nusu ya
Watanzania wote wenye umri wa wapiga kura.
Wizara inabidi kuweka mkakati wa makusudi kabisa katika kuhakikisha kuwa tabaka ili la
watumishi wa serikali na wananchi wa kawaida linawekwa kando kwa kuhakikisha kuwa kila
Mtanzania ana haki ya kupata makazi bora. Wananchi bado wana fikra nzito ya kuuzwa kwa
nyumba za serikali miaka michache iliyopita lakini bado serikali imeendelea kulifumbia macho
suala hili kwa kuendelea kuwanufaisha watu wachache kupata makazi bora wakati wananchi
wengi wakiendelea kuishi katika nyumba ambazo watendaji wa serikali wenyewe wanapenda
kuziita kwa jina la „mazaga zaga‟. Serikali haina budi kufikisha mpango huu hadi vijijini ili
kuwapa wananchi wote haki sawa katika kufaidika na rasilimali zilizopo.
5
MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA BAJETI YA MWAKA 2009/2010 NA MALENGO YA
MWAKA 2010/2011
4. Ukaguzi na Uhakiki wa Milki
Wizara imezungumzia utatuzi wa migogoro ya Ardhi kwa kutumia njia za utawala kutokana na
wananchi kughushi nyaraka za umilki, ugawaji wa kiwanja kwa zaidi ya mtu mmoja, wamiliki
wa asili kutolipwa fidia, na wananchi wenye miliki halali kushindwa kuendeleza viwanja
walivyomilikishwa kwa wakati.
Utatuzi wa migogoro katika mkondo wa utawala sio jambo baya kwani kwanza ni njia ambayo
inapunguza mlolongo wa mashauri na kesi kujaa katika ngazi za kimahakama kuanzia ngazi ya
baraza la ardhi la vijiji, baraza la kata, baraza la ardhi na nyumba la wilaya na kuendelea. Lakini
suala la kuhoji hapa ni kuwa kumekuwa na mafanikio madogo sana kwenye njia hii kutokana na
kutumika amri zaidi kuliko utambuzi wa tatizo na usuluhishi ambao utaleta usuluhishi usiokuwa
na upendeleo kwa upande mmoja, yaani (win to win situation). Manthalani kwenye migogoro ya
ardhi ya vijiji ambapo viongozi wa ngazi ya kata wale wa kisiasa na kiserikali wamekuwa na
uegemezi wa upande mmoja katika utatuzi wa migogoro hii jambo linalopelekea kuhamasisha
migogoro zaidi kuliko kuimaliza. Lakini jambo jingine la kutambua hapa ni kuwa wale
walisababisha migogoro itokee ndio wanaokuwa wasuluhishaji wa migogoro husika kwahiyo ni
vigumu sana kwa migogoro hiyo kutatulika na kumalizika; mifano mizuri ni maafisa ardhi wa
halmashauri za wilaya na mikoa.
Kwa maana hiyo ni vigumu sana kwa migogoro hii kumalizika katika mfumo wa kiutawala zaidi
ya kuahirisha tatizo kwa kipindi fulani tu. Wizara lazima ihakikishe kuwa mfumo huu
unapotumika kunakuwa na watendaji waadilifu ambao wao wenyewe sio chanzo cha migogoro
hiyo. Lakini kikubwa ni kuhakikisha kuwa elimu ya sheria za ardhi inawafikia wananchi kwa
ukaribu zaidi ili kuepuka nguvu kubwa ambayo viongozi wa kisaisa wanakuwa nayo kwenye
utatuzi wa migogoro ya ardhi wakati kimsingi hawajatajwa kwenye sheria za ardhi.
5. Utwaaji na ubatilishaji wa milki
Kwa mujibu wa Wizara ardhi inapohitajika kwa manufaa ya umma hutwaliwa kwa mujibu wa
sheria ya Utwaaji wa ardhi ya na. 7, 1967. Katika mwaka 2009/2010 milki za wananchi 52
zilitwaliwa na kubatilishwa na mchakato unaendelea katika kuchunguza mashamba mengine
yaliyotelekezwa kwa lengo la kubatilisha umiliki wake.
Ardhi ni mali ya umma na wananchi ndio umma wenyewe lakini kumekuwa na aidha
kutokueleweka kwa maana hii kwa upande wa watendaji wa serikali au kupuuzia kutokana na
kutotilia maanani hayo haswa yanayoitwa maslahi ya umma. Tathimini inaonyesha kuwa kuna
maeneo ya mashamba makubwa ambayo wananchi wanataka serikali ifanye ubatilishaji wa milki
zake ili wananchi wasiokuwa na maeneo waweze kupata maeneo yale kwa kuendeshea shughuli
zao ikiwa ni pamoja na Kilimo, ufugaji na makazi. Kuna mifano mingi kwenye wilaya za
Korogwe, Mkinga na maeneo ya mikoa ya Morogoro, Arusha, Manyara na kwingineko ambako
kuna mashamba makubwa katikati ya maeneo ya wananchi mengine yakiwa hayatumiki,
wananchi wamekuwa wakihangaika ili hati hizo zibatilishwe lakini serikali imekuwa kimya
kwenye eneo hilo. Lakini miliki za wananchi 52 ambao wameshindwa kuendeleza maeneo yao
6
zimekuwa rahisi zaidi kubatilishwa na maeneo hayo Wizara haijatamka wazi yako wapi na baada
ya hati hizo kubatilishwa ni akina nani hasa waligawiwa maeneo hayo au yaliingizwa kwenye
hazina ya ardhi kwa ajili ya uwekezaji.
Kilio kikubwa cha wananchi wengi vijijini ni kubatilishwa kwa hatimiliki za wafanyabisahara
wenye mashamba makubwa waiyoyatumia lakini wamechukulia mikopo benki wakati wananchi
wakiwa wameyazunguka maeneo hayo uku wakisikia kuwa Kilimo Kwanza ndio mkombozi
pekee wa kujitoa katika umaskini. Pia kuna mashamba makubwa yanayohodhiwa na taasisi za
umma kwenye makazi na mashamba ya wananchi yakitumika nusu au kutokutumika kabisa
lakini hakuna ubatilishaji wa hati hizi uliofanyika kwa lengo la kuwapatia wananchi maeneo
haya.
6. Utekelezaji wa Sheria ya Ardhi ya Vijiji
Wizara inazungumzia utekelezaji wa wa sheria ya ardhi ya vijiji Na. 5, 1999 katika wilaya
zilizochaguliwa kutekeleza miradi ya mfano, wilaya za Babati, Bariadi, Namtumbo na Manyoni.
Utekelezaji wa miradi hiyo una lengo la kuhakikisha kuwa mipaka ya vijiji imepimwa na
kupatiwa vyeti vya Ardhi ya Kijiji pamoja na kuandaliwa mipango ya matumizi ya Ardhi, kupima
na kumilikisha mashamba ya wananchi kwa kuwapatia Hati za Hakimiliki ya Kimila.
Kwa mujibu wa Wizara bado utekelezaji wa sheria ya ardhi ya Vijiji uko katika wilaya za mfano,
swali la kujiuliza na kuiuliza wizara, zaidi ya miaka kumi sasa toka sheria hii itungwe bado
utekelezaji wake ni kwenye wilaya za mfano tu? Lini hizi wilaya za mfano zitakamilishiwa zoezi
lake ili utekelezaji huu uchukue kasi yake kutokana na ukweli kuwa uchelewashwaji wa
utekelezwaji wa sheria hii ni mojawapo ya changamoto kubwa sana kwa wananchi katika
kuhakikisha usalama na uhakika wa matumizi na ulinzi wa Ardhi yao dhidi ya wawekezaji
wakubwa ambao uchukua maeneo makubwa sana ya Ardhi ya vijiji.
Jambo jingine la muhimu ambalo wizara ilibidi na bado inatakiwa iuambie umma ni gharama za
utekelezaji wa sheria hii kutokana na ukweli kuwa gharama zinazotumika katika utekelezaji huu
chini ya Usimamizi wa Wizara ni kubwa mno kuliko zile ambazo zinatumika na Asasi nyingine
zikiwepo asasi za Kiraia. Utumiaji huu mkubwa wa gharama umepelekea wilaya chache kutumia
fedha nyingi wakati Wizara ingeweza kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuhakikisha
kuwa utekelezaji huu unafanyika kwa wakati ili kuwahakikishia wananchi usalama wa Ardhi yao
kuliko ilivyo sasa ambapo wananchi wamekuwa wakighilibiwa na kuhadaiwa na wawekezaji na
kugawa Ardhi yote ya kijiji kutokana na kutokutambua ukubwa wa Ardhi waliyonayo.
7. Kwa mujibu wa Wizara kwa mwaka ujao wa fedha wa 2010/2011itasimamia uandaaji na
usajili wa vyeti vya ardhi ya vijiji 5,000; hatimiliki za kimila zipatazo 138,000 katika
vijiji 138 vilivyosalia kwenye wilaya za mfano
Suala la kuhoji hapa ni Wizara kuendelea kulala na kukesha katika wilaya za mfano kwa miaka
kadhaa sasa na uongezwaji wa taratibu sana wa Wilaya nyingine katika mchakato mzima wa
kutekeleza sheria hii. Suala jingine ni kuhusu hivi vijiji 5,000 ambavyo uandaaji na usajili wa
vyeti vya Ardhi utatekelezwa kwa mwaka ujao wa fedha, Wizara angalau ingeweka wazi wilaya
ambazo vijiji hivi vitachukuliwa/chaguliwa isije kuwa bado ni kwenye zile zile wilaya za mfano.
7
Lakini jambo jingine la msingi hapa ambalo wizara haijaligusia ni jinsi gani ambavyo wadau
wengine wanaohusika katika kuendeleza utekelezaji wa sheria hii walivyochukuliwa na
kuthaminiwa na wizara kwa mwaka ujao. Hakuna sehemu ambapo Wizara inatambua mchango
wa Asasi za Kiraia katika utekelezaji wa sheria hii kwa mwaka uliopita. Lakini ni ukweli ulio
dhahiri kuwa mchango wa Asasi hizi ni mkubwa sana katika nyanja hii ya utekelezaji wa sheria
hii jambo ambalo lilihitaji kutambuliwa na serikali ikiwa ni pamoja na kuhainisha ni jinsi gani
ambavyo Wizara imepokea mapendekezo na changamoto mbalimbali kutoka Asasi hizi katika
kuhakikisha kuwa lengo la uhakika wa ulinzi wa Ardhi ya Mtanzania unalindwa na kusimamiwa
kwa dhati kabisa.
8. Viwango vya fidia
Kwa mwaka 2009/10 wizara imefanya utafiti wa gharama za fidia za mazao na ardhi katika jiji
la Dar es Salaam. Kwa mwaka 2010/2011 Wizara itaendelea kufanya utafiti katika katika mikoa
iliyobaki ili kuwa na mwongozo wa viwango vya fidia unaozingatia gharama halisi za soko kwa
lengo la kuboresha viwango vya fidia na kumaliza malalamiko ya wananchi kuhusu suala la
fidia.
Ni ukweli ulio dhahiri kuwa suala la fidia ni tatizo kubwa kwenye sekta ya Ardhi nchini
Tanzania kwa sasa. Na limekuwa na linaendelea kuwa tatizo si tu kutokana na kile Wizara
inachoona kuwa kuna viwango visivyo sahihi vya fidia lakini tatizo kubwa linaloibuka hapa ni
akina nani wanastahili kulipwa fidia pale wanapolazimika kuhama au kuhamishwa kwenye
maeneo yao kwa sababu yoyote ile iwe kwa manufaa ya umma au kwa lengo la kuwapisha
wawekezaji wakubwa wenye mitaji inayotambulika na serikali.
Hoja hii ni ya kufikiriwa sambamba na hiki kinachoitwa utafiti wa viwango vya fidia, wizara
ikitambua hili basi tatizo la msingi hapa litakuwa limetatuliwa. Tuchukue mfano wa wakazi wa
Kwembe nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam na wale wa Namwawala na Mngeta huko
Kilombero Morogoro, utafiti huu wa viwango vya fidia hauna mantiki kwao kwani wao
wanaonekana kuwa sio wastahili wa kulipwa fidia kwani ni wavamizi wa maeneo ambayo
wamekuwa wakiishi na kuendeleza kazi zao za Kilimo na makazi kwa zaidi ya hata miaka
thelathini sasa.
Kwa maana hiyo wizara isjikite tu katika kufanya utafiti wa viwango vya gharama za mazao na
ardhi ambazo kimsingi inaeleweka bayana kuwa zitakuwa zinabadilika mwaka hadi mwaka hata
ikibidi mwezi hadi mwezi kutokana na mabadiliko ya kiuchumi na ukuaji wa miji na vijiji.
Wizara inatakiwa ijikite zaidi katika kufanya utafiti kwanini wananchi wengine wanapata fidia
wakati wengine wanakosa. Na hili iende sambamba na serikali kuhakikisha kuwa maeneo
ambayo yanafahamika kama maeneo ya maendelezo kwa kile kinachoitwa maslahi ya umma
yanatambulika mapema ili kuepuka usumbufu kwa wananchi baada ya kuwa wameshaanzisha
makazi na shughuli nyingine kwani kwa kufanya hivyo kunaathiri sana maisha ya wananchi kwa
kiwango ambacho wakati mwingine hata fidia wanazolipwa zinakuwa zinakuwa hazikidhi yale
ambayo wananchi walikuwa wanayapata kwenye maeneo yao ya asili.
8
9. Kuanzishwa kwa hazina ya Ardhi
Kwa mujibu wa wizara uratibu wa kuanzishwa kwa hazina ya ardhi kwa mwaka 2009/2010
uliendelea kwaajili ya wawekezaji wa ndani na nje ya nchi ikiwa ni pamoja na uwekaji wa
miundombinu ya kiuchumi na kijamii, maendeleo ya miji na utekelezaji wa kauli mbiu ya taifa ya
“Kilimo Kwanza”
Kinachoonekana hapa ni kuwa uanzishwaji wa hazina ya ardhi ni kwa lengo moja kubwa ambalo
ni kuweka ardhi kwaajili ya wawekezaji. Wakati ni ukweli ulio dhahiri kuwa hata katika maeneo
ya Morogoro yaliyotajwa na wizara kuwa kuna mashamba yaliyotelekezwa na wawekezaji kuna
wananchi wengi wa kawaida ambao wanahitaji kupata maeneo hayo ili kuimarisha Kilimo
wanachokifanya kwenye hekari moja. Haina mantiki kwa serikali kuondoa kodi ya pembejeo za
Kilimo halafu bado maeneo mengi na mazuri yenye rutuba yachukuliwe na kupewa wawekezaji
wakubwa wakati hata hawa wananchi wa kawaida wana uwezo wa kutosha tu kugawiwa ardhi
hiyo na kuendeleza Kilimo chnye tija na kukuza pato na uchumi wa nchi.
Lakini kwa mshangao mkubwa hazina ya ardhi hapa inaonekana kuwa mahususi kwa
wawekezaji ambao kimsingi kwa mujibu wa Kituo cha Uwekezaji wananchi wa kawaida
hawawezi kuingia kwenye kundi hili la wawekezaji. Ila kama lengo la serikali ni kuona kuwa
wananchi wake wanafaidika na kauli mbiu yao ya Kilimo Kwanza kwa wananchi wenyewe
kuingia kwenye kulima mashamba makubwa kwa teknolojia rahisi zaidi.
Pia kuna suala la msingi sana la kulitazama kwa jicho la mashaka na maulizo nalo ni kuhusiana
na kile kinachoitwa kutekelezwa kwa maeneo. Hapa inabidi kukumbuka kuwa bado kuna
mkanganyo kwenye tafasiri ya makundi ya ardhi hasa kundi la “Ardhi ya Jumla” kwenye ardhi
ya vijiji. Hii ni kutokana na kuwa kuna uwezekano mkubwa ardhi ya wazalishaji wadogo
wadogo kuingizwa katika ardhi iliyotelekezwa; na hapa kimsingi nazungumzia ardhi hasa
inayotumika na wafugaji amabo kutokana na mfumo wao wa kufuga kutokuwekewa misingi
imara ya kulinda uhakika wao kumiliki wamekuwa wakihamahama kutoka eneo moja kwenda
eneo jingine katika kutafuta malisho na maji kwa mifugo yao katika kipindi fulani jambo ambalo
linaweza kupelekea ardhi yao kujumuishwa katika ardhi telekezwa na hatimaye kutupwa katika
hazina ya ardhi kwaajili ya uwekezaji.
Hili ni angalizo ambalo linaendana sambamba na tahadhari iliyotolewa na wizara kuwa ardhi
itakayoingizwa kwenye hazina ya ardhi itakuwa imeandaliwa mipango ya matumizi ya ardhi
yenye kuzingatia maslahi ya wanavijiji na sharti ipimwe. Angalizo hili la wizara sio jambo geni
kwani kwa baadhi ya watendaji wa serikali wamekuwa wakichukulia maagizo ya viongozi wao
kuwa jambo la kawaida na lisilohitaji ufuatiliaji wa karibu hali inayopelekea usumbufu mkubwa
kwa wananchi.
9
10. Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya
Wizara imeahinisha masuala muhimu kuhusu uzuri na umuhimu wa Mabaraza haya katika
utatuzi wa migogoro ya Ardhi katika kuhakikisha kuwa haki za wananchi zinalindwa na
kusimamiwa kisheria. Wizara pia imeahinisha uanzishwaji wa Mabaraza mapya 39, ukarabati
wa ofisi za Mabaraza ya zamani katika baadhi ya wilaya, uajiri wa watumishi wapya pamoja na
kesi zilizofunguliwa, kuamuliwa na zinazoendelea kushughulikiwa. Pia wizara kwa mwaka
2010/2011 imepanga kuanzisha Mabaraza haya katika wilaya za Nzega, Kilosa, Manyoni na
Ngorongoro.
Kuna hoja kuu mbili za kujadili kuhusiana na Mabaraza haya, hoja ya kwanza ni ufanyaji kazi
wake; ufanyaji kazi wa Mabaraza haya umegubikwa na matatizo mengi kama vile kukosa
watumishi wahusika wa kuweza kuyashughulikia mashauri haya na kumalizika kwa wakati na
kwa ufanisi. Na maswali yanayoibuka hapa ni kuwa kama uanzishwaji wa Mabaraza haya
unakwenda kwa kasi ndogo, Je, kwanini serikali isihakikishe kuwa yale yaliyokwishakuanzishwa
yanatekeleza kazi zake kwa ufanisi ili kupunguza kesi nyingi zinazokatiwa rufaa kwenda
mahakama za juu hali inayopelekea Mabaraza haya kuonekana yasiyokuwa na tija katika utatuzi
wa migogoro ya Ardhi jambo ambalo linaonyesha kutokukidhi kiu na malengo ya kuanzishwa
kwa Mabaraza hayo.
Hoja ya kwanza ndio inayoibua hoja ya pili ambayo ni uhakika wa kuendelea kuishi kwa
Mabaraza haya kutokana na pendekezo la kufutwa kwa Mabaraza haya baada ya kuonekana
kuwa badala ya kupelekea kupunguka kwa migogoro ya Ardhi imekuwa kinyume chake kwa
mashauri mengi kukwama katika ngazi hii kwa muda mrefu jambo ambalo limekuwa ni kikwazo
kwa wananchi wengi kupata haki zao. Wananchi wengi walitegemea kauli ya Wizara kuhusu
mchakato wa kile kilichosikika cha kumaliza muda wa kuishi wa Mabaraza haya lakini kinyume
chake wizara imejikita katika kuanzisha Mabaraza mapya kwenye wilaya mpya, kuongeza idadi
ya vikao kwenye Mabaraza yenye mashauri mengi pamoja na kuongeza posho za wazee, lakini
swali la msingi linabaki pale pale, Je, Mabaraza haya yaliyoongezwa yatapelekea kupunguza
migogoro hii au ni katika harakati tu za kutaka kuendelea kupambana na ongezeko la takwimu
na asilimia kwenye bajeti ijayo?
11. Wizara imetamka kuwa ilipitia upya mfumo wa utatuzi wa migogoro ya ardhi na nyumba
na kuchunguza chanzo cha migogoro ya ardhi kwa lengo la kuimarisha utendaji wa kazi
wa Mabaraza katika ngazi ya Wilaya.
Pamoja Na kuwa hii ilikuwa Ni bajeti wananchi walitegemea Wizara ingeweka bayana
kilichogundulika kuwa chanzo cha migogoro hii Ili wananchi watambue kile kilichofanyiwa
utafiti, au wizara inataka wananchi waendelee kuamini kuwa utafiti ufanywa kwa ushirikiano wa
wananchi lakini majibu ya utafiti hayana sababu ya kuwarudia wananchi. Ingawa ukweli ni kuwa
sababu za kuongezeka migogoro ziko wazi na wala hazihitaji tena utafiti ila kinachotakiwa
kushugulikia visababishi vya migogoro hii kutokuzalisha tena migogoro ya aina ile ile kila mara.
12. Wizara pia imezungumzia kuhusu elimu kwa umma juu ya sheria namba 2 ya mwaka
2002 ya Utatuzi wa Migogoro ya Ardhi kupitia vyombo vya habari, katika maonyesho ya
wakulima na wiki ya utumishi wa umma.
10
Hapa kuna kila sababu ya kujiuliza maswali kuhusu mbinu za utoaji wa elimu hii kwa umma,
ukifuatilia kwa undani elimu ya utatuzi wa migogoro ya ardhi ni elimu ambayo kwa kiasi
kikubwa inahitaji kukutana na wadau wenyewe kwa elimu ya moja kwa moja kutokana na elimu
hii kuhitaji mjadala wa pamoja katika kuelekezana masuala mbalimbali ya muhimu. Wizara
inabidi ijikite zaidi katika kutoa elimu hii kwa wananchi hasa wanavijiji kwa kuwashirikisha
wadau mbalimbali zaidi ili kuvijengea vyombo vya utatuzi wa migogoro ya ardhi kuanzia ngazi
ya kijiji pamoja na wananchi kwa ujumla kwani ni njia muhimu sana katika kupunguza
usumbufu kwa wananchi katika kutafuta haki zao kwenye masuala ya ardhi.
SEHEMU YA PILI
KUAINISHA MAENEO YA VIPAUMBELE VYA BAJETI NA NAMNA MAENEO
HAYO YATAKAVYOFIKIWA NA BAJETI
Katika bajeti ya Wizara kwa mwaka 2010/11 hakuna maeneo mahususi kabisa ambayo Wizara
imeyaainisha kama maeneo ya kuwekewa msisitizo kwaajili ya kutekelezwa kwa uhakika katika
kipindi cha mwaka ujao. Wananchi pamoja na wadau wengine wa masuala ya Ardhi
walitegemea kuwa Wizara katika bajeti hii ingetilia mkazo katika maeneo fulani fulani ili
kumaliza kero kubwa ambazo zinaikumba sekta hii nyeti yenye kutoa mwelekeo na mustakabali
wa maisha ya wananchi na taifa
Kwa mfano suala la mpango bora wa matumizi ya ardhi, ili ni eneo ambalo Wizara pamoja na
kuwa na majukumu mengine lakini ilitakiwa kuhakikisha kuwa eneo hili linapewa nafasi ya
muhimu katika kuikamilisha kazi hii kwa wakati. Kukamilika kwa mpango huu ni njia
mojawapo katika kumaliza migogoro ya Ardhi baina ya makundi ya watumiaji wake. Na mpango
ni muhimu sana hasa kutokana na nchi kuingia katika mikataba ya mpanuko mkubwa wa
kiuchumi kama vile Shirikisho la Afrika Mashariki, ulimaji wa mazao ya kuzalisha mafuta
mbadala (jatropha) ambao kutokana na aina ya baadhi ya watendaji walioko katika serikali ni
wazi kuwa wananchi wengi watapoteza uhakika katika kupata, kutumia na kumiliki ardhi huku
wageni wakiibuka kidedea katika kumiliki mashamba makubwa kwa vigezo vya kuwa
wawekezaji.
Maeneo mengine ni kama vile:-
Utatuzi wa migogoro ya Ardhi kwa kuimarisha vyombo vya utoaji maamuzi haya
kuanzia ngazi ya kijiji na kuendelea ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kuwa wajumbe wa
vyombo hivi wanapata mafunzo pindi wanapochaguliwa sambamba na wananchi
kupewa elimu ya sheria za utatuzi wa migogoro ya Ardhi.
Utekelezaji wa sheria ya ardhi ya vijiji Na. 5, 1999 bado haijapewa kipaumbele katika
kuhakikisha kuwa kweli wanavijiji wanaielewa na kuitumia katika kulinda rasilimali hii
na kutambua wajibu wao katika kusimamia na kulinda haki zao katika Ardhi ya kijiji.
Kumaliza usumbufu katika kulipa wananchi fidia wanapokuwa wamehamishwa kwenye
maeneo yao kwaajili ya kupisha miradi mbalimbali inayoanzishwa na serikali na taasisi
zake pamoja na wawekezaji wakubwa wa ndani na nje ya nchi.
11
Ushirkishwaji wa wananchi na taasisi za Kiraia kwenye utekelezaji wa michakato mbali
mbali katika sekta ya ardhi ni suala la kupewa kipaumbele kutokana na kazi nyingi
kutekelezwa kwa lugha ya “hii ni kazi ya wataalamu” lakini kimsingi ni kazi ambayo
pasipo ushiriki wa karibu wa makundi yote ukamilikaji wake utakuwa wa kusuasua na
husiokuwa na mafanikio ya kujivunia.
Mapendekezo
Ardhi ni nyenzo muhimu sana katika maisha ya mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla kwa
maana nyingine takribani sekta nyingine zote zinategemea Ardhi katika kutekeleza majukumu
yake. Kwa kuangalia dhana hii ya “Ardhi kama uhai” basi ardhi hii inahitaji usimamizi ulio
dhabiti wa kuhakikisha kuwa inatumika kwa usahihi na kwa umakini wa hali ya juu lengo ikiwa
ni kukuza uchumi wa wananchi na taifa kwa ujumla. Kwa maana hiyo kuna kila sababu kwa
serikali na wadau wengine wa Ardhi kuhakikisha kuwa ardhi kubwa iliyoko Tanzania kuliko
nchi nyingine za Afrika Mashariki sio laana ila ni baraka kwa kuhakikisha kuwa inatumika kwa
maslahi ya wote na siyo ya umma ambao kwa maana ya Tanzania sasa sio wote.
Kuna masuala muhimu sana kwa Wizara kama chombo kikuu kilichokabidhiwa mamlaka ya
kuisimamia ardhi ya Tanzania hasa inapofika wakati wa kupanga bajeti ambayo ndio utoa picha
ya jumla ya kazi zitakazotekelezwa kwa mwaka mzima. Masuala hayo ni kama vile:-
i. Elimu ya utambuzi wa sheria mbalimbali za ardhi kwa wananchi na wadau wengine,
ii. Kuviwezesha vyombo vya utatuzi wa migogoro ya Ardhi kwa kuwapatia wajumbe wake
elimu, kuvipatia vitendea kazi, posho na mahitaji mengine,
iii. Kuimarisha ushirikiano baina ya Wizara na Asasi za kiraia katika kuhakikisha kuwa
wananchi wanapatiwa hudumu muhimu zinazohusiana na masuala ya ardhi ili
kuimarisha utambuzi wa wajibu wao katika utumiaji na umiliki wa ardhi,
iv. Wananchi kupewa kipaumbele katika kupata, kutumia na kumiliki ardhi zaidi ya
wawekezaji wakubwa kutoka ndani na nje ya nchi ili kuimarisha mfumo wa
kujitegemea kwa wananchi wenyewe kuliko kusisitiza ajira zitakazotolewa na
wawekezaji ambazo hata hivyo hazina uhakika,
v. Kuweka usimamizi dhabiti wa Ardhi ya nchi dhidi ya wageni ambao wanaingia nchini
kutokana na mwingiliano wa soko la pamoja, na kuendelea kukua kwa uchumi huria.
Hili inabidi kwenda sambamba na kuwawajibisha watendaji ambao watagundulika
kuwauzia au kuwagawia wageni ardhi kinyume cha sheria lakini pia kupitia mianya
yote iliyoko katika sheria za sasa ambazo zinaruhusu wageni kukalia ardhi kwa aina
yoyote ile.
12
HITIMISHO
Ardhi ndio tegemeo la pekee lililobaki kwa Watanzania katika kuendesha maisha ya familia na
kuinua uchumi wa taifa kwa ujumla. Kutokana na umuhimu huu kuna kila sababu kwa serikali
kutambua kuwa Ardhi inalindwa kwa gharama zozote ili iendelee kuwa kiungo muhimu katika
maisha ya Watanzania kama ilivyotunzwa toka vizazi vilivyopita hadi leo hii. Utandawazi,
uwekezaji, soko huria na kadhalika lisiwe chanzo na sababu ya kuimalizia ardhi yote kwenye
mikono ya watu wachache pasipo kuonekana tija ya kufanya hivyo.
Ni wakati sasa wa wananchi kuamka na kurudi katika zama za kujitegemea na kuacha kuota
ndoto za ajira zilizoshikiliwa katika vitanzi vya kibepari na zisizo na uhakika wa kumwondoa
Mtanzania wa kawaida katika lindi la umaskini. Si wakati tena wa Watanzania kuwaza ajira za
kimanamba na za kiuonevu zinazotolewa na wawekezaji wakubwa wawe wa ndani au wan je. Ni
katika mwamko huu serikali itambue kuwa kuna umuhimu wa kuweka msisitizo katika
kuhakikisha kuwa kuna usimamizi dhabiti wa rasilimali ya ardhi na nyinginezo dhidi ya watu
wachche wenye nia ya kujinufaisha wenyewe.
Uchambuzi wa bajeti hii uibue mjadala mzito kwa upande wa wananchi katika kuhakikisha kuwa
serikali inatilia mkazo katika kutekeleza masuala ya muhimu na ya msingi kabisa kwenye sekta
zote muhimu za ardhi, afya, elimu, miundombinu na nyinginezo. Na hili linawezekana kwa
wananchi kuwa na viongozi wenye nia dhabiti ya kujadili matatizo na changamoto zinazolikabili
taifa. Zaidi uchambuzi huu uibue chachu ya wananchi katika kuwachagua wawakilishi bungeni
na kwenye udiwani kwa kutambua matatizo yanayowakabili wananchi kwenye maeneo
mbalimbali nchini.